Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA KUMI NA INE

Yale Unayopaswa Kufanya ili Familia Yako Iwe Yenye Furaha

Yale Unayopaswa Kufanya ili Familia Yako Iwe Yenye Furaha
  • Mwanaume aliyeoa anapaswa kutimiza mambo gani ili awe bwana muzuri?

  • Namna gani mwanamuke aliyeolewa anaweza kutimiza daraka lake vizuri?

  • Ili kuwa muzazi muzuri inaomba kufanya nini?

  • Watoto wanaweza kufanya nini ili familia iwe yenye furaha?

1. Kila mumoja anapaswa kufanya nini ili familia iwe yenye furaha?

YEHOVA MUNGU anataka familia yako iwe yenye furaha. Katika Biblia, Neno lake, utakuta mashauri ambayo Mungu anamupatia kila mumoja katika familia. Tena, inaonyesha daraka ambalo Mungu anamupatia kila mumoja wao. Kila mumoja katika familia akitimiza yale ambayo Mungu anamuomba, familia itakuwa yenye furaha. Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!”​—Luka 11:28.

2. Ili familia iwe yenye furaha, kila mumoja anapaswa kwanza kukubali nini?

2 Ili familia iwe yenye furaha, kila mumoja anapaswa kwanza kukubali kama Yehova, ambaye Yesu alimuita “Baba Yetu,” ndiye aliyeanzisha familia. (Mathayo 6:9) Kwa sababu ni yeye aliyeanzisha familia duniani, hakika anajua ni nini inayoweza kufanya familia iwe yenye furaha. (Waefeso 3:14, 15) Sasa Biblia inafundisha nini juu ya daraka la kila mumoja katika familia?

MUNGU NDIYE ALIYEANZISHA FAMILIA

3. Kupatana na Biblia, familia ilianza namna gani, na namna gani tunajua kama familia ilianza hivyo?

3 Yehova aliumba watu wa kwanza, Adamu na Eva, akawaunganisha wakawa bwana na bibi. Aliwaweka katika paradiso nzuri hapa duniani, bustani ya Edeni, na akawaambia wazae watoto. Yehova aliwaambia hivi: ‘Zaeni, muwe wengi, mujaze dunia.’ (Mwanzo 1:26-28; 2:18, 21-24) Hii si hadisi ao jambo la kuwazia tu; Yesu alionyesha kama yale ambayo kitabu cha Mwanzo kinasema juu ya mwanzo wa familia ni kweli. (Mathayo 19:4, 5) Hata ikiwa leo tuna matatizo mengi na maisha hayako kama vile Mungu alivyokusudia, tunaweza kuwa na familia yenye furaha.

4. (a) Kila mumoja katika familia anaweza kufanya nini ili familia iwe yenye furaha? (b) Sababu gani ni lazima kujifunza maisha ya Yesu ili familia iwe yenye furaha?

4 Ikiwa kila mumoja katika familia anaonyesha upendo kama Mungu, familia inaweza kuwa yenye furaha. (Waefeso 5:1, 2) Lakini, namna gani tunaweza kumuiga Mungu ambaye hatumuoni? Tunaweza kujua namna Yehova anavyotenda kupitia Mwana wake muzaliwa wa kwanza aliyetuma hapa duniani. (Yohana 1:14, 18) Alipokuwa hapa duniani, Mwana huyo, Yesu Kristo, alimuiga sana Baba yake wa mbinguni, kwa hiyo, kumuona na kumusikiliza Yesu ilikuwa sawa na kuwa pamoja na Yehova na kumusikiliza. (Yohana 14:9) Basi, ikiwa kila mutu katika familia anajifunza namna Yesu alivyoonyesha upendo na kuiga mufano wake, familia inaweza kuwa na furaha kabisa.

YESU NI MUFANO KWA WANAUME WALIOOA

5, 6. (a) Ni fundisho gani wanaume waliooa wanaweza kupata wanapoangalia namna Yesu alivyolitendea kutaniko? (b) Mutu anapaswa kufanya nini ili asamehewe zambi zake?

5 Biblia inasema kama wanaume wanapaswa kuwatendea bibi zao namna Yesu alivyowatendea wanafunzi wake. Sikia yale Biblia inasema: ‘Waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake. Vivyo hivyo, waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Yeye anayependa muke wake anajipenda mwenyewe, kwa maana hakuna mutu anayeuchukia mwili wake kwa vyovyote; bali huulisha na kuutunza kwa upendo, kama vile Kristo anavyolitendea kutaniko.’​Waefeso 5:23, 25-29.

6 Namna Yesu alivyowapenda wanafunzi wake ni mufano muzuri kwa wanaume. Yesu ‘aliwapenda mupaka mwisho,’ alitoa uzima wake kwa ajili yao, hata ikiwa hawakuwa wakamilifu. (Yohana 13:1; 15:13) Vilevile, wanaume wanashauriwa hivi: ‘Endeleeni kuwapenda wake zenu nanyi musiwakasirikie kwa uchungu.’ (Wakolosai 3:19) Ni nini itakayomusaidia mwanaume kufuata shauri hilo, zaidi sana ikiwa wakati mwingine bibi yake hatendi kwa hekima? Anapaswa kukumbuka kama yeye pia ni mukosaji na kukumbuka kile Mungu anamuomba kufanya ili amusamehe. Anamuomba kufanya nini? Anapaswa kusamehe kila mutu anayemukosea, hata bibi yake pia. Bibi yake anapaswa pia kufanya hivyo. (Mathayo 6:12, 14, 15) Je, unaelewa sasa sababu gani watu fulani wanasema kama ndoa yenye furaha ni ile bwana na bibi wako tayari kusameheana?

7. Yesu alijua nini juu ya wanafunzi wake, na hilo linawafundisha wanaume waliooa nini?

7 Wanaume wanapaswa pia kujua kama sikuzote Yesu alikuwa anawahangaikia wanafunzi wake. Alijua uzaifu wao na kile mwili wao ulikuwa ukiomba. Kwa mufano, siku fulani walipokuwa wenye kuchoka, aliwaambia: ‘Njooni, ninyi wenyewe faragani katika mahali pasipo na watu mupumuzike kidogo.’ (Marko 6:30-32) Wanaume waliooa wanapaswa kuhangaikia bibi zao hivyo. Biblia inasema kama wao ni ‘chombo zaifu zaidi’ na wanaume wanaamuriwa wawape “heshima.” Sababu gani? Kwa sababu wanaume na wanawake wana ‘pendeleo lilelile lisilostahiliwa la uzima.’ (1 Petro 3:7) Wanaume wanapaswa kukumbuka kama uaminifu wa mutu ndio unaomufanya awe wa lazima machoni pa Mungu, wala si kuwa mwaunaume ao mwanamuke.​—Zaburi 101:6.

8. (a) Namna gani mwanaume ‘anayemupenda muke wake, anajipenda mwenyewe’? (b) Inamaanisha nini kusema kama bwana na bibi yake ni ‘mwili mumoja’?

8 Biblia inasema mwanaume ‘anayemupenda muke wake anajipenda mwenyewe.’ Kwa sababu bwana na bibi yake ‘si wawili tena, bali mwili mumoja,’ kama Yesu alivyosema. (Mathayo 19:6) Ndiyo sababu hawapaswi kufanya kitendo cha ndoa na mutu mwingine yeyote. (Methali 5:15-21; Waebrania 13:4) Wataepuka kufanya hivyo ikiwa kila mumoja anahangaikia pia mahitaji ya mwenzake kuliko mahitaji yake mwenyewe. (1 Wakorintho 7:3-5) Jambo lingine la kukumbuka ambalo ni la lazima ni hili: ‘Hakuna mutu anayeuchukia mwili wake kwa vyovyote; bali huulisha na kuutunza kwa upendo.’ Wanaume waliooa wanapaswa kuwapenda bibi zao kama wanavyojipenda wenyewe, wanapaswa pia kukumbuka kama watatoa hesabu kwa Yesu Kristo, aliye kichwa chao.​—Waefeso 5:29; 1 Wakorintho 11:3.

9. Andiko la Wafilipi 1:8, linazungumuzia sifa gani ya Yesu, na sababu gani wanaume wanapaswa kuonyesha bibi zao sifa hiyo?

9 Mutume Paulo alizungumuzia ‘upendo mwororo alio nao Kristo Yesu.’ (Wafilipi 1:8) Sifa hiyo ilikuwa yenye kuburudisha, iliwavutia wanawake waliokuwa wanafunzi wake. (Yohana 20:1, 11-13, 16) Nao wanawake walioolewa wanatamani sana bwana zao wawapende kwa wororo.

YESU NI MUFANO KWA WANAWAKE WALIOOLEWA

10. Namna gani Yesu ni mufano kwa wanawake walioolewa?

10 Familia ni kama kikundi cha watu wenye kufanya kazi pamoja, ili kazi ifanywe vizuri kunapaswa kuwe na kiongozi ao kichwa. Hata Yesu ana Yule aliye Kichwa chake na anamutii. “Kichwa cha Kristo ni Mungu,” kama vile ‘kichwa cha mwanamuke ni mwanamume.’ (1 Wakorintho 11:3) Namna Yesu anavyotii ukichwa wa Mungu ni mufano muzuri kwa sababu sisi wote tuna yule aliye kichwa, yaani, mukubwa ambaye tunapaswa kutii.

11. Mwanamuke anapaswa kujiendesha namna gani mbele ya bwana yake, na mwenendo wake unaweza kuwa na matokeo gani?

11 Wanaume ni watu wasio wakamilifu, ndio sababu wao pia wanafanya makosa, na mara nyingi wanaongoza familia zao isivyofaa. Kwa hiyo, mwanamuke aliyeolewa anapaswa kufanya nini? Hapaswi kumuzarau bwana yake ao kujaribu kumunyanganya ukichwa. Mwanamuke anapaswa kukumbuka kama roho ya utulivu na upole ina bei sana machoni pa Mungu. (1 Petro 3:4) Akionyesha roho hiyo itakuwa vyepesi kwake kutii kama Mungu anavyomuomba, hata katika hali ngumu. Tena, Biblia inasema hivi: ‘Muke anapaswa kumuheshimu sana mume wake.’ (Waefeso 5:33) Basi atafanya nini ikiwa bwana yake anakataa kukubali ukichwa wa Kristo? Biblia inashauria wanawake walioolewa hivi: “Jitiisheni kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kushuhudia kwa macho mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa.”​1 Petro 3:1, 2.

12. Sababu gani si vibaya mwanamuke kueleza mawazo yake kwa heshima?

12 Iwe bwana ni Mukristo ao hapana, mawazo ya bibi yake yanaweza kutofautiana na yake, lakini ikiwa mwanamuke huyo anaeleza mawazo yake kwa heshima, hilo halionyeshi kama anamuvunjia bwana yake heshima. Anaweza kuwa na mawazo mazuri ambayo yanaweza kufaidi familia ikiwa bwana yake anamusikiliza. Abrahamu hakukubali wazo la Sara, bibi yake, juu ya namna ya kumaliza tatizo fulani lililokuwa katika familia yao, lakini Mungu alimuambia Abrahamu: “Sikiliza sauti yake.” (Mwanzo 21:9-12) Hakika, bwana anapochukua uamuzi, bibi yake anapaswa kutii uamuzi huo na kumuunga mukono, ikiwa uamuzi huo hauvunji sheria ya Mungu.​—Matendo 5:29; Waefeso 5:24.

Sara aliwawekea wanawake walioolewa mufano gani muzuri?

13. (a) Andiko la Tito 2:4, 5 linawashauri wanawake walioolewa wafanye nini? (b) Biblia inasema nini juu ya kutengana na kuvunja ndoa?

13 Mwanamuke aliyeolewa anaweza kutimiza daraka lake katika njia nyingi ili kusaidia familia. Kwa mufano, Biblia inasema kama wanawake walioolewa wanapaswa ‘kuwapenda waume zao, kuwapenda watoto wao, kuwa na utimamu wa akili, safi kiadili, wafanyakazi nyumbani, wema, wakijitiisha kwa waume zao wenyewe.’ (Tito 2:4, 5) Bibi ambaye pia ni mama anayefanya hivyo, sikuzote atapendwa na kuheshimiwa na bwana yake na watoto wake. (Methali 31:10, 28) Lakini kwa sababu ndoa ni muungano wa watu wawili wasio wakamilifu, matatizo fulani yaliyo magumu sana yanaweza kuwafanya watengane ao wavunje ndoa. Biblia inasema kama kuna mambo fulani yanayoweza kufanya bwana na bibi watengane. Hata hivyo, kutengana si jambo la muchezo, kwa sababu Biblia inashauri hivi: ‘Muke hapaswi kuondoka kwa mume wake; na mume hapaswi kumuacha muke wake.’ (1 Wakorintho 7:10, 11) Kwa upande mwingine, Biblia inamuruhusu mutu kuvunja ndoa ikiwa tu mumoja anafanya uasherati.​—Mathayo 19:9.

YESU NI MUFANO MUZURI KWA WAZAZI

14. Yesu aliwatendea watoto namna gani, na watoto wanataka wazazi wao wafanye nini?

14 Namna Yesu alikuwa akiwatendea watoto ni mufano muzuri kwa wazazi. Siku fulani walijaribu kuwazuia watoto wadogo wasimukaribie, Yesu alisema hivi: ‘Waacheni watoto wachanga waje kwangu; musijaribu kuwazuia.’ Kisha Biblia inasema kama ‘aliwachukua watoto akawakumbatia na kuanza kuwabariki, akiweka mikono yake juu yao.’ (Marko 10:13-16) Kwa sababu Yesu alipitisha wakati pamoja na watoto, je, wewe pia haupaswi kufanya hivyo na watoto wako? Wanahitaji upitishe wakati mwingi pamoja nao. Inakuomba uchukue wakati wa kuwafundisha, kwani Yehova anawaomba wazazi wafanye hivyo.​—Kumbukumbu la Torati 6:4-9.

15. Wazazi wanaweza kufanya nini ili kuwalinda watoto wao?

15 Kwa sababu dunia hii inaendelea kuharibika, watoto wana lazima ya ulinzi wa wazazi wao ili wasiangukie katika mikono ya watu wabaya, kama vile wale wanaotaka kuwatendea vibaya kingono. Wazia namna Yesu alivyowalinda wanafunzi wake ambao aliwapenda sana na hata kuwaita wanafunzi wake “watoto wadogo.” Alipokamatwa ili auawe alifanya yote ili wanafunzi wake watoroke. (Yohana 13:33; 18:7-9) Kwa kuwa wewe ni muzazi, unapaswa kufungua macho ili kuona njia ambazo Ibilisi anatumia ili kujaribu kuwaharibisha watoto wako. Unapaswa kuwaonya mbele ya wakati. * (1 Petro 5:8) Leo hii mwenendo wa watoto na pia hali yao ya kimwili na ya kiroho viko katika hatari kuliko ilivyokuwa zamani.

Wazazi wanaweza kujifunza nini wanapoangalia namna Yesu alivyokuwa akiwatendea watoto?

16. Wazazi wanaweza kujifunza nini wanapoangalia namna Yesu alivyokuwa akiwatendea wanafunzi wake walipokosea?

16 Usiku uliotangulia kifo cha Yesu, wanafunzi wake walibishana ili kujua ni nani aliye mukubwa kati yao. Yesu hakuwakasirikia, lakini kwa upendo aliendelea kufikiri nao kwa maneno na kwa matendo. (Luka 22:24-27; Yohana 13:3-8) Ikiwa wewe ni muzazi, je unaona namna unaweza kuiga mufano wa Yesu unapolea watoto wako? Ni kweli, inaomba kuwapa adabu, lakini inaomba kufanya hivyo kwa “kiwango kinachofaa” wala si kwa hasira. Si vizuri kutoa maneno bila kuwaza, maneno hayo yanaweza kuwa kama “upanga unaochoma.” (Yeremia 30:11; Methali 12:18) Unapaswa kumupa mutoto adabu katika njia ambayo, mwishowe, ataona kama kweli ulikuwa ukimusaidia.​—Waefeso 6:4; Waebrania 12:9-11.

YESU NI MUFANO KWA WATOTO

17. Yesu aliwawekea watoto mufano gani muzuri wa kuiga?

17 Je, watoto wanaweza kupata faida wakiiga mufano wa Yesu? Ndiyo! Mwenendo wa Yesu ulionyesha namna watoto wanapaswa kuwatii wazazi wao. Alisema: ‘Kama vile Baba alivyonifundisha, ndivyo ninavyosema. Sikuzote mimi hufanya mambo yanayomupendeza.’ (Yohana 8:28, 29) Yesu alimutii Baba yake wa mbinguni, na Biblia inawaambia watoto wawatii wazazi wao. (Waefeso 6:1-3) Hata ikiwa Yesu alikuwa mutoto mukamilifu, aliwatii wazazi wake, Yosefu na Maria, ambao hawakuwa wakamilifu. Hakika, utii wake ulifanya kila mutu katika familia yao awe na furaha!​—Luka 2:4, 5, 51, 52.

18. Sababu gani Yesu alimutii Baba yake wa mbinguni sikuzote, na ni nani anayefurahi watoto wanapowatii wazazi wao?

18 Je, kuna mambo ambayo watoto wanaweza kufanya ili kumuiga Yesu na kuwafurahisha hivyo wazazi wao? Ni kweli kama wakati fulani watoto wanaona kuwa ni vigumu kuwatii wazazi wao, lakini Mungu anataka watoto watii wazazi wao. (Methali 1:8; 6:20) Sikuzote Yesu alikuwa anatii Baba yake wa mbinguni, hata katika hali ngumu. Siku moja, Mungu alitaka Yesu afanye jambo fulani ngumu sana, Yesu alisema: “Niondolee kikombe hiki [jambo ambalo Mungu alitaka].” Hata hivyo, Yesu alifanya mapenzi ya Mungu, kwa sababu alielewa kama Baba yake anajua ni nini lililo jambo nzuri la kufanya wakati huo. (Luka 22:42) Watoto wanapojifunza kutii, watafurahisha wazazi wao na Baba yao wa mbinguni. *​—Methali 23:22-25.

Vijana wanapaswa kukumbuka nini wanaposhawishiwa?

19. (a) Namna gani Shetani anawashawishi watoto? (b) Wazazi watajisikia namna gani ikiwa watoto wao wanakuwa na mwenendo mubaya?

19 Ibilisi alimushawishi Yesu, hivyo atawashawishi pia vijana wafanye mambo mabaya. (Mathayo 4:1-10) Shetani Ibilisi anatumia marafiki ili kuwakaza vijana wengine kufanya mambo mabaya, mikazo hiyo inaweza kuwa nguvu. Basi ni lazima sana watoto waepuke kufanya urafiki na wale wanaotenda mabaya! (1 Wakorintho 15:33) Dina, binti ya Yakobo, alirafikiana na watu wasiomuabudu Yehova, na jambo hilo lilimuletea matatizo makubwa. (Mwanzo 34:1, 2) Wazia namna wengine katika familia watahuzunika ikiwa mumoja wao anaangukia katika mambo ya uasherati!​—Methali 17:21, 25.

JAMBO LA LAZIMA SANA ILI FAMILIA IWE YENYE FURAHA

20. Ili kuwa na familia yenye furaha, kila mumoja anapaswa kufanya nini?

20 Kila mumoja katika familia akitumia mashauri ya Biblia, ni vyepesi kushindana na matatizo yanayotokea katika familia. Hilo ndilo jambo la lazima sana ili familia iwe yenye furaha. Kwa hiyo, wanaume muwapende bibi zenu na muwatendee kama vile Yesu anavyolitendea kutaniko lake. Wanawake, mutii ukichwa wa bwana zetu na mufuate mufano wa mwanamuke anayezungumuziwa katika Methali 31:10-31. Wazazi, muwalee vizuri watoto wenu. (Methali 22:6) Ninyi baba, ‘musimamie nyumba zenu kwa njia nzuri.’ (1 Timotheo 3:4, 5; 5:8) Ninyi watoto, muwatii wazazi wenu. (Wakolosai 3:20) Katika familia hakuna mutu aliye mukamilifu kwa sababu sisi wote tunafanya makosa. Kwa hiyo, muwe wanyenyekevu na muombane musamaha.

21. Ni mambo gani mazuri sana yanayotungojea, na namna gani tunaweza kuwa na familia yenye furaha leo?

21 Hakika, Biblia ina mashauri mengi yenye faida juu ya familia. Tena, inatufundisha juu ya dunia mupya ya Mungu na paradiso itakayokuwa hapa duniani itakayojaa watu wenye furaha wanaomuabudu Yehova. (Ufunuo 21:3, 4) Hayo ni mambo mazuri sana yanayotungojea! Lakini hata sasa, tunaweza kuwa na familia yenye furaha kwa kutumia mashauri ya Mungu yanayopatikana katika Neno lake, Biblia.

^ fu. 15 Ili kujua namna ya kuwalinda watoto, soma Sura ya 32 ya kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 18 Mutoto hatakubali kutii ikiwa muzazi anamuomba kuvunja sheria ya Mungu.​—Matendo 5:29.