Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 7

Jinsi ya Kumfundisha Mtoto Wako

Jinsi ya Kumfundisha Mtoto Wako

“Maneno haya ninayokuamuru leo lazima yawe moyoni mwako; nawe uyakazie kwa mwana wako.”​—Kumbukumbu la Torati 6:6, 7

Yehova alipoanzisha familia, aliwapa wazazi jukumu la kuwatunza watoto wao. (Wakolosai 3:20) Ni jukumu lako ukiwa mzazi kuwafundisha watoto wako kumpenda Yehova na kuwa watu wazima wenye kutegemeka. (2 Timotheo 1:5; 3:15) Pia, lazima ujifunze kutambua hisia na maoni ya watoto wako. Kwa kweli, mfano wako ni muhimu sana. Unaweza kumfundisha vizuri mtoto wako kuhusu sheria za Yehova ikiwa wewe mwenyewe unazifuata.​—Zaburi 40:8.

1 FANYA IWE RAHISI KWA WATOTO KUZUNGUMZA NAWE

BIBLIA INASEMA HIVI: Uwe “mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema.” (Yakobo 1:19) Unapaswa kuwapa watoto wako uhuru wa kuzungumza nawe. Wanapaswa kujua kwamba uko tayari kuwasikiliza wanapohitaji kuzungumza. Hakikisha kwamba kuna hali ambazo zinawaruhusu wajieleze kwa uhuru. (Yakobo 3:18) Wakigundua kwamba wewe ni mkali na unawakosoa-kosoa hawatapenda kuzungumza nawe. Uwe mwenye subira, na uwahakikishie mara kwa mara kwamba unawapenda.​—Mathayo 3:17; 1 Wakorintho 8:1.

UNACHOWEZA KUFANYA:

  • Uwe karibu watoto wako wanapohitaji kuzungumza

  • Zungumza na watoto wako kwa ukawaida, usisubiri tu wanapokuwa na matatizo

2 JITAHIDI KUELEWA WANACHOMAANISHA

BIBLIA INASEMA HIVI: “Anayetumia ufahamu katika jambo atapata mema.” (Methali 16:20)Zaidi ya kuelewa maneno ya mtoto wako unahitaji pia kuelewa hisia zake. Ni kawaida kwa watoto kutia chumvi au kusema mambo ambayo hawamaanishi. “Yeyote anapojibu jambo kabla ya kulisikia, huo ni upumbavu.” (Methali 18:13) Usikasirike haraka.​—Methali 19:11.

UNACHOWEZA KUFANYA:

  • Epuka kumkatisha au kumkasirikia mtoto anapozungumza, hata kama anasema mambo yasiyo muhimu

  • Kumbuka jinsi ambavyo wewe pia ulitenda ulipokuwa mtoto na mambo yaliyokuwa muhimu kwako

3 MUWE NA UMOJA

BIBLIA INASEMA HIVI: “Mwanangu, sikiliza nidhamu ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako.” (Methali 1:8) Yehova amewapa wazazi mamlaka ya kuwalea watoto wao. Mnapaswa kuwafundisha watoto wenu kuwaheshimu na kuwatii mkiwa wazazi. (Waefeso 6:1-3) Watoto wanaweza kugundua kama kweli mmeunganishwa “vema katika akili ileile.” (1 Wakorintho 1:10) Ikiwa hamkubaliani, msibishane mbele ya watoto wenu kwa sababu hilo litawafanya washindwe kuwaheshimu.

UNACHOWEZA KUFANYA:

  • Zungumzeni na kukubaliana jinsi ya kuwatia nidhamu watoto wenu

  • Ikiwa wewe na mwenzi wako mnatofautiana kuhusu kuwazoeza watoto wenu, jitahidi kuelewa maoni ya mwenzi wako

4 FANYENI MIPANGO

BIBLIA INASEMA HIVI: “Mlee mvulana kulingana na njia inayomfaa.” (Methali 22:6) Jitihada zinahitajika ili mfaulu kuwafundisha watoto wenu. Mnahitaji kufanya mipango, ambayo inatia ndani kuwatia nidhamu watoto wenu. (Zaburi 127:4; Methali 29:17) Nidhamu haimaanishi tu kuwaadhibu watoto, pia inatia ndani kuwasaidia kuelewa sababu za kutii sheria. (Methali 28:7) Wafundishe kupenda Neno la Yehova na kufuata kanuni zake. (Zaburi 1:2) Kufanya hivyo kutawasaidia kusitawisha dhamiri njema.​—Waebrania 5:14.

UNACHOWEZA KUFANYA:

  • Wasaidie watoto wako kumwona Mungu akiwa halisi na kumtegemea

  • Wasaidie kujua na kuepuka hatari za kimaadili, kama zile zilizo kwenye Intaneti na mitandao ya kijamii. Wafundishe jinsi ya kuepuka watu wanaowavizia watoto ili kufanya ngono nao

“Mlee mvulana kulingana na njia inayomfaa”