Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watoto Wanavyoweza Kukabiliana na Huzuni

Watoto Wanavyoweza Kukabiliana na Huzuni

Je, unaomboleza kifo cha mshiriki wa familia yenu? Ikiwa ndivyo, unaweza kukabiliana jinsi gani na hali hiyo? Hebu chunguza jinsi ambavyo Biblia iliwasaidia vijana watatu kupambana na hali hiyo ngumu.

SIMULIZI LA DAMI

Dami

Mwanzoni, tulifikiri kwamba baba anahisi maumivu ya kawaida ya kichwa. Hata hivyo, maumivu yalipozidi, mama alipiga simu na kuomba gari la kubebea wagonjwa. Bado ninakumbuka jinsi madaktari walivyombeba na kuondoka naye. Sikujua kwamba hiyo ndio ilikuwa mara ya mwisho kumwona baba akiwa hai. Siku tatu baadaye, baba alikufa kwa sababu ya kutanuka kwa mshipa wa damu. Wakati huo nilikuwa na umri wa miaka sita.

Kwa miaka mingi, nilijilaumu kwa sababu ya kifo cha baba. Akilini, nilikumbuka tena na tena madaktari wakimbeba, na huwa ninajiuliza hivi: Kwa nini nilibaki tu nimesimama? Kwa nini sikufanya jambo lolote kumsaidia baba? Niliwatazama wazee walio na matatizo ya afya na kujiuliza, Kwa nini wao wako hai wakati baba amekufa? Baada ya muda, mama alinisaidia niweze kujieleza kuhusu hisia zangu. Na kwa kuwa sisi ni Mashahidi wa Yehova, tulisaidiwa sana na waamini wenzetu.

Baadhi ya watu hufikiri kwamba mtu huwa na huzuni wakati wa msiba tu na kisha anatulia, lakini haikuwa hivyo kwangu. Sikuhuzunika sana baada ya kifo cha baba, lakini mwanzoni mwa miaka yangu ya utineja mambo yalibadilika.

Ushauri ambao mimi ninawapa vijana waliofiwa na mzazi ni: “Zungumza na mtu kuhusu hali unayokabili. Unapoeleza hisia na mahangaiko yako mapema hilo litakusaidia kuwa na amani ya akili.

Kwa kweli, ni vigumu kufanya matukio muhimu maishani bila baba kuwepo. Hata hivyo, ninapata faraja ninaposoma ahadi ya Biblia katika andiko la Ufunuo 21:4 linalosema kwamba, hivi karibuni, Mungu “atafuta kila chozi kutoka katika macho [yetu], na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”

SIMULIZI LA DERRICK

Derrick

Ninakumbuka vizuri pindi ambazo tulivua samaki na kupiga kambi milimani pamoja na baba. Baba alipenda sana kwenda milimani.

Baba alikuwa na matatizo ya moyo kwa kipindi fulani. Ninakumbuka nikimtembelea hospitalini mara mbili au tatu nilipokuwa mtoto. Hata hivyo, sikujua kwamba alikuwa mgonjwa sana. Baba alikufa kutokana na ugonjwa wa moyo nilipokuwa na umri wa miaka tisa.

Baba alipokufa, nililia sana. Nilihisi nimeishiwa nguvu na sikutaka kuzungumza na yeyote. Sikuwahi hisi uchungu kama huo maishani mwangu, na sikuwa na hamu ya kufanya chochote. Vijana nilioshirikiana nao kanisani walinifariji kwa muda lakini baadaye wakaniacha. Watu walisema mambo tofauti-tofauti kuhusu kifo cha baba kama vile, “Muda wake ulikuwa umefika” au “Mungu amemchukua” au “Yuko mbinguni sasa.” Majibu hayo hayakuniridhisha, lakini sikujua Biblia inafundisha nini kuhusu mambo hayo.

Kisha, mama alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, na baadaye mimi na kaka yangu tulijiunga naye. Tulijifunza kuhusu hali ya wafu na vilevile ahadi ya Mungu yenye kufariji ya ufufuo. (Yohana 5:28, 29) Lakini andiko lililonifariji zaidi ni Isaya 41:10. Katika andiko hilo Mungu anasema hivi: “Usiogope, kwa maana mimi nipo pamoja nawe. Usitazame huku na huku, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu. Nitakusaidia kwelikweli.” Kujua kwamba Yehova alikuwa pamoja nami, kulinifariji sana katika kipindi hicho kigumu na bado jambo hilo linanifariji.

SIMULIZI LA JEANNIE

Jeannie

Nilipokuwa na umri wa miaka saba, mama alikufa kutokana na kansa. Mambo yote yaliyotendeka siku hiyo yalikuwa kama ndoto. Ninakumbuka kwamba alifia nyumbani na kwamba babu na bibi (nyanya) walikuwepo. Kila mtu alikuwa ametulia. Tulikula mayai usiku huo. Nilihisi kana kwamba maisha yangu yalikuwa yakibadilika kabisa, kwa mwendo wa taratibu.

Wakati huo na hata kwa miaka kadhaa baadaye, nilifikiri kwamba nilipaswa kuwa imara ili nimfariji mdogo wangu, hivyo nilizuia hisia zangu. Hadi leo, mimi huficha mambo yanayoumiza, ingawa jambo hilo halifai.

Ninakumbuka upendo na msaada tuliopata kutoka kwa kutaniko la Mashahidi wa Yehova tunaloshirikiana nalo. Ingawa bado tulikuwa wapya kwenye Jumba hilo la Ufalme, waamini wenzetu walitutendea kana kwamba tulifahamiana kwa miaka mingi. Kwa karibu mwaka mzima, nafikiri baba hakuhitaji kupika chakula cha usiku kwa sababu kililetwa kila siku.

Andiko ninalopenda zaidi ni Zaburi 25:16, 17. Mtunga Zaburi alimsihi Yehova hivi: “Unielekezee uso wako, na unionyeshe kibali; kwa maana mimi niko peke yangu nami ni mwenye kuteseka. Taabu za moyo wangu zimeongezeka; uniondoe katika mikazo iliyo juu yangu.” Ninafarijika sana kujua kwamba kuna mtu aliye tayari kunisaidia ninapokuwa na huzuni. Mungu yuko tayari kukufariji. Biblia imenisaidia kusonga mbele na kukazia fikira mambo mazuri, kama vile ahadi ya Biblia ya ufufuo. Nina tumaini la kumwona mama tena akiwa na afya nzuri katika paradiso duniani.—2 Petro 3:13.

Je, ungependa kujifunza mengi zaidi kuhusu ujumbe wa Biblia wenye kufariji kwa wale wanaokabiliana na huzuni? Pakua bila malipo chapisho lenye kichwa, “Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa.” Tembelea tovuti ya www.pr418.com/sw, tafuta kwenye MACHAPISHO > VITABU NA BROSHUA.