Hamia kwenye habari

Wazazi Wanawezaje Kuwafundisha Watoto Wao Kuhusu Ngono?

Wazazi Wanawezaje Kuwafundisha Watoto Wao Kuhusu Ngono?

Jibu la Biblia

 Ni nani anapaswa kuwafundisha watoto kuhusu ngono? Biblia inasema ni wajibu wa wazazi, na wengi wamefaidika na mapendekezo yafuatayo:

  •   Usione aibu. Biblia inasema waziwazi kuhusu ngono na viungo vya uzazi, na Mungu aliliambia taifa la Israeli kwamba “watoto” wanapaswa kufundishwa kuhusu mambo hayo. (Kumbukumbu la Torati 31:12; Mambo ya Walawi 15:​2, 16-​19) Unaweza kutumia maneno yasiyovunja heshima unapozungumza kuhusu ngono au viungo vya uzazi.

  •   Wafundishe hatua kwa hatua. Badala ya kuwafundisha watoto kwa kipindi kimoja tu wanapobalehe, endelea kuwafundisha kadiri wanavyoendelea kuelewa.​—1 Wakorintho 13:11.

  •   Wafundishe viwango vya maadili. Huenda wakajifunza baadhi ya mambo kuhusu ngono wakiwa shuleni. Hata hivyo, Biblia inawatia moyo wazazi wafundishe watoto wao kuhusu viungo vya uzazi na matumizi yanayofaa ya viungo hivyo.​—Methali 5:​1-​23.

  •   Msikilize mtoto wako. Usikasirike au kumhukumu upesi mtoto anapokuuliza maswali kuhusu ngono. Badala yake uwe “mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema.”​—Yakobo 1:​19.

Unaweza kumlindaje mtoto wako kutokana na wanaovizia watoto ili wafanye nao ngono

  • Mfundishe mtoto wako jinsi ya kuwapinga watu wanaowasumbua watoto kingono

      Jielimishe. Jifunze mbinu wanazotumia.​—Methali 18:15; ona sura ya 32 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza​—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1.

  •   Jihusishe na mambo ambayo mtoto wako anafanya. Usimpe mtu mwingine daraka la kulea mtoto wako iwapo hujui ikiwa anaaminika na ‘usimwachilie’ mtoto wako.​—Methali 29:15.

  •   Mfundishe awe na maoni yenye usawaziko kuhusu utii. Watoto wanapaswa kujifunza kuwatii wazazi wao. (Wakolosai 3:​20) Hata hivyo, ikiwa utamfundisha mtoto wako kwamba lazima nyakati zote amtii kila mtu maadamu ni mtu mzima, itakuwa rahisi kutendewa vibaya kingono. Wazazi Wakristo wanaweza kuwaambia watoto wao kwamba ‘Ikiwa mtu fulani anakwambia ufanye jambo fulani ambalo Mungu anasema ni baya, usifanye.’​—Matendo 5:​29.

  •   Wazoeze hatua rahisi wanazoweza kuchukua ili kujilinda. Msaidie mtoto wako ajifunze jambo analoweza kufanya ikiwa mtu fulani atataka kumtendea vibaya wakati haupo. Fanya mazoezi ambayo yatampa ujasiri wa kusema: “Usifanye hivyo! Nitamwambia baba au mama!” na aondoke haraka mahali hapo. Unapaswa kuwakumbusha watoto wako tena na tena, kwa sababu wanaweza kusahau haraka.​—Kumbukumbu la Torati 6:7.