Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

 TUIGE IMANI YAO | YOSEFU

Namna Gani ‘Ninaweza Kufanya Ubaya Huu Mukubwa?’

Namna Gani ‘Ninaweza Kufanya Ubaya Huu Mukubwa?’

YOSEFU anapumua hewa nzito yenye joto, anasikia harufu ya maua ya yungiyungi na mimea mingine inayoota katika maji. Anaongozwa na kikundi cha wafanyabiashara, sasa wanapita katika mabonde ya nafasi kubwa kwenye muto Nile unagabulika katika sehemu nyingi. Wazia mustari wa wanaume hao wakiongoza ngamia zao katika njia ya maji kuelekea muji mwengine wa Misri, wakati kwa wakati wanashangazwa wanapoona ndege kulasitara ao kwarara wanaruka. Yosefu aliwaza tena juu ya nyumbani kwao alipokuwa katika maeneo yenye kuinuka ya Hebroni yenye upepo mukali, mamia ya kilometa mbali na kwao; sasa alikuwa katika ulimwengu mwengine.

Wazia makaku wakifanya makelele na kulalamika wakiwa juu ya miti ya mitende na miti ya tini. Walipokuwa wanapita, Yosefu hakuelewa mazungumuzo ya watu waliokutana nao. Labda alifanya yake yote ili kuelewa hata neno moja. Inawezekana alijifunza. Kama alivyojua, hangeweza tena kuona nyumbani kwao.

Yosefu alikuwa tu kijana, alikuwa na miaka 17 ao 18, lakini alikutana na magumu yenye yangeogopesha wanaume wengi wenye kukomaa. Ndugu zake mwenyewe walikuwa karibu kumuua, walikuwa na wivu sana kumuelekea kwa sababu baba yao alimupenda sana. Kuliko kumuua, walimuuzisha kwa wafanyabiashara waliokuwa wanapita. (Mwanzo 37:2, 5, 18-28) Sasa, kisha kusafiri kwa majuma, inawezekana furaha ya wafanyabiashara hao ilikuwa inaongezeka zaidi walipokuwa wanakaribia muji huo kwenye walitazamia kupata faida nyingi kwa kumuuzisha Yosefu na pia biashara yao ya maana. Yosefu alifanya nini ili asivunjike moyo na kupoteza tumaini? Na namna gani leo tunaweza kuzuia matatizo mbalimbali ya maisha na vizuizi mbalimbali visivunje imani yetu? Tunaweza kujifunza mambo mengi kupitia mufano wa Yosefu.

“YEHOVA ALIKUWA PAMOJA NA YOSEFU”

‘Basi Yosefu akapelekwa Misri, na Potifa, ofisa wa makao ya Farao, mukubwa wa walinzi, Mumisri, akamununua kutoka kwa Waishmaeli waliokuwa wamemuleta huko.’ (Mwanzo 39:1) Katika maneno hayo machache, habari ya Biblia inatusaidia kuwazia namna kijana huyo mwanaume alizarauliwa alipouzishwa tena. Alikuwa tu kama kitu! Tunaweza kumufikiria Yosefu akifuata mukubwa wake wa kazi, ofisa wa makao ya mufalme wa Misri, wote wawili wanapita katika barabara za muji zenye watu wengi na zenye kujaa maduka, wanaelekea kwenye makao ao nyumba mupya ya Yosefu.

Nyumba hiyo ilikuwa tofauti kabisa na kila nyumba Yosefu alikuwa amekwisha kuona. Alikomalia katika familia yenye kuhama-hama iliyoishi katika mahema. Walikuwa wanahama-hama na kulisha makundi yao ya kondoo. Huko Misri, Wamisri wote waliokuwa matajiri kama Potifa waliishi katika nyumba nzuri sana zilizopakwa rangi zenye kuangara. Watu wanaochimba vitu vya zamani wanasema kuwa Wamisri walipenda bustani zenye kuwa muzuri sana. Bustani hizo zilizungukwa na kuta na miti yenye kivuli na visima vyenye utulivu kwenye walipanda mafunjo, yungiyungi na mimea mingine yenye kukomaa ndani ya maji. Nyumba fulani zilijengwa nafasi yenye kufichwa katikati ya bustani. Nyumba hizo zilikuwa na baraza (véranda) za kuvutia hewa, madirisha za juu ili kuingiza hewa ndani ya nyumba, na vyumba vingi, kutia ndani chumba kikubwa cha kulia chakula na vyumba vya watumishi.

Yosefu alipendezwa sana na utajiri kama huo? Inaonekana hapana. Zaidi ya yote, labda alijisikia kuwa peke yake kabisa. Wamisri walikuwa wageni kwake katika luga, namna ya kuvaa, ya kujipamba— na hata zaidi katika mambo ya dini. Walikuwa wanaabudu miungu mbalimbali, walifanya mambo ya uchawi, na walipendezwa na kifo kwa njia isiyofaa na uzima kisha kifo. Hata hivyo, jambo moja lilimusaidia Yosefu ili asihangaishwe sana na hali ya kujisikia kuwa peke yake. Biblia inasema hivi: “Yehova alikuwa pamoja na Yosefu.” (Mwanzo 39:2) Kwa kweli, Yosefu alimuambia Mungu wake mambo yote aliyokuwa nayo moyoni. Biblia inasema kwamba ‘Yehova iko karibu na wote wanaomuitia.’ (Zaburi 145:18) Yosefu alifanya tena nini ili kumukaribia Mungu wake?

Kijana huyo mwanaume hakujiacha akose tumaini, na alijikaza kufanya kazi yake kwa uwezo wake wote. Alitenda mambo yaliyofanya Yehova amubariki, na bila kukawia alipendwa na mukubwa wake mupya wa kazi. Potifa aliona kama Yosefu, mutumishi wake kijana, alikuwa anabarikiwa na Yehova, Mungu wa watu wa familia yake, na kwa kweli baraka hizo zililetea nyumba ya Mumisri huyo utajiri mwingi. Polepole Yosefu alifikia kuheshimiwa sana na Potifa, mukubwa wake wa kazi, mupaka akatia kila kitu katika mikono ya kijana huyo mwanaume mwenye uwezo.—Mwanzo 39:3-6.

Yosefu ni mufano muzuri kwa vijana wanaomutumikia Mungu leo. Kwa mufano, wanapokuwa kwenye masomo, wakati fulani wanaweza kujikuta katika hali yenye kuonekana kuwa mupya na isiyokuwa ya kawaida. Wanaweza kujikuta wanazungukwa na watu wenye kuvutiwa na mambo ya uchawi, wasiokuwa na tumaini na mawazo mazuri juu ya maisha. Ikiwa unajikuta katika hali hiyo, kumbuka kwamba Yehova hajabadilika. (Yakobo 1:17) Bado anajionyesha kuwa pamoja na watu wote wenye kubakia waaminifu kwake na wenye kujikaza sana ili kutenda kwa njia inayomupendeza. Anawabariki sana, na atakubariki wewe pia.

Habari hiyo inatuambia kama wakati huo Yosefu alikuwa anakomaa. Kijana huyo akakuwa mwanaume “mwenye umbo nzuri na mwenye sura ya kupendeza.” Maneno hayo yanaonyesha kuwa hatari ilikuwa inamungojea, kwa sababu mara nyingi uzuri wa mwili unafanya watu wavutiwe na mutu kwa njia isiyofaa na bila yeye kutaka.

Bibi ya Potifa alimuangalia kwa uangalifu Yosefu, kijana mwaminifu

‘HAKUMUSIKILIZA’ HATA KIDOGO

Yosefu aliona uaminifu kuwa wa maana sana; lakini bibi ya Potifa hakuona vile. Tunasoma hivi: ‘Muke [ao bibi] wa bwana wake akaanza kuinua macho yake kumuelekea Yosefu na kusema: Lala na mimi.’ (Mwanzo 39:7) Yosefu alijaribiwa kuitika kishawishi cha mwanamuke huyo mupagani mwenye hakukuwa na haya? Biblia haituonyeshe sababu yoyote ya kusema kama Yosefu hakukuwa na tamaa ao vichocheo vya kawaida kwa vijana. Tena Biblia haituonyeshe kama mwanamuke huyo mwenye kubembelezwa sana wa ofisa mwenye utajiri na mamlaka nyingi alikuwa na sura isiyopendeza. Yosefu angewaza mukubwa wake wa kazi hatajua? Angeshawishiwa kuwaza angepata vitu vya kimwili akikubali kulala na mwanamuke huyo?

 Kwa kweli, hatuwezi kujua mambo yote Yosefu aliwaza. Lakini tuko na maelezo yaliyo wazi ya mambo yaliyokuwa katika moyo wake. Mambo yaliyokuwa katika moyo wake yanaonekana wazi kupitia jibu lake: ‘Tazama bwana wangu hajue kilicho na mimi nyumbani, na vyote ameviweka mukononi mwangu. Hakuna yeyote aliye mukubwa zaidi yangu katika nyumba hii, naye hakunizuilia chochote ila [ao isipokuwa] wewe, kwa sababu wewe ni muke [ao bibi] wake. Basi ninawezaje kufanya ubaya huu mukubwa na kwa kweli nimutendee Mungu zambi?’ (Mwanzo 39:8, 9) Wazia kijana huyo mwanaume akisema maneno hayo kwa bidii nyingi. Hata kuwaza juu ya tendo lenye mwanamuke huyo alitaka afanye kulimuumiza moyoni. Sababu gani?

Kama Yosefu alivyosema, mukubwa wake wa kazi alimutumainia. Potifa alikuwa ametia nyumba yake yote katika mikono ya Yosefu, hakumukataza kitu chochote isipokuwa bibi yake. Namna gani Yosefu angevunja tumaini hilo? Alichukia sana wazo hilo. Lakini kulikuwa sababu kubwa iliyomufanya achukizwe na wazo hilo: kumutendea zambi Yehova, Mungu wake. Kupitia wazazi wake, Yosefu alikuwa amejifunza mambo mengi kuhusu mawazo ya Mungu juu ya ndoa na uaminifu. Yehova alianzisha ndoa ya kwanza na alionyesha waziwazi mawazo yake. Mwanaume na mwanamuke walipaswa kuungana, na kuwa ‘mwili mumoja.’ (Mwanzo 2:24) Wale waliojaribu kuvunja muungano huo walikuwa katika hatari ya kupatwa na hasira ya Mungu. Kwa mufano, wanaume waliokaribia kumulala kwa nguvu bibi ya Abrahamu, aliyekuwa mama ya tate (nkambo) ya Yosefu, na bibi ya Isaka, tate ya Yosefu, walikaribia kupatwa na musiba. (Mwanzo 20:1-3; 26:7-11) Yosefu alikuwa amejifunza kuwa ni mubaya kulala na bibi ya mutu mwengine, na alikusudia kuishi kulingana na jambo hilo.

Bibi ya Potifa hakufurahia jibu la Yosefu. Wazia mutumwa huyo wa hali ya chini akimupinga mwanamuke huyo, na kuita jambo alilomuomba kuwa ‘ubaya mukubwa’! Hata hivyo, mwanamuke huyo hakuchoka. Labda kujisifu kwake na kiburi chake vilimufanya aumizwe moyoni, na kwa sababu hiyo aliamua kufanya yake yote ili Yosefu akubali ombi lake. Alionyesha roho iliyo kama ya Shetani, aliyemujaribu Yesu. Vishawishi vya Shetani vilishindwa, na kuliko kuchoka, alingojea “wakati mwingine unaofaa.” (Luka 4:13) Kwa hiyo, ni lazima watu waaminifu wakuwe imara na wasioyumba-yumba. Ni vile Yosefu alikuwa. Hata ikiwa hali hiyo ilirudia “siku baada ya siku,” hakubadilisha musimamo wake. Biblia inasema kama ‘hakumusikiliza’ bibi ya Potifa hata kidogo. (Mwanzo 39:10) Lakini mwanamuke huyo alikusudia kabisa kumuangusha.

Alitafuta wakati watumishi wote hawakukuwa ndani ya nyumba. Alijua kama Yosefu alipaswa kuja ndani ya nyumba ili kufanya kazi yake. Wakati Yosefu aliingia ndani ya nyumba, mwanamuke huyo alijaribu kumubana kwa nguvu. Alikamata nguo ya Yosefu na kumubembeleza kwa mara ya mwisho hivi: ‘Lala na mimi!’ Yosefu alitenda haraka. Alijiondoa katika mikono yake na kuondoka, lakini mwanamuke huyo alikamata sana nguo yake. Yosefu alijiondoa ndani ya nguo hiyo na kuiacha katika mikono yake na kisha akakimbia.—Mwanzo 39:11, 12.

Hilo linaweza kutukumbusha shauri hili la mutume Paulo lililoongozwa na roho ya Mungu: ‘Mukimbie uasherati!’ (1 Wakorintho 6:18) Yosefu aliwaachia Wakristo wote wa kweli mufano muzuri sana! Maisha yanaweza kutufanya tujikute katikati ya watu wasioheshimu sheria za Mungu juu ya mwenendo muzuri, lakini hilo halimaanishe kuwa tunapaswa kujiacha tushindwe na vishawishi vibaya. Hata ikiwa matokeo yatakuwa gani, tunapaswa kukimbia.

Katika hali ya Yosefu, matokeo yalikuwa mabaya sana. Bibi ya Potifa alitaka kulipiza kisasi. Mara moja, akaanza kulalamika, na kuita watumishi wengine wakuje ndani ya nyumba. Alisema kama Yosefu alitafuta kumulala kwa nguvu na kama Yosefu alikimbia wakati alilalamika. Aliweka nguo hiyo mupaka wakati bwana yake alirudia ili kumuonyesha kwamba Yosefu iko na kosa. Wakati Potifa alirudia nyumbani, alimuambia uongo huo, na kumuonyesha kuwa kosa ni lake kwa sababu ni yeye alileta mugeni huyo nyumbani kwao. Potifa alifanya nini? Biblia inasema hivi: “Hasira yake ikawaka”! Akamupeleka Yosefu kwenye gereza ili afungwe.—Mwanzo 39:13-20.

‘WALIMUFUNGA MIGUU KWA MINYORORO’

Hatujue mambo mengi juu ya magereza ya Wamisri wakati huo. Watu wanaochimbua vitu vya zamani wamepata mabomoko ya nafasi kama hizo, majengo makubwa yaliyo kama ngome yenye kuwa na magereza na vyumba vya chini ya udongo. Baadaye Yosefu alieleza nafasi hiyo kwa kutumia neno linalomaanisha moja kwa moja “tundu.” Hilo linaonyesha kwamba hiyo ilikuwa nafasi yenye giza na bila tumaini. (Mwanzo 40:15) Kitabu cha Zaburi kinaonyesha kuwa Yosefu alipatwa na mateso mengine: ‘Walimufunga  miguu kwa minyororo, na shingoni kwa nira ya chuma.’ (Zaburi 105:17, 18; Biblia Habari Njema) Nyakati fulani, Wamisri walitia wafungwa katika vizuizi vilivyofunga mikono yao nyuma kwenye viwiko vya mikono; wafungwa wengine walikuwa na mikufu ya chuma iliyofungwa kwenye shingo zao. Yosefu anapaswa kuwa aliteseka sana kwa kutendewa vibaya hivyo, wakati hakufanya jambo fulani mbaya lililostahili malipizi hayo!

Na zaidi ya hilo, mateso hayo hayakukuwa ya muda mufupi tu. Habari hiyo inasema kwamba Yosefu ‘aliendelea kuwa humo katika nyumba ya gereza.’ Alifanya miaka mingi katika nafasi hiyo mbaya! * Na hakujua ikiwa siku moja atafunguliwa. Siku hizo za kwanza zenye kuhuzunisha zilipofikia kuwa majuma, na kisha miezi, ni nini kilimusaidia Yosefu asifikie kuvunjika moyo na kukosa tumaini?

Habari hiyo inatupatia jibu hili lenye kutia moyo: ‘Yehova akaendelea kuwa pamoja na Yosefu, akazidi kumufanyia fazili zenye upendo.’ (Mwanzo 39:21) Kuta za gereza, minyororo, vyumba vya chini ya udongo visivyokuwa na mwangaza, vyote hivyo haviwezi kuzuia upendo mushikamanifu wa Yehova kuwafikia watumishi wake. (Waroma 8:38, 39) Tunaweza kumufikiria Yosefu akimuelezea baba yake wa mbinguni mateso yake katika sala na kupata amani na utulivu ambao ni “Mungu wa faraja yote” tu anaweza kutoa. (2 Wakorintho 1:3, 4; Wafilipi 4:6, 7) Yehova alimufanyia tena Yosefu nini? Tunasoma kuwa Yosefu aliendelea ‘kupata kibali machoni pa ofisa mukubwa wa nyumba ya gereza.’

Ni wazi kwamba wafungwa walipewa kazi ya kufanya, na Yosefu alitenda tena jambo fulani lililofanya Yehova amubariki. Alitumika sana, akifanya kwa bidii kazi yoyote alipewa na kuacha mambo mengine katika mikono ya Yehova. Kwa baraka ya Yehova, Yosefu alitumainiwa na kuheshimiwa, kama ilivyokuwa katika nyumba ya Potifa. Tunasoma hivi: ‘Ofisa mukubwa wa nyumba ya gereza akawatia mukononi mwa Yosefu wafungwa wote waliokuwa katika nyumba hiyo ya gereza; na yote waliyokuwa wakifanya humo yeye ndiye aliyekuwa akiagiza yafanywe. Yule ofisa mukubwa wa nyumba ya gereza hakukuwa akiangalia kitu chochote kilichokuwa mukononi mwake, kwa sababu Yehova alikuwa pamoja na Yosefu na yale aliyokuwa akifanya Yehova aliyafanikisha [ao aliyabariki].’ (Mwanzo 39:22, 23) Yosefu alifarijiwa kabisa kujua kama Yehova alikuwa anamuhangaikia!

Yosefu alifanya kazi kwa bidii katika gereza, na Yehova akamubariki

Katika maisha kunaweza kuwa kupanda na kushuka na hata ukosefu wa haki wenye kuhuzunisha sana, lakini tunaweza kujifunza mengi kutokana na imani ya Yosefu. Ikiwa tunabakia karibu na Yehova kupitia sala , tunaendelea kushika amri zake, na kujikaza sana kufanya mambo mema machoni pake, hilo litafanya Yehova atubariki.Katika hali ya Yosefu, Yehova alikuwa anamuwekea baraka nyingi hata zaidi, tutazungumuzia hilo katika habari zinazofuata za sehemu hii.

^ fu. 23 Biblia inaonyesha kama Yosefu alikuwa na miaka karibu 17 ao 18 wakati aliingia katika nyumba ya Potifa na kama alibakia humo siku nyingi mupaka akafikia kuwa kijana mukubwa, pengine alifanya miaka fulani humo. Alikuwa na miaka 30 wakati alifunguliwa kutoka katika gereza.—Mwanzo 37:2; 39:6; 41:46.