Barua kwa Wakolosai 4:1-18

  • Ushauri kwa mabwana (1)

  • “Dumuni katika sala” (2-4)

  • Kutembea kwa hekima kuelekea walio nje (5, 6)

  • Salamu za mwisho (7-18)

4  Enyi mabwana, watendeeni watumwa wenu kwa njia ya uadilifu na haki, mkijua kwamba ninyi pia mna Bwana mbinguni.+  Dumuni katika sala,+ mkikaa macho katika sala pamoja na kutoa shukrani.+  Wakati huohuo, salini pia kwa ajili yetu,+ ili Mungu afungue mlango kwa ajili ya neno ili tutangaze siri takatifu kumhusu Kristo, ambayo kwa ajili yake nimefungwa gerezani,+  na ili niitangaze waziwazi kama ninavyopaswa.  Endeleeni kutembea kwa hekima kuelekea wale walio nje, mkitumia vizuri kabisa wakati wenu.*+  Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote,+ yaliyokolezwa chumvi, ili mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.+  Tikiko,+ ndugu yangu mpendwa na mhudumu mwaminifu na mtumwa mwenzangu katika Bwana, atawaambia habari zote kunihusu.  Ninamtuma kwenu ili mjue jinsi tunavyoendelea na ili aifariji mioyo yenu.  Anakuja pamoja na Onesimo,+ ndugu yangu mwaminifu na mpendwa, ambaye anatoka kwenu; watawaambia kuhusu mambo yote yanayoendelea huku. 10  Aristarko,+ mateka mwenzangu anawatumia salamu zake, na pia Marko,+ binamu ya Barnaba (ambaye mlipokea maagizo ya kumkaribisha+ ikiwa atakuja kwenu), 11  na Yesu anayeitwa Yusto, walio kati ya wale waliotahiriwa. Ni hawa tu walio wafanyakazi wenzangu kwa ajili ya Ufalme wa Mungu, nao wamekuwa chanzo cha faraja* nyingi kwangu. 12  Epafra,+ mtumwa wa Kristo Yesu, ambaye ametoka kwenu, anawatumia salamu zake. Sikuzote anajikaza kwa ajili yenu katika sala zake, ili mwishowe msimame mkiwa kamili na kwa usadikisho imara katika mapenzi yote ya Mungu. 13  Kwa maana ninamtolea ushahidi kwamba anajitahidi sana kwa ajili yenu na kwa ajili ya wale walio Laodikia na Hierapoli. 14  Luka,+ daktari mpendwa anawatumia salamu zake, na pia Dema.+ 15  Wapeni salamu zangu ndugu huko Laodikia na pia msalimuni Nimfa na kutaniko lililo katika nyumba yake.+ 16  Na baada ya kusoma barua hii miongoni mwenu, pangeni isomwe+ pia katika kutaniko la Walaodikia, nanyi pia msome ile ya kutoka Laodikia. 17  Pia, mwambieni Arkipo hivi:+ “Zingatia huduma uliyoikubali katika Bwana, ili uitimize.” 18  Hii ni salamu yangu, Paulo, kwa mkono wangu mwenyewe.+ Endeleeni kukumbuka vifungo vyangu vya gereza.+ Fadhili zisizostahiliwa ziwe pamoja nanyi.

Maelezo ya Chini

Tnn., “mkijinunulia wakati unaofaa.”
Au “msaada wa kunitia nguvu.”