Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 2

Uwe Mshikamanifu kwa Mwenzi Wako

Uwe Mshikamanifu kwa Mwenzi Wako

“Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”​—Marko 10:9

Yehova anataka ‘tupende fadhili.’ (Mika 6:8) Kulingana na Biblia neno fadhili linamaanisha upendo unaofanya vitu au watu wawili washikamane. Hilo ni jambo muhimu katika ndoa kwa sababu ushikamanifu unahitajiwa ili watu waaminiane na kupendana.

Leo, watu wengi si washikamanifu kwa wenzi wao. Ili kuilinda ndoa yako, unapaswa kuazimia kufanya mambo mawili.

1 TANGULIZA NDOA YAKO

BIBLIA INASEMA HIVI: “Mhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.” (Wafilipi 1:10) Ndoa yako ni moja kati ya mambo ya maana zaidi maishani mwako. Hivyo, inapaswa kutangulizwa.

Yehova anataka umkazie fikira mwenzi wako na ‘mfurahie maisha’ pamoja. (Mhubiri 9:9) Anaonyesha waziwazi kwamba hupaswi kamwe kumpuuza mwenzi wako, badala yake, mnapaswa kutafuta njia za kufurahishana. (1 Wakorintho 10:24) Mwonyeshe mwenzi wako kwamba unamhitaji na unamthamini.

UNACHOWEZA KUFANYA:

  • Hakikisha kwamba unatumia wakati wa kutosha pamoja na mwenzi wako na umsikilize kwa makini

  • Usijifikirie mwenyewe tu

2 LINDA MOYO WAKO

BIBLIA INASEMA HIVI: “Kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” (Mathayo 5:28) Hivyo, mtu akiendelea kufikiria mambo machafu kiadili anakosa kuwa mwaminifu kwa mwenzi wake wa ndoa.

Yehova anasema kwamba unapaswa ‘kuulinda moyo wako.’ (Methali 4:23; Yeremia 17:9) Ili kufanya hivyo, unapaswa kudhibiti macho yako. (Mathayo 5:29, 30) Fuata mfano wa mzee wa ukoo Ayubu, ambaye alifanya agano na macho yake ili asimtazame mwanamke mwingine kwa tamaa. (Ayubu 31:1) Azimia kabisa kutotazama ponografia. Epuka uhusiano wowote wa kimapenzi na mtu ambaye si mwenzi wako wa ndoa.

UNACHOWEZA KUFANYA:

  • Onyesha wazi kwamba wewe ni mshikamanifu kabisa kwa mwenzi wako

  • Fikiria hisia za mwenzi wako na ukatishe mara moja uhusiano wowote unaoweza kumuumiza