Hamia kwenye habari

Je, Kuna Mtu Ambaye Amewahi Kumwona Mungu?

Je, Kuna Mtu Ambaye Amewahi Kumwona Mungu?

Jibu la Biblia

 Hakuna mwanadamu ambaye amewahi kumwona Mungu kihalisi. (Kutoka 33:20; Yohana 1:​18; 1 Yohana 4:​12) Biblia inasema kwamba “Mungu ni Roho.” Roho ni aina ya uhai ambao hauwezi kuonekana kwa macho ya mwanadamu.​—Yohana 4:​24; 1 Timotheo 1:​17.

 Hata hivyo, malaika wanaweza kumwona Mungu moja kwa moja, kwa sababu wao ni viumbe wa roho. (Mathayo 18:10) Isitoshe, kuna wanadamu fulani watakaofufuliwa wakaishi mbinguni wakiwa na miili ya roho nao pia watapata fursa ya kumwona Mungu wakati huo.​—Wafilipi 3:​20, 21; 1 Yohana 3:2.

Jinsi unavyoweza “kumwona” Mungu leo

 Mara nyingi, Biblia inapotaja kuhusu kuona, inahusianisha wazo hilo na uelewaji. (Isaya 6:​10; Yeremia 5:​21; Yohana 9:​39-​41) Basi kwa kuzingatia maana hiyo, mtu anaweza kumwona Mungu leo kwa “macho ya moyo” wake kwa kuwa na imani itakayomwezesha Kumjua na kuthamini sifa Zake. (Waefeso 1:​18) Biblia inaeleza hatua ambazo tunapaswa kuchukua ili tujenge imani ya aina hiyo:

  •   Jifunze kuhusu sifa za Mungu, kama vile upendo na ukarimu wake, kutia ndani hekima na nguvu zake, kupitia vitu alivyoumba. (Waroma 1:​20) Baada ya kukumbushwa kuhusu kazi za Mungu za uumbaji, yule mwanamume mwaminifu Ayubu alihisi ni kana kwamba Mungu alikuwa amesimama mbele yake.​—Ayubu 42:5.

  •   Mjue Mungu kwa kujifunza Biblia. Biblia inatuhakikishia hivi: “Ukimtafuta [Mungu], ataacha umpate.”​—1 Mambo ya Nyakati 28:9; Zaburi 119:2; Yohana 17:3.

  •   Jifunze kumhusu Mungu kupitia maisha ya Yesu. Kwa kuwa Yesu aliiga kikamilifu utu wa Baba yake, Yehova Mungu, angeweza kusema hivi: “Yule ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.”​—Yohana 14:9.

  •   Ishi kwa njia inayompendeza Mungu, na ujionee jinsi anavyotenda kwa niaba yako. Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale walio safi moyoni, kwa kuwa watamwona Mungu.” Kama ilivyotajwa mwanzoni, baadhi ya wale wanaoishi kwa njia inayompendeza Mungu, watafufuliwa waishi mbinguni na basi wao “watamwona Mungu” wakiwa huko.​—Mathayo 5:8; Zaburi 11:7.

Kwani Musa, Abrahamu, na wengine hawakumwona Mungu kihalisi?

 Katika masimulizi ambayo huenda ikadhaniwa kwamba Biblia inasema wanadamu walimwona Mungu kihalisi, muktadha unaonyesha kwamba Mungu alikuwa akiwakilishwa na malaika au alimtokea mtu katika maono.

 Malaika.

Katika nyakati za kale, Mungu aliwatuma malaika waonekane na wanadamu na waseme kwa niaba yake. (Zaburi 103:20) Kwa mfano, wakati fulani Mungu alizungumza na Musa kutoka kwenye mti uliokuwa ukiwaka moto, na Biblia inasema kwamba ‘Musa aliuficha uso wake, kwa sababu aliogopa kumtazama Mungu wa kweli.’ (Kutoka 3:​4, 6) Hata hivyo, Musa hakumwona Mungu kihalisi, kwa kuwa muktadha unaonyesha kwamba alimwona “malaika wa Yehova.”​—Kutoka 3:2.

 Vivyo hivyo, Biblia inaposema kwamba Mungu ‘alisema na Musa uso kwa uso,’ inamaanisha kwamba Mungu alizungumza na Musa kwa undani na kwa kina. (Kutoka 4:​10, 11; 33:11) Musa hakuuona uso wa Mungu, kwa kuwa habari ambayo alipata kutoka kwa Mungu “ilipitishwa kupitia malaika.” (Wagalatia 3:​19; Matendo 7:​53) Licha ya hilo, Musa alikuwa na imani yenye nguvu katika Mungu hivi kwamba Biblia inamfafanua kuwa ‘mtu aliyemwona Yeye asiyeonekana.’​—Waebrania 11:27.

 Mungu pia alizungumza na Abrahamu kwa njia ileile aliyozungumza na Musa, yaani, kupitia malaika. Kwa kweli, mtu anaposoma Biblia kijuujuu tu huenda akafikiri kwamba Abrahamu alimwona Mungu kihalisi. (Mwanzo 18:​1, 33) Hata hivyo, muktadha unaonyesha kwamba wale “wanaume watatu” waliomtembelea Abrahamu walikuwa malaika waliotumwa na Mungu. Abrahamu aliwatambua kuwa wawakilishi wa Mungu na akazungumza nao kana kwamba alikuwa akizungumza na Yehova moja kwa moja.​—Mwanzo 18:​2, 3, 22, 32; 19:1.

 Maono.

Pia Mungu amewatokea wanadamu kupitia maono, au matukio fulani yanayojitokeza katika akili ya mtu. Kwa mfano, Biblia inaposema kwamba Musa na Waisraeli wengine ‘walimwona Mungu wa Israeli,’ inamaanisha kwamba “walipata maono ya Mungu wa kweli.” (Kutoka 24:​9-​11) Hata nyakati nyingine Biblia inasema kwamba manabii ‘walimwona Yehova.’ (Isaya 6:1; Danieli 7:9; Amosi 9:1) Katika kila kisa, muktadha unaonyesha kwamba walipata maono ya Mungu na si kwamba walimwona moja kwa moja.​—Isaya 1:1; Danieli 7:2; Amosi 1:1.