Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mema na Mabaya: Ushauri Unaoweza Kutusaidia

Mema na Mabaya: Ushauri Unaoweza Kutusaidia

Ushauri wa Biblia umewasaidia mamilioni ya watu katika maeneo haya manne maishani.

1. Ndoa

Watu wana maoni tofauti-tofauti kuhusu ndoa na kile kinachohitajika ili kuwa na ndoa yenye furaha.

BIBLIA INASEMA: “Kila mtu kati yenu anapaswa kumpenda mke wake kama anavyojipenda mwenyewe; kwa upande mwingine, mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.”—Waefeso 5:33.

MAANA: Mungu ndiye mwanzilishi wa ndoa, hivyo yeye anajua kile ambacho wenzi wa ndoa wanahitaji ili kuwa na furaha. (Marko 10:​6-9) Wenzi wa ndoa wanapotanguliza masilahi ya mwenzi wao badala ya kujitanguliza wenyewe, ndoa inakuwa yenye furaha. Mume anayempenda mke wake atamwonyesha upendo huo kwa kumjali na kumtendea vizuri. Naye mke anayemheshimu mume wake ataonyesha heshima hiyo kwa jinsi anavyozungumza na kutenda.

USHAURI WA BIBLIA UNAWEZA KUTUSAIDIA: Quang na Thi, wenzi wa ndoa kutoka Vietnam, walihisi ndoa yao haiwezi kuwa yenye furaha. Quang hakuwa mwenye fadhili. Anasema hivi: “Sikujali hisia za Thi na mara nyingi nilimwaibisha.” Thi alitaka watalikiane. Alisema: “Nilihisi siwezi tena kumwamini au kumheshimu mume wangu.”

Hatimaye, Quang na Thi walijifunza kile ambacho Biblia inafundisha na jinsi ya kutumia Waefeso 5:33 katika ndoa yao. Quang anasema, “Mstari huo ulinisaidia nione umuhimu wa kuwa mwenye fadhili na kumfanya Thi ahisi kwamba ninampenda na niko tayari kumtunza kimwili na kihisia. Ninapofanya hivyo, ananipenda na kuniheshimu zaidi.” Naye Thi anasema, “Kadiri ninavyotumia ushauri ulio kwenye Waefeso 5:33 na kumheshimu mume wangu, ndivyo anavyoendelea kufanya nihisi ananipenda, ananilinda na ninapata amani.”

Ili kupata habari zaidi kuhusu ndoa, soma Amkeni! Na. 2 2018, yenye kichwa “Siri 12 za Mafanikio Katika Familia” kwenye jw.org.

2. Jinsi ya Kuwatendea Wengine

Mara nyingi watu huwatendea wengine vibaya kwa sababu ya rangi yao, taifa, mwonekano, dini, au msimamo wao kuhusu ngono.

BIBLIA INASEMA: “Waheshimuni watu wa namna zote.” —1 Petro 2:17.

MAANA: Biblia haiungi mkono ubaguzi wa rangi na wa kijamii au chuki kuelekea watu wanaofanya ngono za jinsia moja. Badala yake inatutia moyo tuwaheshimu watu wote bila kujali rangi, taifa, au hali yao ya kiuchumi. (Matendo 10:34) Hata ingawa hatukubaliani na mambo ambayo wengine wanaamini au jinsi wanavyotenda, bado tunaweza kuwatendea kwa fadhili na heshima.—Mathayo 7:12.

USHAURI WA BIBLIA UNAWEZA KUTUSAIDIA: Daniel alifundishwa kuwaona watu wa bara la Asia kuwa tishio kwa nchi yake. Alimchukia mtu yeyote mwenye asili ya Asia na mara nyingi aliwatukana hadharani. Daniel anasema, “Nilijiambia sifanyi kosa, ni ‘uzalendo’ tu. Hata sikuwazia kwamba nilikuwa nikifikiri au kutenda kimakosa.”

Baadaye, Daniel alijifunza kile ambacho Biblia inafundisha. Daniel anasema, “Nilihitaji kubadili kabisa njia yangu ya kufikiri. Nilihitaji kuwaona watu kama Mungu anavyowaona, yaani, kwamba sisi sote tuko sawa hata iwe tunatoka wapi.” Daniel anaeleza jinsi anavyohisi sasa anapokutana na watu. Anasema: “Mara nyingi hata sifikirii wanatoka wapi. Sasa ninawapenda watu wote na nina marafiki kutoka sehemu mbalimbali duniani.”

Ili kupata habari zaidi, soma Amkeni! Na. 3 2020, yenye kichwa “Je, Inawezekana Kuushinda Ubaguzi?” kwenye jw.org.

3. Pesa

Watu wengi hufuatilia utajiri ili kuwa na furaha na maisha bora baadaye.

BIBLIA INASEMA: “Hekima ni ulinzi kama pesa zilivyo ulinzi, lakini hii ndiyo faida ya ujuzi: Hekima humhifadhi hai yule aliye nayo.”—Mhubiri 7:12.

MAANA: Tunahitaji pesa, lakini kuwa na pesa hakumaanishi tutakuwa na furaha au maisha mazuri wakati ujao. (Methali 18:11; 23:​4, 5) Badala yake tutapata furaha ya kweli na wakati ujao salama tukitumia hekima ya Mungu inayopatikana katika Biblia.— 1 Timotheo 6:​17-19.

USHAURI WA BIBLIA UNAWEZA KUTUSAIDIA: Cardo, mwanamume kutoka Indonesia, alikuwa akifuatilia sana utajiri. Anasema: “Nilifurahia mambo ambayo kwa wengine ni ndoto tu, nilisafiri, nilinunua vitu vya kifahari, magari, na hata nyumba.” Lakini pesa zake hazikudumu. Cardo anasema: “Nilitapeliwa, na pesa ambazo nilipata kwa jasho zikatoweka ghafla. Nilitumia maisha yangu kufuatilia utajiri, lakini mwishowe nilipoteza kila kitu na nilikata tamaa na kujihisi sifai.”

Cardo alianza kutumia ushauri wa Biblia kuhusu pesa. Hatumii tena nguvu zake zote kufuatilia utajiri bali amechagua kuishi maisha rahisi. Anasema: “Utajiri wa kweli ni wa kiroho. Ninapata usingizi mzuri, na nina furaha ya kweli.”

Ili kujua maoni ya Biblia kuhusu pesa, soma makala “Je, Elimu ya Juu na Pesa Zitakuhakikishia Maisha Bora ya Wakati Ujao?” katika Mnara wa Mlinzi Na. 3 2021, kwenye jw.org.

4. Ngono

Watu wana maoni mbalimbali kuhusu mwenendo wa kingono unaofaa.

BIBLIA INASEMA: “Mjiepushe na uasherati. Kila mmoja wenu anapaswa kujua jinsi ya kuudhibiti mwili wake mwenyewe katika utakatifu na heshima, si kwa hamu yenye pupa ya ngono kama ya watu wa mataifa wasiomjua Mungu.”—1 Wathesalonike 4:​3-5.

MAANA: Kuhusu ngono, Biblia inatuwekea mipaka fulani. Neno “uasherati” linatia ndani uzinzi, ukahaba, ngono kati ya watu ambao hawajafunga ndoa, ngono kati ya watu wa jinsia moja, na ngono na wanyama. (1 Wakorintho 6:​9, 10) Mahusiano ya kingono ni zawadi kutoka kwa Mungu na alikusudia zawadi hiyo iwe kati ya mwanamume na mwanamke waliofunga ndoa tu.— Methali 5:​18, 19.

USHAURI WA BIBLIA UNAWEZA KUTUSAIDIA: Mwanamke anayeishi Australia anayeitwa Kylie alisema: “Nilipokuwa mseja nilihisi kwamba ikiwa ningefanya ngono basi ningehisi kwamba ninapendwa na niko salama. Lakini mambo yalikuwa tofauti. Sikujiamini na nilivunjika moyo.”

Baadaye, Kylie alijifunza mambo ambayo Biblia inasema kuhusu ngono na akayatumia. Anasema, “Ninaona kwamba Mungu ametuwekea viwango ili tusiumie. Ninahisi kwamba ninapendwa na niko salama kwa sababu ya kufanya mambo katika njia ambayo Yehova anataka tufanye. Kufuata ushauri wa Biblia kumenisaidia kuepuka maumivu mengi sana!”

Ili kupata habari zaidi, soma makala yenye kichwa “Biblia Inasema Nini Kuhusu Kuishi Pamoja Bila Kufunga Ndoa?” kwenye jw.org.

Muumba wetu anatusaidia kujua mema na mabaya. Wakati mwingine huenda isiwe rahisi kushikamana na viwango vyake lakini kufanya hivyo kuna faida. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba tukivifuata tutakuwa na furaha ya kudumu.