Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unaweza Kumwona Mungu Asiyeonekana?

Je, Unaweza Kumwona Mungu Asiyeonekana?

“MUNGU ni Roho,” na wanadamu hawawezi kumwona. (Yohana 4:24) Hata hivyo, Biblia inataja watu ambao walimwona Mungu kwa njia fulani. (Waebrania 11:27) Hilo linawezekanaje? Je, kweli unaweza kumwona “Mungu asiyeonekana”?Wakolosai 1:15.

Linganisha hali yetu na ya mtu aliyezaliwa kipofu. Je, upofu wake unamzuia kabisa kuelewa mambo yanayomzunguka? La hasha. Mtu aliye kipofu hupata habari kupitia njia mbalimbali zinazomwezesha kutambua watu, vitu, na shughuli zilizo karibu naye. Mwanamume mmoja kipofu alisema hivi: “Mtu haoni tu kwa macho. Akili inahusika pia.”

Vivyo hivyo, ingawa huwezi kumwona Mungu kwa macho halisi, unaweza kutumia “macho ya moyo” wako kumwona. (Waefeso 1:18) Hebu chunguza njia tatu za kufanya hivyo.

SIFA ZA MUNGU “ZINAONEKANA WAZIWAZI TANGU KUUMBWA KWA ULIMWENGU”

Kwa kawaida, kipofu huwa na uwezo mkubwa zaidi wa kusikia na kugusa ambao humsaidia kuelewa vitu asivyoweza kuona. Vivyo hivyo, unaweza kutumia hisi zako kuchunguza ulimwengu unaokuzunguka na kumwelewa Mungu asiyeonekana ambaye ni Muumba. “Sifa zake ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa.”Waroma 1:20.

Kwa mfano, fikiria makao yetu. Dunia imebuniwa kwa njia ya pekee ili tufurahie maisha bila shida. Tunapopigwa na upepo mtulivu, tunapoota jua, tunapoonja tunda tamu, au kusikia wimbo wenye kutuliza wa ndege, tunafurahia. Je, zawadi hizo hazionyeshi jinsi Muumba wetu alivyo mwenye ufikirio, mwenye kujali, na mkarimu?

Unaweza kujifunza nini kumhusu Mungu kutokana na yale unayoona katika ulimwengu? Jambo moja ni kwamba mbingu hufunua nguvu za Mungu. Utafiti wa kisayansi unaonyesha ulimwengu unapanuka, na isitoshe unapanuka kwa kasi sana! Unapotazama angani usiku, jiulize: Ni nini chanzo cha nguvu hizo zinazofanya ulimwengu upanuke kwa kasi hivyo? Biblia inatuambia kuwa Muumba ana “wingi wa nguvu zenye msukumo.” (Isaya 40:26) Uumbaji wa Mungu unatuonyesha kwamba ndiye “Mweza-Yote”—ambaye “ameinuliwa katika nguvu.”Ayubu 37:23.

‘YULE AMBAYE AMEELEZA JUU YAKE’

Mama mmoja mwenye watoto wawili walio na matatizo ya kuona anasema: “Mazungumzo ni mojawapo ya njia muhimu zaidi ambazo watoto wangu hutumia kujifunza. Waambie kila kitu unachoona na kusikia, [na] uwe tayari kuendelea kueleza unachoona. Wewe ndiye macho yao.” Vivyo hivyo, ingawa “hakuna mwanadamu ambaye amemwona Mungu wakati wowote,” Mwana wa Mungu, Yesu, “aliye kifuani pa Baba, ndiye ambaye ameeleza juu yake.” (Yohana 1:18) Akiwa kiumbe wa kwanza na Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu, Yesu alikuwa “macho” yetu ili tuone mbinguni. Yeye ndiye chanzo bora zaidi cha habari kumhusu Mungu asiyeonekana.

Hebu ona mambo kadhaa ambayo Yesu aliyeishi miaka mingi sana pamoja na Baba yake, alieleza kumhusu Mungu:

  • Mungu hufanya kazi kwa bidii. “Baba yangu anaendelea kufanya kazi mpaka sasa.”Yohana 5:17.

  • Mungu anajua mahitaji yetu. “Baba yenu anajua ni vitu gani mnavyohitaji hata kabla hamjamwomba.”Mathayo 6:8.

  • Kwa rehema Mungu hutuandalia mahitaji yetu. “Baba yenu aliye mbinguni . . . hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.”Mathayo 5:45.

  • Mungu anamthamini kila mtu binafsi. “Je, shomoro wawili hawauzwi kwa sarafu ya thamani ndogo? Na bado hakuna hata mmoja wao atakayeanguka chini bila Baba yenu kujua. Lakini nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote. Kwa hiyo msiogope: Ninyi ni bora kuliko shomoro wengi.”Mathayo 10:29-31.

MWANADAMU ALIYEONYESHA SIFA ZA MUNGU ASIYEONEKANA

Kwa kawaida, vipofu huelewa mambo kwa njia tofauti na watu wenye uwezo wa kuona. Kipofu anaelewa kivuli si kama mahali penye giza, bali kama mahali penye ubaridi pasipo na joto la jua. Kama vile tu kipofu asivyoweza kuona kivuli wala mwangaza wa jua, sisi pia hatuwezi kumwelewa Yehova bila msaada. Hivyo, Yehova alimtoa mwanadamu ambaye alionyesha kikamili sifa na utu wake.

Mwanadamu huyo alikuwa Yesu. (Wafilipi 2:7) Yesu hakuongea tu kumhusu Baba yake bali alituonyesha pia jinsi alivyo. Filipo aliyekuwa mwanafunzi wa Yesu alimwambia: “Bwana, tuonyeshe Baba.” Naye Yesu akajibu: “Yule ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” (Yohana 14:8, 9) Unawezaje ‘kumwona’ Baba kupitia matendo ya Yesu?

Yesu alikuwa mchangamfu, mnyenyekevu, na mwenye urafiki. (Mathayo 11:28-30) Utu wake wenye kuburudisha ulifanya watu wamkaribie. Yesu alihuzunika watu walipohuzunika, na akashangilia waliposhangilia. (Luka 10:17, 21; Yohana 11:32-35) Unaposoma au kusikiliza masimulizi ya Biblia kumhusu Yesu, husisha hisia zako na uwazie hali ilivyokuwa. Ukitafakari jinsi Yesu alivyoshughulika na watu, utaona waziwazi utu wa pekee wa Mungu na hivyo kumkaribia.

KUELEWA HABARI

Akizungumza kuhusu kipofu, mwandishi mmoja alisema: “Yeye hupata habari ndogondogo kutoka vyanzo mbalimbali (kupitia kugusa, kunusa, kusikia, na kadhalika), na anahitaji kuziunganisha ili aelewe habari kamili.” Vivyo hivyo, unapotazama uumbaji wa Mungu, kusoma yale ambayo Yesu alisema kumhusu Baba yake, na kuchunguza jinsi Yesu alivyoonyesha sifa za Mungu, utamwona Yehova vizuri. Atakuwa halisi zaidi kwako.

Ayubu aliyeishi nyakati za kale alijionea jambo hilo. Mwanzoni aliongea ‘lakini hakuelewa.’ (Ayubu 42:3) Hata hivyo, alipochunguza kwa makini maajabu ya uumbaji wa Mungu, Ayubu alichochewa kusema: “Nimesikia habari zako . . . , lakini sasa jicho langu mwenyewe linakuona wewe.”Ayubu 42:5.

‘Ukimtafuta Yehova, ataacha umpate’

Inaweza kuwa hivyo kwako pia. “Ukimtafuta [Yehova], ataacha umpate.” (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia umtafute na kumpata Mungu asiyeonekana.