Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, tunaweza kutegemea hisia zetu zituongoze ifaavyo?

Mema na Mabaya: Mwongozo Unaofuatwa na Wengi

Mema na Mabaya: Mwongozo Unaofuatwa na Wengi

Karibu kila mtu hukubali kwamba matendo fulani ni mema na mengine ni mabaya kabisa. Kwa mfano, watu wengi wanakubali kwamba kuua, kubaka, na kuwatendea watoto vibaya kingono ni mambo yanayochukiza. Kwa upande mwingine, watu wanafurahi wengine wanapotenda kwa haki, fadhili, na kuonyesha hisia-mwenzi. Lakini inapohusu maamuzi mengine maishani kama vile maamuzi kuhusu ngono, unyoofu, na kulea watoto, watu wengine wanaamini kwamba chochote utakachoamua ni sawa, hakuna uamuzi mzuri au mbaya. Maamuzi ya watu wengi yanategemea hisia zao na za wale wanaowazunguka. Je, hiyo ni njia inayotegemeka?

HISIA ZETU

Mara nyingi tunafanya maamuzi tukiongozwa na hisia, au hisi yetu ya ndani ya mema au mabaya, yaani, dhamiri. (Waroma 2:14, 15) Hata watoto wadogo wanaweza kutofautisha matendo ya haki na yasiyo ya haki na pia wanahisi hatia wanapokosea. Kadiri tunavyokua tunajifunza mema na mabaya kutoka kwa watu wa familia yetu, watu wa rika letu, walimu, jamii, dini, na utamaduni wetu. Tunapofanya maamuzi dhamiri yetu inatusaidia kujua ikiwa maamuzi hayo yanapatana na maadili yetu au la.

Hisi yetu ya mema na mabaya inaweza kutuchochea kuonyesha hisia-mwenzi, kuwa wenye shukrani, kutenda kwa haki na kuwaonyesha wengine huruma. Pia inaweza kutuzuia tusifanye mambo yanayoweza kuwaumiza wale tunaowapenda au mambo yanayoweza kutuaibisha au kufanya tuwe na hatia.

Je, tunaweza kutegemea hisia zetu zituongoze ifaavyo? Garrick anasema hivi kuhusu maisha yake alipokuwa kijana, “Nilifanya chochote nilichotaka.” Hata hivyo, aligundua kwamba kufanya kile alichohisi ni sawa, hakukumletea matokeo mazuri. Hatimaye, alikosa furaha kwa sababu aliishi maisha yaliyojaa “ukosefu wa maadili, ulevi, ujeuri, na hata alitumia dawa za kulevya.”

HISIA ZA WENGINE

Mbali na hisia zetu sisi huongozwa pia na maoni ya watu wengine kuhusu maamuzi yetu. Kufanya hivyo hutuwezesha kunufaika na uzoefu na hekima yao. Tunapofanya mambo ambayo familia, marafiki, na jamii huyaona kuwa sawa wao hutuheshimu.

Je, tunaweza kutegemea hisia za wengine zituongoze ifaavyo? Alipokuwa kijana, Priscila alifanya jambo lililokuwa la kawaida kwa vijana wenzake, yaani, alifanya ngono kabla ya ndoa. Hata ingawa wengine waliona yale aliyofanya kuwa sawa, yeye hakuwa na furaha. Alisema: “Kufanya yale ambayo wengine walikuwa wakifanya hakukuniletea furaha. Kulisababisha nifanye mambo ya kipumbavu na hatari.”

JE, KUNA NJIA BORA YA KUFANYA MAAMUZI?

Tunapofanya maamuzi kuhusu mema na mabaya, kuzingatia hisia zetu na za watu wengine kunaweza kutunufaisha. Hata hivyo, njia hiyo pekee haitoshi kutuongoza kwenye matokeo mazuri. Tunaweza kujiumiza au kuwaumiza wengine kwa sababu huenda tusielewe vizuri matokeo ya maamuzi yetu. (Methali 14:12) Hata ingawa huenda sisi na wengine tukafikiri kwamba jambo fulani ni sawa, bado jambo hilo linaweza kuwa lenye kudhuru na huenda pia tukahitaji kubadili maoni hayo. Kwa mfano, tabia ambazo pindi fulani zilionekana kuwa hazifai, sasa zinakubalika na matendo ambayo hayakukubalika, sasa yanaonekana kuwa yanafaa.

Je, tunaweza kutegemea hisia za wengine zituongoze ifaavyo?

Je, kuna njia bora zaidi ya kuamua lililo jema au baya? Je, kuna viwango vya maadili tunavyoweza kufuata leo ambavyo havitatufanya tujute baadaye?

Tunafurahi kujua kwamba kuna chanzo kinachotegemeka cha mwongozo na ambacho kinawanufaisha wote wanaokitumia. Makala inayofuata itazungumzia mahali tunapoweza kupata mwongozo wenye kutegemeka utakaotusaidia kuamua mema na mabaya.