Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Upendo wa Mungu Unavyoweza Kukunufaisha

Jinsi Upendo wa Mungu Unavyoweza Kukunufaisha

Mungu ameumba miili yetu ikiwa na uwezo wa pekee wa kujiponya. Unapokatwa, kukwaruzwa, au kuchanwa, mwili wenye afya nzuri “hutenda kwa njia tata sana iliyokusudiwa kuponya vidonda vikubwa na vidogo pia.” (Johns Hopkins Medicine) Mara moja, mwili huanza kutenda ili kuzuia damu isiendelee kuvuja, kuponya kidonda, na kuimarisha sehemu ya mwili iliyojeruhiwa.

FIKIRIA HILI: Ikiwa Muumba aliipa miili yetu uwezo wa kujiponya, je, hatupaswi kuwa na uhakika kwamba atatimiza ahadi yake ya kutusaidia kupona majeraha ya kihisia ambayo tumepata? Mtunga zaburi alisema hivi kumhusu Mungu: “Huwaponya waliovunjika moyo; huyafunga majeraha yao.” (Zaburi 147:3) Lakini ikiwa una majeraha ya kihisia, labda kutokana na hali zilizotukia wakati uliopita au unazokabili sasa, unawezaje kuwa na uhakika kwamba Yehova atayafunga majeraha yako sasa na wakati ujao?

BIBLIA INATUFUNDISHA NINI KUHUSU UPENDO WA MUNGU?

Mungu anatuahidi hivi: “Usiogope, kwa maana mimi niko pamoja nawe. Usihangaike, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia.” (Isaya 41:10) Mtu anayeamini kwamba Yehova anamjali huwa na amani ya akili na nguvu za kukabiliana na changamoto mbalimbali. Mtume Paulo aliuita utulivu huo wa moyoni kuwa “amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote.” Aliongezea kusema: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yule anayenipa nguvu.”—Wafilipi 4:4-7, 9, 13.

Maandiko hutusaidia kusitawisha imani katika ahadi za Yehova kuhusiana na wakati ujao wa wanadamu. Kwa mfano, andiko la Ufunuo 21:4, 5 linatuambia yale atakayofanya na kutaja sababu za kumwamini:

  • “Atafuta kila chozi kutoka katika macho” ya wanadamu. Yehova ataondoa mahangaiko na mateso yote tunayokabili, hata yale ambayo wengine wanayaona kuwa madogo.

  • Akiwa ameketi “kwenye kiti cha ufalme” katika utukufu wa mbinguni, Mfalme Mweza-Yote aliyeumba kila kitu atatumia nguvu na mamlaka yake kuzuia mateso na kutupatia msaada tunaohitaji.

  • Yehova anatuhakikishia kwamba maneno yake ni ya “uaminifu na ya kweli.” Yaani, anahusianisha moja kwa moja kutimizwa kwa ahadi zake na cheo chake akiwa Mungu wa kweli.

“‘Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.’ Na Yule aliyeketi kwenye kiti cha ufalme akasema: ‘Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.’ Pia anasema: ‘Andika, kwa maana maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.’”—Ufunuo 21:4, 5.

Uumbaji na Biblia hufunua utu na sifa za Baba yetu wa mbinguni. Tunapochunguza uumbaji, tunaona sifa zinazotuchochea kujenga urafiki wa karibu na Mungu. Hata hivyo, Biblia hutupatia mwaliko huo waziwazi inaposema: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:8) Andiko la Matendo 17:27 linasema: “Hayuko mbali na kila mmoja wetu.”

Kadiri unavyotenga muda wa kujifunza ili umjue Mungu, ndivyo utakavyopata uhakika zaidi kwamba ‘anakujali.’ (1 Petro 5:7) Tutapata faida gani ikiwa tutamwamini Yehova kwa njia hiyo?

Hebu fikiria kisa cha Toru, anayeishi Japani. Alilelewa na mama Mkristo, lakini alianza kushirikiana na yakuza, kikundi cha wahalifu nchini Japani. Anasimulia hivi: “Niliamini kwamba Mungu ananichukia, na nilihisi kwamba alisababisha vifo vya watu wangu wa karibu, hasa wale niliowapenda sana, ili kuniadhibu.” Toru anasema kwamba kwa sababu ya kushirikiana na watu wabaya na kuwa na mawazo yasiyofaa, alianza kuwa “mtu asiye na huruma wala hisia zozote.” Anaendelea kusema hivi: “Nilitamani nife nikiwa mdogo baada ya kuwa nimeua mtu mashuhuri kuliko mimi na hivyo kujitengenezea jina.”

Hata hivyo, baada ya yeye na mke wake, Hannah, kujifunza Biblia, maisha ya Toru yalibadilika haraka sana, kutia ndani mtazamo wake. Hannah anasema: “Nilishuhudia mume wangu akifanya mabadiliko.” Sasa, Toru anasema hivi kwa uhakika: “Kuna Mungu ambaye anamjali kila mmoja wetu. Hataki yeyote afe, na yuko tayari kuwasamehe wale wanaotubu kikweli makosa yao. Yeye husikiliza tunapomweleza mambo ambayo hatuwezi kumwambia mtu mwingine yeyote na ambayo hakuna anayeweza kuyaelewa. Hivi karibuni, Yehova ataondoa matatizo yote, kuteseka, na uchungu. Hata sasa, yeye hutusaidia katika njia tusizotazamia kabisa. Anatujali na hutusaidia tunapolemewa na hisia.”​—Zaburi 136:23.

Kama simulizi la Toru linavyoonyesha, kujua kwamba Mungu ana uwezo wa kuondoa matatizo yote na kufuta machozi yote na kwamba atafanya hivyo hivi karibuni, hutupatia tumaini hakika la wakati ujao. Na si hilo tu, bali pia hutusaidia kuishi maisha mazuri sasa. Naam, hata ingawa unaishi katika ulimwengu uliojaa changamoto nyingi, unaweza kunufaishwa na upendo wa Mungu.