Hamia kwenye habari

Mtaala wa Kujifunza Biblia Unaotolewa na Mashahidi wa Yehova Ni Nini?

Mtaala wa Kujifunza Biblia Unaotolewa na Mashahidi wa Yehova Ni Nini?

 Ni nini hutendeka kwenye funzo la Biblia?

 Mwalimu wako atakusaidia kuielewa Biblia, habari moja baada ya nyingine. Ukitumia masomo ya kujifunzia Biblia ya Furahia Maisha Milele! utajifunza hatua kwa hatua ujumbe wa Biblia kutia ndani jinsi unavyoweza kukusaidia. Ili ujifunze mengi zaidi, tazama video hii.

 Je, ninapaswa kulipia funzo hilo?

 Hapana. Mashahidi wa Yehova wanafuata mwongozo huu ambao Yesu aliwapa wanafunzi wake: “Mlipokea bure, toeni bure.” (Mathayo 10:8) Isitoshe, huhitaji kulipa ili kupata vifaa vitakavyotumiwa, yaani, Biblia na chapisho lenye kichwa Furahia Maisha Milele!

 Mtaala ni mrefu kadiri gani?

 Mtaala wote una masomo 60. Wewe ndiye utakayeamua utashughulikia masomo hayo kwa muda gani, lakini wanafunzi wengi hupenda kumaliza somo moja kwa juma.

 Nitaanzaje?

  1.  1. Jaza fomu mtandaoni. Tutatumia habari za kibinafsi unazojaza ili tu kupanga mtu atakayewasiliana nawe kama ulivyoomba.

  2.  2. Mwalimu atawasiliana nawe. Mwalimu wako atakueleza ni mambo gani unayoweza kutarajia katika mtaala huu wa kujifunza Biblia naye atajibu maswali yoyote ambayo huenda ukawa nayo.

  3.  3. Wewe na mwalimu wako mtafanya mipango. Mnaweza kukutana kihalisi ili kujifunza au mnaweza kujifunza kupitia simu, mtandao, barua, au barua-pepe. Vipindi vya kujifunza huwa na urefu wa saa moja hivi, lakini vinaweza kuwa vifupi au virefu zaidi ikitegemea ratiba yako.

 Je, ninaweza kufanya majaribio ya kipindi kimoja cha funzo?

 Ndiyo. Ili kufanya hivyo, jaza fomu mtandaoni. Mwalimu anapowasiliana nawe, mjulishe kwamba ungependa kujaribu kipindi kimoja cha funzo ili uone ikiwa utafurahia. Atatumia broshua Furahia Maisha Milele! ambayo ina masomo matatu ya kwanza, ili kukusaidia kuona ikiwa utafurahia somo hilo.

 Nikikubali kujifunza Biblia, je, nitashinikizwa kuwa Shahidi wa Yehova?

 Hapana. Mashahidi wa Yehova wanapenda kuwafundisha watu kuhusu Biblia, lakini hatuwashinikizi watu kujiunga na dini yetu. Badala yake, tunafundisha kwa heshima kile ambacho Biblia inasema, tukitambua kwamba kila mtu ana haki ya kuchagua kile ambacho yeye ataamini.—1 Petro 3:15.

 Je, ninaweza kutumia Biblia yangu binafsi?

 Ndiyo, unaweza kutumia tafsiri yoyote ya Biblia unayotaka. Ingawa tunapenda kutumia Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kwa sababu ni tafsiri sahihi na inayosema mambo wazi, tunatambua kwamba watu wengi wanapenda kutumia tafsiri ambayo wao wamezoea.

 Je, ninaweza kuwaalika wengine wajiunge nami katika funzo langu?

 Ndiyo. Unaweza kualika familia yako yote au marafiki ambao unachagua.

 Namna gani ikiwa nilijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova wakati uliopita? Ninaweza kujifunza tena?

 Ndiyo. Kwa kweli, huenda ukafurahia hata zaidi mtaala wa sasa wa kujifunza kwa sababu umeboreshwa ili upatane na mahitaji ya watu leo. Inatumia picha na video nyingi zaidi na kuna nafasi nyingi zaidi za kuwa na mazungumzo kuliko ilivyokuwa katika programu zetu za awali za kujifunzia Biblia.

 Je, kuna njia ya kujifunza Biblia bila kuwa na mwalimu?

 Ndiyo. Ingawa wanafunzi wengi hujifunza vizuri zaidi wakisaidiwa na mwalimu, kuna baadhi wanaopenda kujifunza wakiwa peke yao kwanza. Ukurasa wetu wa Vifaa vya Kujifunzia Biblia una orodha ya vifaa ambavyo vinaweza kukusaidia kujifunza Biblia bila malipo. Huenda ukafaidika na vifaa vifuatavyo:

  •   Masomo ya Biblia Kwenye Mtandao. Masomo hayo yanajibu maswali muhimu zaidi maishani, kama vile: Mungu ni nani? Kwa nini kuna mateso na uovu? Je, Mungu atakomesha mateso?

  •   Video za Biblia. Video hizo fupi zinaeleza mafundisho muhimu ya Biblia.

  •   Maswali ya Biblia Yajibiwa. Makala hizi zinatoa majibu ya maswali mengi sana ya Biblia.

  •   Mistari ya Biblia Yafafanuliwa. Jifunze maana ya mistari na maneno ya Biblia yanayojulikana sana.