Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU

Ukweli Kuhusu Simulizi la Uumbaji

Ukweli Kuhusu Simulizi la Uumbaji

MABILIONI ya watu wamesoma au kusikia simulizi la Biblia kuhusu mwanzo wa ulimwengu. Simulizi hilo lililoandikwa miaka 3,500 iliyopita linaanza kwa maneno haya: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.”

Hata hivyo, watu wengi hawajui kwamba viongozi wa dini, kutia ndani watu wenye imani kali na wanauumbaji wamegeuza simulizi la Biblia kuhusu uumbaji na kupotosha yale ambayo Biblia inasema. Ufafanuzi wao haupatani na sayansi. Ingawa mambo wanayosema hayako katika Biblia, yamewafanya watu wengi wapuuze simulizi la Biblia

na kuliona kama hadithi ya kutungwa tu.

Watu wengi hawajui simulizi halisi la Biblia. Hilo linasikitisha,

kwa kuwa Biblia inafafanua mwanzo wa ulimwengu kwa njia inayopatana na akili. Isitoshe, ufafanuzi huo unapatana na uvumbuzi wa kisayansi. Naam, huenda ukashangaa kujua ukweli wa simulizi la Biblia kuhusu uumbaji!

MUUMBA ASIYE NA MWANZO

Simulizi la Biblia kuhusu uumbaji linategemea uhakika wa kwamba kuna Mungu Mweza-Yote, ambaye aliumba vitu vyote. Yeye ni nani, na ana utu gani? Biblia inafunua kwamba yuko tofauti sana na miungu inayoabudiwa katika jamii nyingi na katika dini zenye wafuasi wengi. Yeye ndiye Muumba wa vitu vyote, lakini watu wengi hawajui mengi kumhusu.

  • Mungu ana utu. Yeye si nguvu isiyo na utu inayoelea kotekote ulimwenguni. Ana mawazo, hisia, na makusudi.

  • Mungu ana nguvu nyingi na hekima isiyo na kifani. Hilo linaonyesha ni kwa nini kuna ubuni wa hali ya juu katika uumbaji wote, hasa viumbe vyenye uhai.

  • Mungu aliumba vitu vyote vyenye mwili. Hivyo, yeye hana mwili kama wa vitu alivyoviumba. Badala yake, yeye ni roho, hawezi kuonekana.

  • Mungu hana mwanzo. Amekuwepo sikuzote na ataendelea kuwepo milele. Kwa hiyo, yeye hakuumbwa.

  • Mungu ana jina lake ambalo linapatikana mara nyingi sana katika Biblia. Jina hilo ni Yehova.

  • Yehova Mungu anawapenda na kuwajali wanadamu.

 MUNGU ALITUMIA MUDA GANI KUUMBA ULIMWENGU?

Biblia inasema kwamba Mungu aliumba “mbingu na dunia.” Maneno hayo yenye maana pana hayataji kipindi kilichohusika kuumba ulimwengu wote au njia iliyotumiwa kuutokeza. Namna gani madai ya wanauumbaji wanaosema kwamba Mungu aliumba ulimwengu kwa siku sita zenye urefu wa saa 24 kila moja? Wazo hilo linalopingwa vikali na wanasayansi linategemea ufafanuzi usio sahihi kuhusu simulizi hilo la Biblia. Acheni tuchunguze yale ambayo Biblia inasema.

Biblia haiungi mkono watu wenye imani kali wala wanauumbaji wanaodai kwamba dunia iliumbwa kwa siku sita zenye urefu wa saa 24 kila moja

  • Biblia haiungi mkono watu wenye imani kali wala wanauumbaji wanaodai kwamba dunia iliumbwa kwa siku sita zenye urefu wa saa 24 kila moja.

  • Mara nyingi, Biblia hutumia neno “siku” kumaanisha vipindi mbalimbali vya wakati. Nyakati nyingine vipindi hivyo havina urefu hususa. Mfano mmoja ni simulizi la uumbaji lililo kwenye kitabu cha Mwanzo.

  • Katika simulizi la Biblia, inawezekana kwamba kila siku ya uumbaji ilikuwa na urefu wa maelfu ya miaka.

  • Kabla ya siku ya kwanza ya uumbaji, tayari Mungu alikuwa ameumba ulimwengu, kutia ndani Dunia isiyo na uhai.

  • Ni wazi kwamba zile siku sita za uumbaji zilikuwa vipindi virefu vya wakati ambapo Yehova Mungu alitayarisha dunia ili ikaliwe na wanadamu.

  • Masimulizi ya Biblia ya uumbaji hayapingani na sayansi kuhusu kipindi ambacho ulimwengu umekuwepo.

JE, MUNGU ALITUMIA MAGEUZI?

Watu wengi wasioamini Biblia wanadai kwamba viumbe vyote vilitokana na kemikali zisizo na uhai bila kuumbwa na mtu yeyote. Wanadai kwamba bakteria fulani inayojifanyiza upya iligeuka hatua kwa hatua na kutokeza jamii zote za viumbe tunazoona leo. Hilo linamaanisha kwamba mwanadamu ambaye amefanyizwa kwa njia ya kustaajabisha alitokana na bakteria.

Watu fulani wanaokubali kwamba Biblia ni Neno la Mungu, wanaamini pia fundisho la mageuzi. Wanadai kwamba Mungu alitokeza kiumbe cha kwanza duniani kisha akakiongoza katika hatua za mageuzi. Lakini Biblia haisemi hivyo.

Masimulizi ya uumbaji yanapatana na utafiti wa kisayansi unaoonyesha kwamba jamii moja inaweza kutokeza viumbe vya aina mbalimbali

  • Kulingana na Biblia Yehova Mungu ndiye aliyeumba aina zote za mimea na wanyama, kutia ndani wanadamu wakamilifu waliokuwa na uwezo wa kujielewa na kuonyesha sifa kama upendo, hekima, na haki.

  • Bila shaka, jamii za wanyama na mimea iliyoumbwa na Mungu zimebadilika na kutokeza aina nyingine mbalimbali. Mara nyingi, aina mpya zinazotokezwa hazifanani.

  • Masimulizi ya uumbaji yanapatana na utafiti wa kisayansi unaoonyesha kwamba jamii moja inaweza kutokeza viumbe vya aina mbalimbali.

 UUMBAJI UNAFUNUA KWAMBA KUNA MUUMBA

Katika miaka ya 1800, mwanabiolojia Mwingereza Alfred Russel Wallace alikubaliana na Charles Darwin kuhusiana na nadharia ya mageuzi ya uteuzi wa kiasili. Ingawa hivyo, mwanamageuzi huyo alisema: “Watu wanaoona kwa macho na wanaotumia akili kufikiri, wameona kwamba katika chembe ndogo zaidi, katika damu, katika dunia yote, na katika ulimwengu wote wa nyota . . . , kuna mtu mwenye akili anayeongoza mambo, yaani kuna Muumba.”

Karibu miaka 2,000 kabla ya Wallace, tayari Biblia ilikuwa imesema hivi: “Kwa maana sifa [za Mungu] ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu.” (Waroma 1:20) Mara kwa mara, ni vizuri kutumia muda fulani kutafakari maajabu ya uumbaji—kuanzia unyasi mdogo mpaka mbingu zenye nyota. Kwa kuchunguza uumbaji unaweza kuona kwamba kuna Muumba.

Lakini huenda ukajiuliza, ‘Kama kuna Mungu mwenye upendo aliyeumba vitu vyote, kwa nini anaacha watu wateseke? Je, kweli anajali viumbe vyake? Itakuwaje wakati ujao?’ Biblia inafunua ukweli kuhusu masimulizi mengine mengi ambayo yamefichwa na hekaya za wanadamu na mafundisho ya kidini. Wachapishaji wa gazeti hili, Mashahidi wa Yehova, watafurahi kukusaidia ujifunze ukweli wa Biblia na mengi kumhusu Muumba na kuhusu wakati wetu ujao.