Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI KUBWA | WAPANDA-FARASI INE​—WANAKUHUSU NAMNA GANI?

Wale Wapanda-Farasi Ine​—Ni Nani?

Wale Wapanda-Farasi Ine​—Ni Nani?

Habari juu ya wale wapanda-farasi ine inaonekana kuwa yenye kuogopesha na yenye kuwa nguvu kuelewa. Lakini haipaswe kuwa hivyo. Sababu gani? Kwa sababu Biblia na matukio ya historia ya leo yanatusaidia kuelewa muzuri kama kila mupanda-farasi anafananisha nini. Na hata kama mwendo wao ni alama ya mambo mabaya juu ya dunia, hilo linaweza kuwa pia habari njema kwako na kwa familia yako. Namna gani? Kwanza, tuone kama kila mupanda-farasi anafananisha nini.

MWENDESHAJI WA FARASI MWEUPE

Maono yanaanza hivi: “Nikaona, na, tazama! farasi mweupe; na yule anayeketi juu yake alikuwa na upinde; naye akapewa taji, naye akaenda akishinda na kukamilisha ushindi wake.”​—Ufunuo 6:2.

Mwendeshaji wa farasi mweupe ni nani? Mambo yenye kutusaidia kumutambua yanapatikana katika kitabu hicho cha Ufunuo, chenye baadaye kinaita mupanda-farasi huyo wa mbinguni “Neno la Mungu.” (Ufunuo 19:11-13) Jina la cheo Neno, limepewa Yesu Kristo, kwa sababu anatenda kama musemaji wa Mungu. (Yohana 1:1, 14) Zaidi ya hilo, anaitwa ‘Mufalme wa wafalme na Bwana wa mabwana’ na anaitwa pia “Mwaminifu na wa Kweli.” (Ufunuo 19:16) Ni wazi kwamba, iko na mamlaka ya kutenda kama mufalme-shujaa, na hatumie mubaya mamlaka yake. Hata hivyo, maulizo fulani yanatokea.

Ni nani anamupatia Yesu mamlaka ya kufanya vita? (Ufunuo 6:2) Katika maono, nabii Danieli aliona Masiya mwenye kufananishwa na “mwana wa binadamu” ambaye Yehova Mungu, * ‘Muzee wa Siku,’ alimupatia “utawala na heshima na ufalme.” (Danieli 7:13, 14) Kwa hiyo, ni Mungu Mweza-Yote ndiye anamupatia Yesu mamlaka na haki ya kutawala na kuleta hukumu. Farasi mweupe ni alama yenye kufaa ili kuonyesha vita yenye inafanywa na Mwana wa Mungu, kwa sababu Maandiko yanatumia rangi ya mweupe ili kuonyesha haki.​—Ufunuo 3:4; 7:9, 13, 14.

Ni wakati gani wapanda-farasi hao walianza mwendo wao? Biblia inaonyesha kwamba Yesu, mupanda-farasi wa kwanza, alianza mwendo wake kisha kupewa taji. (Ufunuo 6:2) Ni wakati gani Yesu alivalishwa taji ili kuwa Mufalme huko mbinguni? Haikuwa wakati alirudi mbinguni kisha kifo chake. Biblia inaonyesha kwamba kipindi cha kungojea kilianza wakati huo. (Waebrania 10:12, 13) Yesu alipatia wanafunzi wake alama yenye ingewasaidia kujua mwisho wa kipindi hicho cha kungojea na mwanzo wa utawala wake huko mbinguni. Alisema kwamba wakati angeanza kutawala, hali ya ulimwengu ingeharibika sana. Kungekuwa vita, upungufu wa chakula, na magonjwa ya kuambukiza. (Mathayo 24:3, 7; Luka 21:10, 11) Kisha tu kutokea kwa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu katika mwaka wa 1914, ilionekana wazi kwamba wanadamu waliingia katika kipindi hicho cha muvurugo chenye Biblia inaita “siku za mwisho.”​—2 Timotheo 3:1-5.

Lakini sababu gani hali ya ulimwengu imeharibika, kuliko kuwa muzuri, tangu Yesu kupewa mamlaka katika mwaka wa 1914? Ni kwa sababu wakati huo Yesu alianza kutawala mbinguni, hapana duniani. Kisha, vita ikatokea mbinguni, na Yesu ambaye alitoka tu kuwekwa kuwa Mufalme, ambaye anaitwa Mikaeli, alitupa Shetani na mashetani wake juu ya dunia. (Ufunuo 12:7-9, 12) Tangu ametupwa duniani, Shetani iko na hasira kubwa kwa sababu anajua kwamba anabaki na siku kidogo. Kwa kweli, hivi karibuni Mungu atatimiza mapenzi yake hapa duniani kumuhusu Shetani. (Mathayo 6:10) Tuone sasa namna gani wapanda-farasi wengine watatu wanatusaidia tukuwe hakika kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” zenye muvurugo. Tofauti na mupanda-farasi wa kwanza, mwenye kufananisha mutu wa kweli, wale wapanda-farasi watatu wenye kufuata wanafananisha hali ya mubaya yenye imepata wanadamu katika ulimwengu.

MWENDESHAJI WA FARASI MWEKUNDU

“Na mwingine akatokea, farasi mwenye rangi ya moto; na yeye anayeketi juu yake akapewa ruhusa ya kuondoa amani duniani ili wauane; naye akapewa upanga mukubwa.”​—Ufunuo 6:4.

Mupanda-farasi huyo anafananisha vita. Ona kwamba mupanda-farasi huyo haondoe amani katika mataifa fulani tu, lakini katika dunia yote. Katika 1914, kwa mara ya kwanza katika historia ya wanadamu, vita ilitokea katika dunia yote. Kisha, kulitokea vita ya pili ya ulimwengu yenye iliua watu wengi zaidi. Watu fulani wanakadiria kwamba hesabu ya watu wenye walikufa kwa sababu ya vita na mapambano ya watu wenye kutumia silaha tangu mwaka wa 1914 ilikuwa zaidi ya milioni 100! Tena, watu wengine wengi waliteseka kwa sababu ya matatizo makali.

Ni kwa kiasi gani vita vinaenea leo? Kwa mara ya kwanza katika historia, wanadamu wanaonekana kuwa na uwezo wa kuharibu watu wote katika dunia. Hata mashirika yenye kusema kwamba yanaleta amani, kama vile Umoja wa Mataifa, hayajaweza kuzuia mwendeshaji wa farasi mwekundu.

MWENDESHAJI WA FARASI MWEUSI

“Nikaona, na, tazama! farasi mweusi; na yeye anayeketi juu yake alikuwa na mizani mukononi mwake. Nami nikasikia sauti kana kwamba ni katikati ya wale viumbe hai wanne ikisema: ‘Kibaba cha ngano kwa dinari moja, na vibaba vitatu vya shayiri kwa dinari moja; wala usizuru mafuta ya zeituni na divai.”’​—Ufunuo 6:5, 6.

Mupanda-farasi huyo anafananisha njaa. Tunaona kwamba kupata chakula kungekuwa nguvu sana hivi kwamba kibaba kimoja (litre 1,08) cha ngano kingekuwa na bei ya dinari moja, mushahara wa siku nzima ya mufanyakazi wakati huo! (Mathayo 20:2) Dinari hiyo moja ingetumiwa pia ili kuuza vibaba vitatu (litre 3,24) vya shayiri, yenye ilionwa kuwa ya hali ya chini kuliko ngano. Namna gani familia kubwa ingeweza kupata chakula cha kutosha katika hali hiyo? Watu wanashauriwa wasitumie ovyoovyo hata chakula kwa ajili ya siku. Jambo hilo linaonyeshwa wazi kupitia kilimo na chakula cha musingi cha wakati huo kama vile mafuta ya zeituni na muvinyo.

Tangu 1914, tumeona mambo yenye kuhakikisha kwamba mwendeshaji wa farasi mweusi iko katika mwendo? Ndiyo! Katika kipindi kati ya mwaka wa 1901 na 2000, watu karibu milioni 70 walikufa kwa sababu ya njaa. Ripoti moja ilikadiria kwamba “watu milioni 805​—karibu mutu mumoja kati ya watu kenda katika dunia yote​—walikuwa wanakula mubaya katika 2012-2014.” Ripoti ingine inasema hivi: “Kila mwaka, njaa inaua watu wengi kuliko wale wenye wanakufa na magonjwa ya UKIMWI, malaria na kifua kikuu yakiunganishwa pamoja.” Hata kama watu wamejikaza sana ili kulisha watu wenye kuwa na njaa, mwendeshaji wa farasi mweusi angali katika mwendo wake.

MWENDESHAJI WA FARASI WA RANGI YA KIJIVU

“Nikaona, na, tazama! farasi wa rangi ya kijivu; na yeye anayeketi juu yake alikuwa na jina Kifo. Na Kaburi lilikuwa likimufuata kwa ukaribu. Nao wakapewa mamlaka juu ya sehemu ya ine ya dunia, ili kuua kwa upanga murefu na kwa upungufu wa chakula na kwa pigo lenye kufisha na kwa wanyama-mwitu wa dunia.”​—Ufunuo 6:8.

Mupanda-farasi wa ine anafananisha kifo chenye kinatokana na pigo na mambo mengine. Kisha tu 1914, homa ya Hispania iliua mamilioni ya watu. Inawezekana watu milioni 500 waliambukizwa, ni kusema, karibu mutu mumoja kati ya watu watatu duniani!

Lakini, homa ya Hispania ilikuwa mwanzo tu. Wachunguzi wanakadiria kwamba zaidi ya milioni 300 ya watu walikufa kwa sababu ya ugonjwa wa ndui (variole) katika kipindi cha kuanzia 1901 mupaka 2000. Mupaka leo, mamilioni ya watu wanakufa kwa sababu ya UKIMWI, kifua kikuu na malaria hata kama kumekuwa maendeleo mengi katika mambo ya kinganga.

Matokeo ni yaleyale, watu wanaendelea kufa, ikuwe kwa sababu ya vita, njaa, ao magonjwa. Kaburi linaendelea kukusanya watu, bila kutoa tumaini lolote.

WAKATI MUZURI UKO KARIBU!

Kipindi hiki chenye muvurugo kitaisha hivi karibuni. Kumbuka jambo hili: Yesu ‘alienda akishinda’ katika mwaka wa 1914 kwa kumutupa Shetani hapa duniani, lakini Yesu hakukamilisha ushindi wake. (Ufunuo 6:2; 12:9, 12) Hivi karibuni, katika vita ya Har-Magedoni, Yesu ataondoa uvutano wa Shetani na ataharibu watu wenye kumuunga mukono. (Ufunuo 20:1-3) Yesu hatamaliza tu uendeshaji wa wale wapanda-farasi watatu, lakini pia ataondoa hata matokeo mabaya ya uendeshaji wao wenye kuua. Namna gani? Tuone mambo yenye Biblia inaahidi.

Pahali pa vita, kutakuwa amani. Yehova ‘anakomesha vita mupaka kwenye mwisho wa dunia. Upinde anauvunja na kuukata mukuki vipande-vipande.’ (Zaburi 46:9) Wale wenye kupenda amani “watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”​—Zaburi 37:11.

Pahali pa njaa, kutakuwa chakula kwa uwingi. “Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.”​—Zaburi 72:16.

Yesu ataondoa matokeo mabaya ya wale wapanda-farasi watatu wengine

Pahali pa mapigo na kifo, watu wote watakuwa na afya kamilifu na wataishi milele. Mungu “atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”​—Ufunuo 21:4.

Wakati Yesu alikuwa duniani, alionjesha watu mambo mazuri yenye atafanyia wanadamu chini ya utawala wake. Aliendeleza amani, alikulisha maelfu ya watu kimuujiza, aliponyesha wagonjwa, na alifufua hata wafu.​—Mathayo 12:15; 14:19-21; 26:52; Yohana 11:43, 44.

Mashahidi wa Yehova watafurahi kukuonyesha kupitia Biblia yako namna unaweza kuwa tayari wakati wapanda-farasi hao watamaliza mwendo wao. Utapenda kujua mengi zaidi?