Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

 TUIGE IMANI YAO | YOSEFU

‘Tafazali, Musikilize Ndoto Hii’

‘Tafazali, Musikilize Ndoto Hii’

YOSEFU aliangalia sana upande wa mashariki, akitamani kuponyoka katika kikundi cha watu wanaosafiri pamoja naye. Mahali fulani nyuma ya milima hiyo, lakini si mbali sana, ndiko nyumbani kwao katika Hebroni. Baba yake, Yakobo, alikaa nyumbani mangaribi hiyo akiwa mwenye kutulia, bila kujua kabisa kilichomufikia mwana wake mupendwa. Lakini sasa Yosefu hatarudi tena kwa baba yake; kwa vyovyote kijana huyo anajua kwamba hatauona tena uso wa baba yake mupendwa mwenye kuzeeka. Wafanyabiashara walimuona Yosefu walipokuwa wakiongoza ngamia zao kwenye njia ndogo iliyotumiwa sana inayoelekea katika barabara ya kusini. Sasa Yosefu alikuwa mutu wao, na hawangemuachilia tena. Kwa wafanyabiashara hao, kijana huyo alikuwa kama muzigo wao wa bei sana wa gundi yenye harufu nzuri ao mafuta, biashara ya maana ambayo ingewaletea faida katika inchi ya Misri iliyokuwa mbali sana.

Inawezekana Yosefu hakuwa na miaka zaidi ya 17. Umuwazie anapogeuka na akifungua macho kidogo ili kujikaza kuangalia anga upande wa mangaribi, ambapo jua lilianza kutua ngambo ya Bahari Kubwa. Anajaribu kuelewa namna maisha yake yalibadilika sana na kuwa mabaya. Ilikuwa vigumu kuamini kwamba ndugu zake wa damu moja walitaka kumuua na kisha wamemuuzisha kama mutumwa. Ilikuwa vigumu kwa Yosefu kuzuia machozi yake. Hakujua wakati wake unaokuja utakuwa namna gani.

Yosefu alipoteza uhuru wake lakini hakupoteza imani yake

Namna gani Yosefu aliingia katika hali ngumu kama hiyo? Na tunaweza kujifunza nini kutokana na imani ya kijana huyo aliyetendewa vibaya na kukataliwa na watu wa familia yake mwenyewe?

ALIKOMALIA KATIKA FAMILIA NGUMU

Yosefu alitoka katika familia kubwa, lakini haikuwa yenye furaha na umoja. Habari ya Biblia juu ya familia ya Yakobo inaonyesha waziwazi matokeo mabaya ya kuoa wanawake wengi. Mungu aliruhusu matendo hayo yaliyokuwa yametia mizizi kati ya watu wake mupaka wakati Mwana wake aliweka sheria mupya ya kuoa mwanamuke mumoja. (Mathayo 19:4-6) Yakobo alikuwa na watoto 14 hivi aliozaa na wanawake ine tofauti, ni kusema, bibi zake wawili, Lea na Raheli, na wajakazi wao, Zilpa na Bilha. Tangu mwanzo, Yakobo alikuwa anamupenda Raheli aliyekuwa na sura nzuri. Hakuwa anamupenda Lea, dada mukubwa wa Raheli, ambaye alidanganywa ili amuoe. Ushindani mukali ulidumu kwa muda murefu kati ya wanawake hao wawili, na hilo lilifanya wivu uenee kati ya watoto wa familia hiyo.—Mwanzo 29:16-35; 30:1, 8, 19, 20; 37:35.

Raheli alifanya muda murefu bila kuzaa, na mwishowe wakati alizaa Yosefu, Yakobo alimutendea mwana huyo wa uzee kwa njia ya pekee. Kwa mufano, wakati familia ilikuwa njiani wakikaribia hatari ya kukutana na Esau, ndugu ya Yakobo aliyekuwa  muuaji, Yakobo aliweka Raheli na Yosefu mahali salama nyuma ya watu wote wa familia. Siku hiyo yenye kuogopesha ilipaswa kuwa na matokeo makubwa juu ya Yosefu. Wazia namna alijisikia asubuhi hiyo alipokuwa akifikiri, macho yake yakiwa yamefunguliwa kwa mushangao. Hakuelewa sababu gani baba yake mwenye kukomaa sana lakini mwenye nguvu alikuwa akitembea sasa kwa kuchechemea (boîter). Anapaswa kuwa alishangazwa sana kujua sababu: Baba yake alipambana na malaika mwenye nguvu usiku muzima! Sababu gani baba yake alifanya hivyo? Kwa sababu alipenda apate baraka kutoka kwa Yehova Mungu. Baraka ambayo Yakobo alipata ilikuwa ni kubadilisha jina lake kuwa Israeli. Taifa nzima lingechukua jina lake! (Mwanzo 32:22-31) Baadaye, Yosefu alijua kwamba watoto wa Israeli wangetokeza makabila ya taifa hilo!

Kisha, kijana Yosefu alijionea musiba macho kwa macho wakati mutu aliyependa sana katika utoto wake alimuacha mbele ya wakati. Mama yake alikufa wakati alikuwa anamuzaa ndugu yake mudogo, Benyamini. Baba yake aliomboleza sana kwa sababu ya kifo hicho. Fikiria Yakobo akipanguza kwa upendo machozi kwenye uso wa Yosefu, akimufariji kupitia tumaini lenye lilimufariji Abrahamu, tate (ao nkambo) yake. Yosefu alipaswa kuwa aliguswa moyo kujua kwamba siku moja Yehova atamufufua mama yake! Labda Yosefu alifikia kupenda sana Mungu mukarimu wa walio hai. (Luka 20:38; Waebrania 11:17-19) Kisha kumupoteza bibi yake, Yakobo aliendelea kuwa na upendo na huruma kuelekea watoto hao wanaume wawili, aliozaa na Raheli.—Mwanzo 35:18-20; 37:3; 44:27-29.

Watoto wengi wanaweza kuharibika ao kuwa na tabia mbaya wakitendewa kwa njia ya pekee hivyo; lakini Yosefu alijifunza sifa nyingi nzuri kutoka kwa wazazi wake, na alikomalisha imani yenye nguvu na pia uwezo mukubwa wa kutambua mema na mabaya. Alipokuwa na miaka 17, alikuwa muchungaji wa wanyama, akiwasaidia ndugu zake fulani wakubwa, na wakati huo alitambua matendo yao fulani mabaya. Alishawishiwa kuficha makosa yao ili kukubaliwa nao? Iwe hivyo ao hapana, alifanya yaliyokuwa sawa. Alimuelezea baba yake mambo hayo. (Mwanzo 37:2) Labda tendo hilo la uhodari ndilo lilimufanya Yakobo amutumainie mwana wake mupendwa. Huo ni mufano muzuri ambao vijana Wakristo wanaweza kufikiria! Wakati unajaribiwa kuficha zambi nzito ya mutu mwengine, labda mutu wa familia ao rafiki, ni jambo la hekima kumuiga Yosefu na kujulisha jambo hilo kwa watu walio na daraka la kumusaidia mutu aliyefanya makosa.—Mambo ya Walawi 5:1.

Tunaweza pia kupata somo kutokana na maisha ya familia ya Yosefu. Hata ikiwa Wakristo wa kweli leo hawaruhusiwe kuoa wanawake wengi, kuna familia  nyingi ambamo bibi ao bwana ana watoto wake, na watu wa familia wa bibi ao wa bwana ambao walikuja nao katika ndoa. Sisi wote tunaweza kujifunza kutokana na familia ya Yakobo kwamba upendeleo na ubaguzi vinaweza kuharibu umoja wa familia. Wazazi wenye hekima walio katika familia ambamo bibi ao bwana ana watoto wake wanafanya yote wanayoweza ili kuwahakikishia watoto wao na watoto waliokuja nao katika ndoa kwamba kila mumoja anapendwa. Wanapaswa kutolea kila mutoto zawadi ya pekee na kuonyesha kila mumoja wao kwamba anaweza kuchangia furaha ya familia.—Waroma 2:11.

WIVU UNAANZA

Yakobo alimupendelea Yosefu kwa sababu mutoto huyo alikuwa muaminifu na mutenda-haki

Yakobo alimuonyesha Yosefu heshima, labda kwa sababu ya bidii yake ya kutetea mambo yaliyo sawa. Alimushonea Yosefu nguo ya pekee. (Mwanzo 37:3) Mara nyingi nguo hiyo imeitwa koti lenye mistari ao koti la rangi nyingi, lakini hakuna uhakika mwingi juu ya maelezo hayo. Inawezekana ilikuwa kanzu ndefu yenye kuvutia, ambayo labda ilifika kwenye mwisho wa mikono na miguu. Inawezekana ilikuwa aina ya nguo yenye tajiri ao mwana wa mufalme angeweza kuvaa.

Ni kweli kwamba Yakobo hakuwa na nia mbaya, na Yosefu anapaswa kuwa aliguswa na tendo hilo lililoonyesha kwamba baba yake alimuona kuwa mutu wa maana na alimupenda. Lakini nguo hiyo ingemuletea shida kubwa. Kwanza, kumbuka kwamba kijana huyo alikuwa muchungaji wa wanyama. Hiyo inamaanisha kwamba alipaswa kufanya kazi ngumu ya mikono. Umuwazie kijana huyo akiwa mwenye kuvaa nguo hiyo ya kifalme anapotembea katika nyasi ndefu, anapopanda juu ya majiwe makubwa, ao anapojaribu kumutosha kondoo aliyepotea katika miti yenye miiba. Hata hivyo, jambo mbaya zaidi, ni kusema, tendo hilo la Yakobo la upendeleo lingekuwa na matokeo gani juu ya uhusiano kati ya Yosefu na ndugu zake?

Biblia inajibu hivi: ‘Ndugu zake walipoona kwamba baba yao alimupenda kuliko ndugu zake wote, wakaanza kumuchukia, nao hawakusema naye kwa amani.’ * (Mwanzo 37:4) Wivu wao unaweza kueleweka, lakini hawakuonyesha hekima walipojiacha waongozwe na chuki hiyo yenye kuua. (Methali 14:30; 27:4) Wakati fulani umejikuta ukiwa mwenye kujaa wivu mutu fulani anapopewa uangalifu ao pendeleo ambalo ulitaka? Kumbuka ndugu za Yosefu. Wivu wao uliwaongoza kufanya jambo ambalo lingewaletea huzuni kubwa baadaye. Mufano wao unawakumbusha Wakristo kwamba ni jambo la hekima ‘kushangilia pamoja na watu wanaoshangilia.’—Waroma 12:15.

Bila shaka, Yosefu aliona kwamba ndugu zake hawakuwa wanamupenda. Je, alificha nguo yake hiyo ya hali ya juu sana wakati ndugu zake walikuwa karibu ili wasiione? Inawezekana alishawishiwa kufanya hivyo. Hata hivyo, kumbuka kwamba Yakobo alitaka kanzu hiyo iwe ishara ya kwamba anamukubali Yosefu na anamupenda. Yosefu alipenda baba yake aendelee kumuamini, kwa hiyo aliendelea kuvaa nguo hiyo. Mufano wake unaweza kutusaidia. Hata ikiwa baba yetu wa mbinguni hana ubaguzi hata siku moja, wakati fulani anachagua wale wanaomutumikia kwa uaminifu na kuwapa pendeleo fulani. Zaidi ya hayo, anawaomba  wawe tofauti kabisa na ulimwengu huu muovu na usiokuwa na mwenendo muzuri. Kama vile kanzu ya pekee ya Yosefu, tabia ya Wakristo wa kweli inawafanya wawe tofauti na watu wanaowazunguka. Wakati fulani, tabia kama hiyo inachochea wivu na uadui. (1 Petro 4:4) Mukristo anaweza kuficha mambo yanayoweza kumutambulisha kwelikweli kuwa mutumishi wa Mungu? Hapana—Yosefu pia hakuficha kanzu yake.—Luka 11:33.

NDOTO ZA YOSEFU

Kisha muda mufupi, Yosefu aliota ndoto mbili zisizo za kawaida. Katika ndoto ya kwanza, Yosefu alijiona yeye na ndugu zake, kila mumoja alikuwa anafunga muganda wa mbegu. Lakini muganda wake ulisimama na miganda ya ndugu zake iliuzunguka muganda wake na kuuinamia. Katika ndoto ya pili, jua, mwezi, na nyota 11 vilimuinamia Yosefu. (Mwanzo 37:6, 7, 9) Yosefu angefanya nini juu ya ndoto hizo zisizo za kawaida na zenye maana?

Ndoto hizo zilitoka kwa Yehova Mungu. Zilikuwa za kiunabii, na Mungu alimuambia Yosefu aeleze habari ya ndoto hizo. Katika njia fulani, Yosefu alipaswa kufanya kama vile manabii wa wakati uliopita walivyofanya wakati walieleza ujumbe wa Mungu na hukumu juu ya watu wake wasiotii.

Kwa heshima, Yosefu aliwaambia ndugu zake hivi: ‘Tafazali, musikilize ndoto hii ambayo nimeota.’ Ndugu zake walisikia ndoto hiyo na hawakuipenda hata kidogo. Walijibu hivi: ‘Je, kwa kweli utakuwa mufalme juu yetu? Ao utatutawala?’ Habari hiyo inaendelea hivi: ‘Basi wakapata sababu mupya ya kumuchukia kwa sababu ya ndoto zake na maneno yake.’ Wakati Yosefu alielezea baba yake na ndugu zake ndoto ya pili, nayo pia haikuwapendeza. Habari hiyo inasema hivi: ‘Baba yake akamukemea na kumuambia: Ndoto hii ambayo umeota inamaanisha nini? Je, mimi na pia mama yako na ndugu zako kwa kweli tutakuja na kukuinamia?’ Lakini, Yakobo aliendelea kufikiria maneno hayo. Inawezekana Yehova alikuwa anazungumuza na kijana huyo?—Mwanzo 37:6, 8, 10, 11.

Yosefu hakuwa mutumishi wa Yehova wa kwanza wala wa mwisho aliyeombwa aeleze ujumbe wa kiunabii ambao haukuwa unapendwa na watu wengi na ambao hata ungemuletea mateso. Yesu alikuwa mujumbe mukubwa zaidi kati ya watu waliokuwa na ujumbe kama huo, na aliwaelezea wafuasi wake hivi: “Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa ninyi pia.” (Yohana 15:20) Wakristo wa miaka yote wanaweza kujifunza mambo mengi kutokana na imani na uhodari wa kijana Yosefu.

CHUKI INALIPUKA

Muda mufupi kisha hapo, Yakobo alimutuma kijana Yosefu katika safari. Ndugu zake wakubwa walikuwa wanachunga makundi ya wanyama upande wa kusini karibu na Shekemu, mahali walikuwa wameanzisha uadui mukubwa muda mufupi mbele ya hapo. Kwa kawaida, Yakobo alikuwa anawahangaikia watoto wake, kwa hiyo, alimutuma Yosefu aende aone ikiwa wako salama. Unaweza kufikiria namna Yosefu alijisikia? Alijua kwamba ndugu zake walimuchukia zaidi kuliko zamani! Wangemuona namna gani akija kwao kama vile musemaji wa baba yao? Hata hivyo, Yosefu alianza safari kwa sababu ya kumutii baba yake.—Mwanzo 34:25-30; 37:12-14.

Labda ilikuwa safari ndefu ya siku ine ao tano kwa miguu. Muji wa Shekemu ulikuwa kwenye kilometa 80 kaskazini mwa Hebroni. Lakini Yosefu alipofika Shekemu, walimuambia kwamba ndugu zake walienda Dothani, muji uliokuwa kwenye kilometa 22 ao zaidi upande wa kaskazini. Mwishowe wakati Yosefu alikaribia Dothani, ndugu zake walimuona akija kwa mbali. Mara moja, chuki yao ilipanda. Habari hiyo inaeleza hivi: ‘Wakasemezana: Tazama! Yule muota-ndoto anakuja. Basi na tumuue, tumutupe ndani ya moja la mashimo ya maji; halafu tutasema munyama mukali wa mwitu alimurarua. Ndipo tuone itakuwaje kwa ndoto zake.’ Lakini, Reubeni, aliwashawishi ndugu zake wamutupe Yosefu katika shimo akiwa muzima, akitumaini kwamba baadaye anaweza kumutosha ndani ya shimo hilo.—Mwanzo 37:19-22.

Bila kuwazia jambo lolote ambalo walikuwa wanapanga juu yake, Yosefu aliwakaribia ndugu zake, akiwazia kwamba watakutana kwa amani. Tofauti na hilo, ndugu zake wakamukamata! Kwa ukali, wakamutosha kanzu yake ya pekee, wakamukokota na kumutupa katika shimo la maji lenye kukauka. Yosefu akaanguka katika shimo hilo! Alipotulia kisha mushituko huo, alijaribu kutoka ndani, lakini hangeweza kutoka ndani kwa uwezo wake mwenyewe.  Aliona tu anga wakati sauti ya ndugu zake ilipofifia. Aliwalalamikia, na kuwabembeleza, lakini hawakumuhangaikia. Bila huruma, walikula chakula karibu na shimo hilo. Wakati Reubeni hakuwa hapo, walipanga tena kumuua kijana huyo, lakini Yuda aliwaomba wamuuzishe kwa wafanya-biashara waliokuwa wakipita kuliko kumuua. Muji wa Dothani ulikuwa kwenye barabara ya biashara iliyoenda Misri, na muda mufupi kisha Yuda kusema hivyo kikundi cha Waishmaeli na Wamidiani kikapita. Mbele Reubeni arudi, walitimiza mupango wao. Walimuuzisha ndugu yao kama mutumwa kwa shekeli 20. *Mwanzo 37:23-28; 42:21.

Yosefu alitetea mambo yaliyokuwa sawa, hata ikiwa ndugu zake walimuchukia

Sasa turudie kwenye maelezo ya mwanzo wa habari hii. Walipomuchukua Yosefu na kuenda naye upande wa kusini kupitia barabara inayoelekea Misri, alionekana kuwa amepoteza kila kitu. Alitenganishwa kinguvu na familia yake! Kwa miaka mingi, Yosefu hangejua kitu chochote juu ya familia yake, hangejua kitu chochote juu ya namna Reubeni ataumizwa wakati atarudia na kukuta ameenda, hangejua kitu chochote juu ya maumivu ya Yakobo wakati atabaki akiamini kwamba mwana wake mupendwa amekufa. Tena hangejua kitu chochote juu ya hali ya Isaka, tate (ao nkambo) yake, ambaye alikuwa angali muzima; na hangejua kitu chochote juu ya Benyamini, ndugu yake mupendwa, ambaye hangeona tena. Lakini, Yosefu alipoteza kila kitu?—Mwanzo 37:29-35.

Yosefu alibaki na kitu fulani ambacho ndugu zake hawangeweza kumunyanganya: imani yake. Alijua mambo mengi juu ya Mungu wake Yehova, na hakuna kitu ambacho kingemunyanganya jambo hilo. Kwa mufano, kuwa mbali na familia yake, mateso ya kukamatwa kuwa mutumwa na kufanya safari ndefu kuenda Misri, na kushushiwa heshima kwa kuuzishwa kuwa mutumwa kwa tajiri wa Misri anayeitwa Potifa, mambo hayo yote hayakumunyanganya imani yake. (Mwanzo 37:36) Imani ya Yosefu na kusudi lake la kubaki karibu na Mungu viliendelea kuwa nguvu hata ikiwa alipitia magumu kama hayo. Katika habari zitakazofuata, tutaona namna gani imani ya Yosefu ilimufanya awe tayari kutumiwa sana na Mungu wake, Yehova, na namna imani hiyo ilisaidia familia yake yenye haikuwa na umoja. Ni jambo la hekima kabisa tuige imani ya Yosefu!

^ fu. 15 Wachunguzi fulani wanasema kwamba ndugu za Yosefu waliona zawadi ambayo baba yao alimupatia Yosefu kuwa uhakika wa kwamba alitaka kumupatia kijana huyo haki ya muzaliwa wa kwanza. Walijua kwamba Yosefu alikuwa mutoto wa kwanza ambaye Yakobo alizaa na bibi aliyekuwa anapenda sana—bibi ambaye alipanga kuoa mbele. Zaidi ya hayo, Reubeni, mutoto wa kwanza wa Yakobo alilala na kijakazi aliyekuwa bibi wa baba yake, kwa kufanya hivyo alikosa heshima kwa baba yake na alipoteza haki yake ya muzaliwa wa kwanza.—Mwanzo 35:22; 49:3, 4.

^ fu. 25 Hata katika maelezo haya madogo, habari ya Biblia inaonekana kuwa ya kweli. Maandishi ya wakati huo yanaonyesha kwamba bei ya kawaida ya mutumwa huko Misri ilikuwa shekeli 20.