Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

UNAWEZA KUKABILIANA NA MKAZO—JINSI GANI?

Jinsi ya Kukabiliana na Mkazo

Jinsi ya Kukabiliana na Mkazo

Ili kukabiliana na mkazo kwa njia inayofaa, unahitaji kufikiria kuhusu afya yako, jinsi unavyoshughulika na wengine, malengo yako na mambo unayotanguliza maishani, yaani, mambo yaliyo muhimu zaidi. Makala hii itafafanua kanuni zinazoweza kukusaidia kushughulika na mkazo kwa njia inayofaa na labda hata kuupunguza.

Hangaikia Mahitaji ya Leo Si ya Kesho

“Msihangaike kamwe kuhusu kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe.”—MATHAYO 6:34.

Maana yake: Mahangaiko ya kila siku ni sehemu ya maisha. Hata hivyo, usijiongezee mzigo zaidi kwa kubeba mahangaiko ya kesho. Jaribu kuhangaikia mahitaji ya leo tu.

  • Mkazo unaweza kusababisha wasiwasi. Kwa hiyo jaribu kutumia mapendekezo yafuatayo: Kwanza, kumbuka kwamba kuna aina fulani ya mkazo ambayo huwezi kuepuka. Wasiwasi kuhusu mambo ambayo huwezi kuepuka huongeza mkazo. Pili, kumbuka kwamba mara nyingi mambo unayohofia huenda yasitokee.

Jiwekee Viwango Unavyoweza kufikia

“Hekima inayotoka juu . . . ni . . . yenye usawaziko.”—YAKOBO 3:17.

Maana yake: Usitazamie ukamilifu. Epuka kujiwekea au kuwawekea wengine viwango vya juu kupita uwezo wao.

  • Uwe na kiasi, jiwekee viwango unavyoweza kufikia, na tambua mambo ambayo wewe na wengine mnaweza kufanya na yale msiyoweza kufanya. Ukifanya hivyo, utapunguza mkazo wako na wa wengine na hata itakuwa rahisi kufikia viwango ulivyojiwekea. Pia, uwe mcheshi. Ukicheka, hata kama mambo yamekwenda vibaya, utapunguza mkazo na kufanya ujihisi vizuri.

Jitahidi Kutambua Mambo Yanayokupa Mkazo

“Mtu mwenye utambuzi atabaki mtulivu.”—METHALI 17:27.

Maana yake: Hasira, wasiwasi au kutokuwa na subira kunaweza kukuzuia usifikiri kwa njia nzuri, kwa hiyo, jitahidi kuwa mtulivu.

  • Jitahidi kutambua mambo yanayokuletea mkazo, na jinsi unavyotenda hali hiyo inapotokea. Kwa mfano, unapokuwa na mkazo, changanua mambo unayofikiria, hisia zako, na tabia; na hata unaweza kuandika mambo hayo. Kuwa makini kutambua jinsi unavyotenda unapopata mkazo, kutakusaidia kushughulikia hali hiyo kwa njia bora. Pia, fikiria njia za kuondoa mambo yanayokupa mkazo maishani. Ikiwa hilo haliwezekani, tafuta njia za kupunguza matokeo ya mkazo, labda kwa kupanga kazi zako vizuri au muda unaotumia kufanya kazi.

  • Jitahidi kubadili njia yako ya kuona mambo. Huenda jambo linalokuhangaisha, lisimhangaishe mtu mwingine. Inawezekana tofauti ikawa ni njia yenu ya kuona mambo. Fikiria mapendekezo haya matatu:

    1. Usifikiri haraka kwamba watu wana nia mbaya. Kwa mfano, ukiwa kwenye mstari, mtu anaweza kukupita na kwenda mbele yako. Ukihisi umetendewa kwa njia isiyofaa, huenda ukakasirika. Badala yake, kwa nini usifikiri kwamba alikuwa na nia nzuri? Huenda ukawa hujakosea!

    2. Uwe na mtazamo unayofaa. Kwa mfano, itakuwa rahisi kupunguza mkazo ikiwa utaamua kusoma au kufanya kazi au kutuma barua pepe wakati unaposubiri kwa muda mrefu huduma kutoka kwa daktari au ukiwa uwanja wa ndege.

    3. Fikiria mambo kwa upana zaidi. Jiulize, ‘Je, tatizo hili litakuwa kubwa kesho au juma lijalo kama linavyoonekana leo?’ Tofautisha kati ya mambo madogo au ya muda mfupi na mambo mazito zaidi.

Jitahidi Kuwa Mwenye Utaratibu

“Mambo yote na yatendeke kwa adabu na kwa mpango.”—1 WAKORINTHO 14:40.

Maana yake: Jitahidi kuwa mwenye utaratibu maishani mwako.

  • Tunapenda kuwa na kiwango kinachofaa cha utaratibu katika maisha yetu. Jambo moja linaloweza kuvuruga utaratibu na kusababisha mkazo ni kuahirisha mambo, na hilo husababisha mtu awe na kazi nyingi zisizokamilika. Jaribu kutumia mapendekezo haya mawili:

    1. Panga ratiba inayofaa, na ushikamane nayo.

    2. Tambua na urekebishe mtazamo wowote unaosababisha kuahirisha mambo.

Uwe na Maisha Yenye Usawaziko

“Ni afadhali konzi moja ya pumziko kuliko konzi mbili za kazi ngumu na kukimbiza upepo.” —MHUBIRI 4:6.

Maana yake: Watu wanaopenda kufanya kazi kupita kiasi wanaweza kukosa faida ya ‘kazi yao ngumu.’ Huenda wasiwe na wakati au nguvu za kufurahia matunda ya kazi yao.

  • Uwe na maoni yanayofaa kuhusu kazi na pesa. Kuwa na pesa nyingi hakumaanishi kwamba utakuwa na furaha zaidi au utapunguza mkazo. Zinaweza kuwa chanzo cha mkazo zaidi na kukosa furaha. Mhubiri 5:12 inasema, “Wingi alionao tajiri haumruhusu kulala usingizi.” Kwa hiyo, jitahidi kuishi kulingana na mapato yako.

  • Tenga wakati wa kustarehe. Utapunguza mkazo ukifanya mambo unayofurahia. Hata hivyo, burudani zinazofanya mwili wako usijishughulishe kama vile kutazama televisheni, hazitakusaidia.

  • Tumia teknolojia kwa kiasi. Epuka kusoma mara kwa mara barua pepe, jumbe au kutumia muda mwingi kwenye mitandao ya kijamii. Epuka kusoma barua pepe zinazohusiana na kazi baada ya muda wa kazi isipokuwa iwe ni lazima kufanya hivyo.

Tunza Afya Yako

“Mazoezi ya kimwili ni yenye faida.” —1 TIMOTHEO 4:8.

Maana yake: Kufanya mazoezi mara kwa mara kunaboresha afya.

  • Sitawisha mazoea yanayofaa. Mazoezi ya kimwili yanaweza kufanya ujihisi vizuri na kuboresha njia yako ya kushughulikia mkazo. Kula vyakula vyenye lishe na ujitahidi kuepuka zoea la kutokula chakula. Pia, hakikisha unalala vya kutosha.

  • Mazoea yenye kudhuru kama vile kutumia dawa za kulevya, sigara au kunywa kileo kupita kiasi si suluhisho la kuondoa mkazo. Mazoea hayo yatakuongezea mkazo, labda kwa kukusababishia matatizo ya afya na hata kupoteza pesa zako.

  • Ukilemewa na mkazo kupita kiasi mwone daktari. Kupata msaada wa kitiba si ishara ya udhaifu.

Panga Mambo ya Kutanguliza

“Mhakikishe mambo muhimu zaidi.” —WAFILIPI 1:10.

Maana yake: Chunguza kwa uangalifu mambo unayotanguliza.

  • Orodhesha kazi zako kwa kuanza na zilizo muhimu zaidi. Hilo litakusaidia kukazia fikira kazi zinazopaswa kufanywa haraka, kujua zile unazohitaji kuwagawia wengine na ambazo hazihitaji kufanywa.

  • Kwa juma moja, jaribu kufuatilia jinsi unavyotumia muda wako. Kisha fikiria jinsi ya kuutumia vizuri. Kadiri unavyotumia wakati vizuri ndivyo utakavyohisi huru zaidi.

  • Tenga muda wa kupumzika. Hata kupumzika kwa muda mfupi kunaweza kuburudisha na kupunguza mkazo.

Tafuta Msaada

“Mahangaiko yaliyo moyoni mwa mtu huulemea moyo, lakini neno jema huuchangamsha.”—METHALI 12:25.

Maana yake: Maneno ya fadhili na huruma kutoka kwa wengine yanaweza kukuburudisha.

  • Zungumza na mtu anayekuelewa kuhusu mambo yanayokupa mkazo. Rafiki unayemwamini anaweza kukusaidia uone mambo kwa njia tofauti au hata upate suluhisho kwa njia ambayo hukufikiria. Kutua mzigo huo kutafanya ujihisi vizuri.

  • Omba msaada. Je, unaweza kumwomba mtu mwingine afanye kazi hiyo au mshirikiane kuifanya?

  • Ikiwa mfanyakazi mwenzako ndiye anayesababisha upate mkazo, tafuta mbinu za kuboresha hali hiyo. Kwa mfano, je, unaweza kumwambia kwa njia ya fadhili na busara, jinsi matendo yake yanavyokuathiri? (Methali 17:27) Mbinu hiyo isipofaulu, punguza muda unaotumia na mtu huyo.

Sitawisha Uhusiano Mzuri na Mungu

“Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—MATHAYO 5:3.

Maana yake: Tukiwa wanadamu, tuna uhitaji mwingine zaidi ya chakula, mavazi na makazi. Tunahitaji kuwa na uhusiano mzuri na Mungu. Ili tuwe na furaha, tunapaswa kutambua uhitaji huo na kuhakikisha tunautimiza.

  • Sala inaweza kukusaidia sana. Mungu anakualika ‘umtupie mahangaiko yako yote, kwa sababu yeye anakujali.’ (1 Petro 5:7) Sala na kutafakari kwa kina kuhusu mambo yanayofaa kunaweza kukupatia amani ya moyoni.—Wafilipi 4:6, 7.

  • Soma mambo ambayo yatakusaidia uwe na uhusiano mzuri na Mungu. Kanuni zilizozungumziwa kwenye gazeti hili, zinatoka katika Biblia, ambayo iliandikwa ili kukusaidia uwe na uhusiano mzuri na Mungu. Kanuni hizo zitakusaidia upate “hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri.” (Methali 3:21) Unaweza kujiwekea lengo la kusoma Biblia. Kitabu cha Methali kinaweza kuwa kitabu kizuri kuanza kusoma.