Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU

Mtazamo Unaweza Kuboresha Maisha Yako!

Mtazamo Unaweza Kuboresha Maisha Yako!

Furaha yako inategemea jambo gani kati ya haya:

  • hali zako

  • chembe zako za urithi

  • mtazamo wako

WATU wengine wanaweza kufikiri ni “hali,” labda wakijiambia, “Ningekuwa na furaha . . .

  • “ikiwa ningekuwa na pesa zaidi”

  • “ikiwa ningekuwa na ndoa nzuri zaidi”

  • “ikiwa ningekuwa na afya nzuri zaidi”

Hata hivyo, mara nyingi mtazamo wako ndio huamua ikiwa utakuwa na furaha, si hali au chembe zako za urithi. Na hilo ni jambo zuri. Kwa nini? Kwa sababu unaweza kubadili mtazamo wako, lakini huwezi kudhibiti hali zako wala chembe zako za urithi.

“DAWA NZURI”

Methali moja ya Biblia inasema hivi: “Moyo wenye shangwe ni dawa nzuri, lakini roho iliyopondeka huikausha mifupa.” (Methali 17:22) Yaani, mtazamo wako ndio huamua ikiwa utakuwa na furaha au la! Mtazamo unaweza kuamua kama utatimiza lengo lako au utakata tamaa. Pia, mtazamo utaamua ikiwa utatenda kwa njia inayofaa au la unapokabili hali mbaya.

Huenda watu fulani wakawa na shaka kuhusu hilo. Huenda wakasema:

  • ‘Kwa nini nitazamie mema ilhali ninakabili matatizo?’

  • ‘Kufikiria mema hakuwezi kubadili hali yangu.’

  • ‘Afadhali kuona mambo kihalisi badala ya kuota ndoto.’

Huenda mawazo hayo yakaonekana kuwa yanafaa. Lakini kuwa na mtazamo unaofaa kuna faida. Kwa mfano, fikiria hali zifuatazo.

Alex na Brian wanafanya kazi kwa bidii wakishughulikia mambo tofauti. Baada ya msimamizi wao kukagua kazi walizofanya, anawaonyesha makosa yao.

  • Alex: “Nilitumia muda na jitihada nyingi sana katika kazi hiyo, na bado sikuifanya vizuri! Sitafanikiwa katika kazi hii. Hata nikitia bidii kadiri gani, bado siifanyi kwa njia inayofaa. Kwa nini nijisumbue?”

  • Brian: “Msimamizi wangu alitaja mambo yaliyompendeza, lakini pia kazi yangu ilikuwa na makosa kadhaa makubwa. Nimejifunza mambo muhimu ambayo yatanisaidia niifanye vizuri zaidi wakati ujao.”

UNA MAONI GANI?

  • Miezi sita kutoka sasa, kati ya Alex na Brian, ni nani atakayekuwa mfanyakazi mzuri zaidi?

  • Ikiwa wewe ni mwajiri, ni mwanamume gani kati ya hao wawili ambaye ungemwajiri au ungetaka aendelee kukufanyia kazi?

  • Unapokata tamaa, wewe hutenda kama mwanamume gani kati ya hao wawili?

Mara kwa mara Andrea na Brittney huwa wapweke. Kila mmoja wao ana njia tofauti ya kukabiliana na hali hiyo.

  • Andrea anajielekezea fikira sana. Hawezi kuwatendea wengine mambo mazuri isipokuwa wao wamtendee hivyo kwanza. Yeye hujiambia, ‘Kwa nini nipoteze muda wangu na watu ambao hawanisaidii kwa njia yoyote?’

  • Brittney anajitahidi kuwa mwenye fadhili na kuwatendea wengine mema, iwe wanathamini au la. Kila siku anafuata ile Kanuni Bora—anawatendea wengine kama anavyotaka kutendewa. (Luka 6:31) Kwa maoni ya Brittney, unafurahi unapowatendea wengine mema iwe wamethamini au la.

UNA MAONI GANI?

  • Kati ya wanawake hao wawili ni yupi ambaye ungependa awe rafiki yako?

  • Ni yupi ambaye huenda ataridhishwa zaidi na urafiki wake pamoja na wengine?

  • Unapokuwa mpweke, wewe hutenda kama Andrea au kama Brittney?

Huenda unawafahamu watu walio na mtazamo kama wa Brian na Brittney. Huenda ukahisi kwamba wewe pia una mtazamo kama wao. Ikiwa ndivyo, basi unatambua kwamba mtazamo wako unaweza kuboresha maisha yako. Lakini, namna gani ikiwa una mtazamo kama wa Alex au Andrea? Hebu ona njia tatu ambazo Biblia inaweza kukusaidia kuwa na mtazamo unaofaa unapokabili hali ngumu maishani.

1 EPUKA KUTAZAMIA MABAYA

BIBLIA INASEMA HIVI: “Je, umejionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako zitakuwa chache.”—Methali 24:10.

HILO LINAMAANISHA NINI? Kutazamia mabaya kunaweza kumaliza nguvu unazohitaji kukabiliana na hali ngumu.

MFANO: Juliza alipokuwa mtoto hakuwa na maisha yenye furaha. Baba yake alikuwa mlevi, familia yao ilikuwa maskini, na walihamahama sana. Mwanzoni, Juliza alitazamia mabaya tu maishani mwake. Lakini mtazamo wake ulibadilika. Ni nini kilichomsaidia? Juliza anasema hivi: “Biblia ilinisaidia kuboresha mtazamo wangu hata kabla ya wazazi wangu kutatua matatizo yao. Hadi leo, mambo ninayojifunza katika Biblia yananisaidia nisitazamie mambo mabaya tu. Siku hizi watu wanapofanya mambo yanayoniudhi, ninajaribu kuelewa kwa nini wanatenda kwa njia hiyo.”

Juliza alijifunza kwamba Biblia ni kitabu kilicho na kanuni zinazofaa. Ushauri wake unaweza kukusaidia kukabiliana na hali ngumu. Kwa mfano, Waefeso 4:23 inasema: “Mnapaswa kufanywa upya katika nguvu zinazoendesha akili yenu.”

Mstari huo unaonyesha kwamba unaweza kubadili mtazamo wako. Unaweza “kufanywa upya” katika akili yako. Hata hivyo, kubadili fikira zako ni jambo la kuendelea.

2 KAZIA FIKIRA MAMBO YANAYOFAA

BIBLIA INASEMA HIVI: “Siku zote za mwenye kuteseka ni mbaya, lakini mtu aliye mchangamfu moyoni huwa na karamu sikuzote.”—Methali 15:15.

HILO LINAMAANISHA NINI? Ikiwa kila wakati unaona mambo kwa njia isiyofaa, utahisi kuwa ‘unateseka’ na kila siku itakuwa “mbaya” kwako. Lakini ukikazia fikira mambo yanayofaa, utakuwa na ‘moyo mchangamfu’ na utakuwa na shangwe. Uamuzi ni wako.

MFANO: Baada ya Yanko kufanyiwa upasuaji mara kadhaa ili kuondoa uvimbe kwenye ubongo, alilemaa kidogo hivi kwamba hangeweza kutembea vizuri na kuzungumza kwa njia ya kawaida. Kwa miaka kadhaa Yanko alivunjika moyo sana kwa sababu alihisi ulemavu wake ungemzuia kufikia miradi yake. Kisha akabadili maoni. Jinsi gani? Anasema hivi, “Badala ya kukazia fikira udhaifu wangu, nilijifunza kukazia fikira mambo yenye kunitia moyo.”

Njia moja ambayo Yanko hufanya hivyo ni kwa kusoma Biblia. Anasema: “Kufanya hivyo hunisaidia kufikiria mambo mazuri. Sijabadili miradi yangu, lakini kwa sasa ninakazia fikira miradi midogo ambayo ninaweza kuifikia. Mawazo yenye kuvunja moyo yanapoingia akilini, mimi hutafakari sababu nyingi nilizo nazo za kuwa na furaha.”

Kama Yanko, unaweza kukabiliana na mawazo yasiyofaa na kuyabadili kwa kufikiria mambo mazuri. Ikiwa unakabiliana na tatizo la afya au hali nyingine ngumu, jiulize hivi: ‘Je, kweli hali yangu itaendelea tu kuwa mbaya? Kweli siwezi kushinda tatizo hili?’ Jifunze kuepuka mawazo yasiyofaa kwa kukazia fikira mambo mazuri.

3 WASAIDIE WENGINE

BIBLIA INASEMA HIVI: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.

HILO LINAMAANISHA NINI? Unapotoa bila ubinafsi unaridhika sana. Kwa nini? Kwa sababu tuliumbwa tukiwa na uwezo wa kushughulikia si mahitaji yetu tu bali ya wengine pia. (Wafilipi 2:3, 4; 1 Yohana 4:11) Shangwe inayotokana na kutoa inaweza kutusaidia kukabiliana na hali mbaya maishani.

MFANO: Josué alizaliwa akiwa na tatizo la uti wa mgongo (spina bifida). Mara nyingi yeye huwa na maumivu. Lakini Josué anafurahia sana kuwasaidia wengine. Josué anasema hivi: “Badala ya kusema, ‘Siwezi kufanya jambo fulani,’ mimi hujitahidi kufikiria njia zinazofaa za kuwasaidia watu kushughulikia mahitaji yao ya kila siku. Ninajitahidi kutafuta njia za kuwasaidia wengine, na hilo huniletea furaha maishani.”

UNAWEZA KUFANYA NINI?

Tafuta nafasi za kuwasaidia wengine. Kwa mfano, unaweza kumtayarishia jirani yako mlo anapokuwa mgonjwa? Je, unajua watu wenye umri mkubwa wanaohitaji kusaidiwa kazi za nyumbani?

Sitawisha mtazamo unaofaa, kama mtu anavyofanya anapotunza bustani. Ng’oa mitazamo isiyofaa, kama unavyoweza kung’oa magugu. Panda mbegu, yaani, tazamia mema, na utie mbolea kwa kutenda mambo yanayokufanya uwe na hisia zinazofaa. Utavuna mambo yatakayofanya maisha yako yawe yenye kuthawabisha sana. Na utakuwa na uhakika kwamba mtazamo mzuri unaweza kuboresha maisha yako!

Epuka mitazamo isiyofaa kama vile baadhi ya watu wanavyoepuka vyakula fulani kwa sababu ya afya