Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

TUIGE IMANI YAO | YOSEFU

“Je, Tafsiri Si za Mungu?”

“Je, Tafsiri Si za Mungu?”

YOSEFU alitembea katika njia iliyo kati ya vyumba, akitokwa na jasho kutokana na kazi yake ngumu katika joto kali. Inje, jua la Misri lilichoma gereza kama vile tanuru (four) ya moto. Wakati fulani ilionekana sawa vile alijua kila tofali la nyumba hiyo na kila mupasuko katika ukuta. Sasa hayo ndiyo yalikuwa makao yake. Kwa kweli, aliheshimiwa sana mahali hapo. Lakini, alikuwa mufungwa.

Yosefu anapaswa kuwa alikumbuka sana maisha yake katika eneo la juu la milimani lenye majiwe-majiwe katika Hebroni mahali alikuwa anachunga makundi ya baba yake! Alikuwa na miaka karibu 17 wakati Yakobo, baba yake, alimutuma katika safari iliyomuchukua kilometre nyingi kutoka nyumbani kwao. Sasa, hana tena uhuru kama huo. Ndugu zake wenye wivu walimugeukia wakiwa na chuki ya kutaka kumuua na kisha wakamuuzisha kama mutumwa. Alipelekwa Misri, ambapo alitumika kwanza katika nyumba ya ofisa Mumisri anayeitwa Potifa. Yosefu alitumainiwa sana na Potifa, mukubwa wake wa kazi, mupaka wakati bibi ya Potifa alimusingizia kuwa alitaka kumulala kwa nguvu na kwa hiyo akatupwa katika gereza. *​—Mwanzo, sura ya 37 na 39.

Yosefu alikuwa sasa na miaka 28, lakini kwa miaka hiyo amekuwa mutumwa na mufungwa kwa miaka karibu kumi. Kwa kusema bila kutia chumvi, maisha yake hayakuendeka namna alikuwa anatazamia. Angefunguliwa siku fulani? Angemuona tena baba yake mupendwa aliyezeeka ao Benyamini, ndugu yake mudogo aliyependa sana? Angebakia katika shimo hilo la gereza kwa muda gani?

Umekwisha kujisikia kama Yosefu? Wakati fulani, maisha yanabadilika na kuwa tofauti kabisa na vile tulitazamia katika ujana. Kwa kweli, hali ngumu zinaweza kuonekana kuwa zenye kuendelea, na inaweza kuwa vigumu kuona njia ya kutokea ao ya kuvumilia. Acha tuone mambo yenye tunaweza kujifunza kutokana na imani ya Yosefu.

“YEHOVA AKAENDELEA KUWA PAMOJA NA YOSEFU”

Yosefu alijua kuwa Mungu wake, Yehova, hakumusahau hata kidogo, na bila shaka kujua hivyo kulimusaidia avumilie. Hata katika gereza la inchi ya kigeni, Yehova alipata njia za kumubariki Yosefu. Biblia inasema hivi: ‘Yehova akaendelea kuwa pamoja na Yosefu, akazidi kumufanyia fazili zenye upendo na kumuwezesha kupata kibali machoni pa ofisa mukuu wa nyumba ya gereza.’ (Mwanzo 39:21-23) Yosefu alipoendelea kutumika kwa bidii, aliendelea kutolea Mungu wake sababu za kumubariki. Anapaswa kuwa alifarijika sana kwa kujua kama Yehova aliendelea kuwa pamoja na yeye!

Yehova alikusudia kumuacha Yosefu katika gereza hilo milele? Yosefu hakujua jibu, lakini aliendelea kumuambia Mungu wake jambo hilo katika sala. Kama vile inatokea mara nyingi, jibu lilikuja katika njia yenye hakutazamia kabisa. Siku moja, kulikuwa makelele katika gereza kwa kuwa wafungwa wawili wanaume walikuwa wamefika, wafungwa hao walikuwa maofisa kati ya wafanyakazi wa Farao. Mumoja alikuwa mukubwa wa watumishi wa kumupatia mufalme mukate na mwengine alikuwa mukubwa wa watumishi wa kumupatia mufalme kinywaji.​—Mwanzo 40:1-3.

Mukubwa wa walinzi alimupatia Yosefu kazi ya kuchunga watu hao waliojulikana sana. * Siku moja usiku, kila mumoja aliota ndoto ngumu kueleweka iliyoonekana kuwa ya kweli. Wakati Yosefu aliwaona asubuhi, alitambua kuwa jambo fulani halikuendeka. Kwa hiyo, aliwauliza hivi: “Kwa nini nyuso zenu zina huzuni leo?” (Mwanzo 40:3-7) Pengine wanaume hao waliona kuwa wanaweza kumuelezea mambo yaliyowasumbua kwa sababu alizungumuza nao kwa adabu. Yosefu hakujua kuwa mazungumuzo hayo yangeleta mabadiliko makubwa katika maisha yake. Ikiwa Yosefu hakuhangaikia wanaume hao, mazungumuzo hayo hayangefanyika. Tendo la Yosefu linaweza kutuchochea tujiulize, ‘Je, ninaonyesha imani yangu kwa Mungu kwa kupendezwa na wanadamu wenzangu?’

Yosefu alitendea wafungwa wenzake kwa wema na heshima

Wanaume hao wawili walieleza kuwa walisumbuliwa na ndoto zao ngumu kueleweka zilizoonekana kuwa za kweli, walisumbuliwa pia kwa sababu hawakuwa na mutu wa kueleza maana ya ndoto zao. Wamisri waliona ndoto kuwa za maana sana na walitegemea sana watu waliosema kuwa wana uwezo wa kueleza ndoto. Wanaume hao wawili hawakujua kuwa ndoto zao zilitoka kwa Yehova, Mungu wa Yosefu. Lakini Yosefu alijua hivyo. Aliwahakikishia hivi: ‘Je, tafsiri si za Mungu? Tafazali, munisimulie [ndoto zenu].’ (Mwanzo 40:8) Maneno ya Yosefu yangali ya maana leo kwa watu wote wanaojifunza Biblia kwa moyo wote. Ingekuwa muzuri ikiwa kila mutu wa dini angeonyesha unyenyekevu kama huo! Tunapaswa kuwa tayari kuachana na mawazo ya watu yenye kiburi na kumutegemea Mungu tunapotafuta mafasirio ya kweli ya neno lake.​—1 Wathesalonike 2:13; Yakobo 4:6.

Mukubwa wa watumishi wa kumupatia mufalme kinywaji alieleza kwanza ndoto yake. Alimuambia Yosefu kuwa katika ndoto aliona muzabibu wenye kuwa na matawi matatu yaliyokuwa na zabibu. Zabibu zilikuwa zimeiva, na munyweshaji alikamua maji yake ndani ya kikombe cha Farao. Kwa musaada wa Yehova, Yosefu alijua mara moja maana ya ndoto hiyo. Alimuambia mukubwa wa watumishi wa kumupatia mufalme kinywaji kama matawi matatu yalimaanisha siku tatu; katika siku hizo tatu, Farao angemurudisha katika cheo chake cha zamani. Kisha sura ya mwanaume huyo kuonyesha kuwa ametulia, Yosefu alimuomba hivi: ‘Tafazali, usikose kunitendea fazili zenye upendo na kunitaja kwa Farao.’ Yosefu alimuambia kuwa alikamatwa kwa nguvu kutoka nyumbani kwake na kufungwa bila sababu.​—Mwanzo 40:9-15.

Mukubwa wa watumishi wa kumupatia mufalme mukate alitiwa moyo na habari za muzuri zenye mwenzake aliambiwa. Alimuomba Yosefu amuelezee maana ya ndoto yake pia. Katika ndoto yake, aliona vikapu vitatu na pia ndege waliokuwa wanakula katika kikapu kimoja kati ya vikapu vyenye vilikuwa kwenye kichwa chake. Mungu alimujulisha Yosefu maana ya fumbo hilo pia. Lakini haikukuwa habari ya muzuri kwake. Yosefu alisema hivi: ‘Hii ndiyo tafsiri yake: Vile vikapu vitatu ni siku tatu. Baada ya siku tatu tokea sasa Farao atakiinua kichwa chako na kukiondoa juu yako naye atakutundika juu ya muti; nao ndege wataikula nyama yako.’ (Mwanzo 40:16-19) Kama watumishi wote waaminifu wa Mungu, Yosefu alifunua bila woga ujumbe wa Mungu, ujumbe wa muzuri na ujumbe wa hukumu iliyokaribia.​—Isaya 61:2.

Siku tatu kisha hapo, maneno ya Yosefu yalitimia. Farao alifanya karamu ya siku ya kuzaliwa kwake na akatangaza hukumu juu ya watumishi wake wawili. Desturi ya kufanya karamu ya siku ya kuzaliwa haikufanywa na watumishi wa Mungu wa zamani. Mukubwa wa watumishi wa kumupatia mufalme mukate aliuawa, kama vile Yosefu alikuwa amesema, lakini mukubwa wa watumishi wa kumupatia mufalme kinywaji alirudishwa kwenye cheo chake cha zamani. Hata hivyo, jambo la kuhuzunisha ni hili: mwanaume huyo asiyekamata mambo kwa uzito alisahau Yosefu kabisa.​—Mwanzo 40:20-23.

“MIMI SIPASWI KUFIKIRIWA!”

Miaka miwili mizima ikapita. (Mwanzo 41:1) Wazia namna hilo lilimuvunja Yosefu moyo kabisa! Pengine alitumaini sana kisha Yehova kumusaidia kuelewa ndoto zilizokuwa ngumu kueleweka za watumishi wa Farao. Kisha hapo, kila siku asubuhi, Yosefu aliamuka na tumaini mupya akifikiri kuwa hiyo ndiyo itakuwa siku ya kufunguliwa kwake, alitambua tu mara ingine kuwa maisha hayo mabaya ya kila siku katika gereza yaliendelea kwa muda murefu, bila kubadilika. Labda miaka hiyo miwili ndiyo ilikuwa migumu zaidi kwa Yosefu kuvumilia. Lakini, hakuacha hata siku moja kumutumainia Yehova Mungu wake. Kuliko kuvunjika moyo, alikusudia kuvumilia, na alitoka katika majaribu hayo akiwa na nguvu nyingi.​—Yakobo 1:4.

Katika nyakati hizi ngumu, ni nani kati yetu asiyekuwa na lazima ya kukomalisha uvumilivu? Ili kupambana na magumu ya maisha yenye kuendelea, tuko na lazima ya kukusudia, kuwa na uvumilivu, na amani ya ndani ambayo ni Mungu tu anaweza kutupatia. Kama vile alimusaidia Yosefu, anaweza kutusaidia tusivunjike moyo na tusipoteze tumaini.​—Waroma 12:12; 15:13.

Labda mukubwa wa watumishi wa kumupatia mufalme kinywaji alimusahau Yosefu, lakini Yehova hakumusahau hata kidogo. Siku moja usiku, Yehova alimutumia Farao ndoto mbili zenye haziwezi kusahauliwa. Katika ndoto ya kwanza, mufalme aliona ngombe saba wanene na wenye sura ya muzuri waliotoka katika Muto Nile. Ngombe hao wanene walifuatwa na ngombe saba wenye sura mbaya na wenye kukonda. Ngombe wenye kukonda walimeza ngombe wanene. Kisha hapo, katika ndoto Farao aliona tawi moja la nafaka likitokeza masuke saba ya muzuri. Lakini baadaye masuke mengine saba, yaliyokaushwa na upepo na membamba, yakatokea na kumeza masuke hayo ya muzuri. Asubuhi, Farao aliamuka akiwa mwenye kuhangaishwa sana kwa sababu ya ndoto hizo. Kwa hiyo, aliita watu wake wote wenye hekima na makuhani wenye kufanya uchawi ili wamuelezee maana ya ndoto yake. Wote hawakuweza. (Mwanzo 41:1-8) Hatujue ikiwa ndoto hizo ziliwashangaza sana ao ikiwa walitoa mawazo yenye kupingana. Kwa vyovyote, Farao alivunjika moyo sana, lakini alitamani zaidi kuelewa maana ya ndoto zake zisizoeleweka.

Mwishowe, mukubwa wa watumishi wa kumupatia mufalme kinywaji alimukumbuka Yosefu! Zamiri yake ilimusumbua, kwa hiyo akamuambia Farao juu ya kijana mwanaume wa pekee katika gereza ambaye, miaka mbili iliyopita, alimuelezea bila kukosea maana ya ndoto yake na ya mukubwa wa watumishi wa kumupatia mufalme mukate. Mara moja, Farao aliagiza Yosefu aitwe kutoka katika gereza.​—Mwanzo 41:9-13.

Wazia namna Yosefu alijisikia wakati wajumbe wa Farao walikuja kumuambia kuwa mufalme anamuita. Bila kukawia, alibadilisha nguo zake na kunyolewa, labda alikata nywele zote kwenye kichwa chake, kwa sababu hiyo ndiyo ilikuwa desturi ya Wamisri. Bila shaka, alisali kwa bidii kuwa Yehova amubariki katika mazungumuzo yake pamoja na Farao! Mara moja, alijikuta katika uwanja wenye utajiri sana wa makao ya mufalme akisimama mbele yake. Tunasoma hivi: ‘Kisha Farao akamuambia Yosefu: Nimeota ndoto, lakini hapana mutu wa kuitafsiri. Sasa mimi mwenyewe nimesikia ikisemwa juu yako ya kwamba unaweza kusikia ndoto na kuitafsiri.’ Jibu la Yosefu lilionyesha tena unyenyekevu wake na imani yake katika Mungu wake. Alisema hivi: ‘Mimi sipaswi kufikiriwa! Mungu atamutangazia Farao hali njema.’​—Mwanzo 41:14-16.

Yosefu alimuambia Farao kwa unyenyekevu hivi: “Mimi sipaswi kufikiriwa!”

Yehova anapenda watu wanyenyekevu na waaminifu, kwa hiyo, haishangaze kuona kuwa alimupatia Yosefu jibu ambalo lilishinda watu wenye hekima na makuhani. Yosefu alieleza kuwa ndoto mbili za Farao zilikuwa na maana moja. Kwa kurudilia ujumbe huo mara mbili, Yehova alikuwa anaonyesha kuwa jambo hilo lilikuwa “limewekwa imara,” ni kusema, lingetimia kabisa. Ngombe wanene na masuke ya muzuri ya nafaka yalifananisha miaka saba ya chakula kingi katika Misri, lakini ngombe wenye kukonda na masuke membamba ya nafaka yalifananisha miaka saba ya njaa yenye ingefuata miaka ya chakula kingi. Njaa hiyo ingemaliza chakula katika inchi.​—Mwanzo 41:25-32.

Farao alijua kuwa majibu ya Yosefu kwa ndoto zake yalikuwa ya kweli. Lakini ni jambo gani lingefanywa? Yosefu aliagiza mupango fulani ufanywe ili kushugulikia tatizo hilo. Farao alikuwa na lazima ya mutu “mwenye busara na mwenye hekima” ili asimamie kazi ya kukusanya nafaka za zaidi katika depo wakati wa miaka saba ya chakula kingi na kisha kuzigawia watu wenye kukosewa wakati wa njaa iliyokuwa inakuja. (Mwanzo 41:33-36) Ujuzi wa Yosefu na uwezo wake vilimufanya astahili kabisa kupewa kazi hiyo, lakini hakujitukuza mwenyewe. Kwa sababu alikuwa munyenyekevu na mwenye imani hakuona ulazima wa kujifikiria kwa kimbelembele kuwa ni yeye angestahili kufanya kazi hiyo. Ikiwa tuko na imani ya kweli katika Yehova hatuna lazima ya kutamani mambo makubwa ao kujitukuza. Tunaweza kuwa na amani, na kuacha mambo katika mikono yake yenye uwezo!

‘KUNAWEZA KUPATIKANA MUTU MWINGINE KAMA HUYU?’

Farao na watumishi wake wote waliona kuwa mupango wa Yosefu ulikuwa wenye hekima. Mufalme alitambua pia kuwa Mungu wa Yosefu ndiye alimuwezesha kusema maneno hayo yenye hekima. Aliwaambia hivi watumishi wake katika makao ya mufalme: ‘Je, kunaweza kupatikana mutu mwingine kama huyu ambaye roho ya Mungu iko ndani yake?’ Mufalme alimuambia Yosefu hivi: ‘Kwa kuwa Mungu amekuwezesha kuyajua yote hayo, hakuna mutu mwenye busara na mwenye hekima kama wewe. Wewe binafsi utaisimamia nyumba yangu, na watu wangu wote watakutii kabisa. Mimi nitakuwa mukuu kuliko wewe katika kiti cha ufalme tu.’​—Mwanzo 41:38-41.

Farao alitimiza maneno yake. Yosefu alivalishwa nguo za kitani ya muzuri bila kukawia. Farao alimupatia mukufu wa zahabu, pete ya muhuri, gari la kifalme, na mamlaka ya kusafiri kotekote katika inchi na kutimiza mipango yake. (Mwanzo 41:42-44) Kwa hiyo, katika siku moja, Yosefu alitoka katika gereza na kuingia katika nyumba ya mufalme. Aliamuka asubuhi akiwa mufungwa wa hali ya chini, na alilala usiku akiwa kwenye cheo cha pili kisha Farao. Inaonekana wazi kuwa imani yake katika Yehova Mungu ilitetewa! Yehova aliona ukosefu wote wa haki mutumishi wake alitendewa kwa miaka mingi. Alishugulikia mambo hayo kwa wakati wenye kufaa na kwa njia yenye kufaa. Yehova alitaka kushugulikia mambo mabaya yenye Yosefu alitendewa lakini alitaka pia kulinda taifa la Israeli la wakati uliokuwa unakuja. Katika habari inayokuja ya sehemu hii, tutaona namna Yehova alifanya hivyo.

Ikiwa unapitia hali ngumu, pengine ukosefu wa haki unaoonekana kuwa unaendelea kwa miaka mingi, usivunjike moyo. Umukumbuke Yosefu. Kwa sababu hakupoteza wema, unyenyekevu, uvumilivu wake, na imani yake, mambo hayo yalifanya Yehova amubariki mwishowe.

^ fu. 4 Soma habari “Tuige Imani Yao” katika gazeti Munara wa Mulinzi la tarehe 01/08/2014 na la tarehe 01/11/2014.

^ fu. 10 Wamisri wa zamani walifurahia zaidi ya aina 90 za mikate na keki. Kwa hiyo, mukubwa wa watumishi wa kumupatia Farao mukate alikuwa mutu mwenye kujulikana sana. Na mukubwa wa watumishi wa kumupatia mufalme kinywaji alisimamia kikundi cha watumishi waliohakikisha kuwa divai ya Farao na labda pombe yake ilikuwa ya hali ya juu na ililindwa salama ili mutu yeyote asijaribu kumupatia mufalme sumu. Kulikuwa hatari kubwa, kwa sababu kufanya njama na mauaji yalikuwa mambo ya kawaida kwenye makao ya mufalme. Kwa kawaida mukubwa wa watumishi wa kumupatia mufalme kinywaji aligeuka kuwa mushauri wake mwenye kutumainika.