Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 5

Jinsi ya Kuishi kwa Amani na Watu wa Ukoo

Jinsi ya Kuishi kwa Amani na Watu wa Ukoo

“Jivikeni . . . fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu.”​—Wakolosai 3:12

Watu wanapofunga ndoa wanaanzisha familia mpya. Ingawa utaendelea kuwapenda na kuwaheshimu wazazi wako, sasa mwenzi wako ndiye mtu muhimu zaidi maishani mwako. Huenda ikawa vigumu kwa baadhi ya watu wa ukoo kukubali jambo hilo. Lakini kanuni za Biblia zinaweza kukusaidia kuwa na usawaziko, ili udumishe amani na watu wa ukoo na wakati uleule ujitahidi kuiimarisha familia yako mpya.

1 UWE NA MAONI YANAYOFAA KUHUSU WATU WA UKOO

BIBLIA INASEMA HIVI: “Mheshimu baba yako na mama yako.” (Waefeso 6:2) Hata uwe na umri gani, sikuzote unapaswa kuwaheshimu wazazi wako. Kumbuka kwamba mwenzi wako pia, akiwa mwana au binti, anahitaji kuwafikiria wazazi wake. “Upendo hauna wivu,” hivyo usihisi vibaya kwa sababu ya uhusiano wa mwenzi wako pamoja nao.​—1 Wakorintho 13:4; Wagalatia 5:26.

UNACHOWEZA KUFANYA:

  • Epuka kusema mambo kwa ujumla, kama vile “Familia yako hunidharau sikuzote” au “Mama yako hapendi chochote ninachofanya”

  • Jaribu kuelewa maoni ya mwenzi wako

2 WEKENI MIPAKA INAPOHITAJIKA

BIBLIA INASEMA HIVI: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake nao watakuwa mwili mmoja.” (Mwanzo 2:24) Mnapofunga ndoa, huenda wazazi wenu wakahisi kwamba wanapaswa kuendelea kuwatunza, na huenda wakataka kuingilia ndoa yenu kupita kiasi.

Wewe na mwenzi wako mnahitaji kukubaliana kuhusu mipaka ambayo mtawawekea na kuwaeleza kwa upendo. Mnaweza kuwaambia moja kwa moja na waziwazi bila kuwakosea heshima. (Methali 15:1) Mkionyesha unyenyekevu, upole, na subira mtakuwa na uhusiano mzuri na watu wa ukoo na kuendelea “kuvumiliana katika upendo.”​—Waefeso 4:2.

UNACHOWEZA KUFANYA:

  • Ikiwa unahisi kwamba watu wa ukoo wanajihusisha kupita kiasi na maisha yenu, zungumzia jambo hilo pamoja na mwenzi wako kwa utulivu

  • Kubalianeni jinsi mtakavyoshughulikia hali hizo