Hamia kwenye habari

Je, Mashahidi wa Yehova Huwashinikiza Watu Wabadili Dini?

Je, Mashahidi wa Yehova Huwashinikiza Watu Wabadili Dini?

 Hapana, hatufanyi hivyo. Katika gazeti letu kuu, Mnara wa Mlinzi tumesema hivi: “Ni kosa kulazimisha watu wabadili dini.” * Sababu zifuatazo zinaonyesha kwa nini tunaepuka kuwashinikiza watu:

  •   Yesu hakuwahi kuwashinikiza watu wakubali mafundisho yake. Alijua kwamba ni watu wachache sana ambao wangekubali ujumbe wake. (Mathayo 7:​13, 14) Baadhi ya wanafunzi wake walipokwazwa na maneno yake, aliwaacha waondoke badala ya kuwalazimisha wabaki.​—Yohana 6:​60-​62, 66-​68.

  •   Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasiwalazimishe watu wabadili imani yao. Badala ya kuwalazimisha watu kukubali habari njema ya Ufalme, wanafunzi walipaswa kuwatafuta watu waliokuwa tayari kusikiliza.​—Mathayo 10:​7, 11-​14.

  •   Kugeuzwa imani kwa sababu ya kulazimishwa ni bure, kwa kuwa Mungu hukubali tu ibada inayotoka moyoni.​—Kumbukumbu la Torati 6:​4, 5; Mathayo 22:37, 38.

Je, tunageuza watu imani kinyume cha sheria?

 Ni kweli kwamba tunaeneza ujumbe wa Biblia “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia,” na tunafanya hivyo “hadharani na nyumba kwa nyumba,” kama Biblia inavyoamuru. (Matendo 1:8; 10:42; 20:20) Na kama Wakristo wa mapema, nyakati nyingine tunashtakiwa kwamba tunawageuza watu imani kinyume cha sheria. (Matendo 18:12, 13) Hata hivyo, mashtaka hayo ni ya uwongo. Hatujaribu kuwalazimisha watu wakubali imani yetu. Badala yake, tunaamini kwamba watu wanapaswa kuruhusiwa kupata ujuzi ili waweze kufanya uamuzi wakiwa na habari kamili.

 Hatuwalazimishi watu wabadili dini, wala hatujihusishi katika utendaji wowote wa kisiasa huku tukijifanya tunaendeleza dini na hatutoi msaada wa kimwili au wa kijamii ili tujipatie waumini wapya. Kwa njia hii tunatofautiana na wale wanaodai kuwa Wakristo lakini wanamshushia Kristo heshima kwa kufanya mambo hayo. *

Je, mtu ana haki ya kubadili dini?

Nabii Abrahamu aliacha dini ya watu wake wa ukoo

 Ndiyo, Biblia inaonyesha kwamba watu wana haki ya kubadili dini yao. Inasimulia kuhusu watu wengi ambao waliacha dini ya watu wa familia yao, na kwa hiari yao wakaamua kumwabudu Mungu wa kweli. Mifano kadhaa ni kama vile Abrahamu, Ruthu, baadhi ya watu wa Athene, na mtume Paulo. (Yoshua 24:2; Ruthu 1:​14-​16; Matendo 17:22, 30-​34; Wagalatia 1:​14, 23) Zaidi ya hilo, Biblia pia inaonyesha kwamba mtu ana haki ya kufanya uamuzi usio na hekima wa kuacha ibada ambayo Mungu anakubali.​—1 Yohana 2:​19.

 Haki ya kubadili dini inategemezwa na Azimio la Watu Wote la Haki za Kibinadamu, ambalo Umoja wa Mataifa umeliita “msingi wa sheria za haki ya kibinadamu ya kimataifa.” Sheria hiyo inasema kwamba kila mtu ana “uhuru wa kubadili dini au imani yake” na “kutafuta, kupokea, na kutoa habari na mawazo,” kutia ndani mawazo ya kidini. * Bila shaka, haki hizo zinampa kila mtu daraka la kuheshimu kwamba wengine wana haki ya kudumisha imani yao na kukataa maoni wasiyokubaliana nayo.

Je, kubadili dini kunavunja utamaduni na desturi za familia?

 Si lazima iwe hivyo. Biblia inawatia watu moyo wawaheshimu wengine, haidhuru wao ni wa dini gani. (1 Petro 2:​17) Isitoshe, Mashahidi wa Yehova wanatii amri ya Biblia ya kuwaheshimu wazazi wao, hata ikiwa wana imani tofauti na ya wazazi wao.​—Waefeso 6:​2, 3.

 Hata hivyo, si kila mtu anayekubaliana na maoni ya Biblia. Mwanamke mmoja aliyelelewa nchini Zambia anasema hivi: “Katika jamii yangu, kubadili dini . . . kulionwa kuwa sawa na kusaliti familia na jamii.” Mwanamke huyo alikabili jambo hilo alipoamua kubadili dini yake baada ya kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova akiwa tineja. Anasema hivi: “Wazazi wangu waliniambia mara nyingi kwamba nimewakasirisha na kuwaaibisha. Hilo lilinivunja moyo sana kwa kuwa kupata kibali cha wazazi ni jambo la maana sana kwangu. . . . Hata hivyo, haimaanishi nimeisaliti familia yangu kwa kuwa mwaminifu kwa Yehova badala ya kushikamana na desturi za kidini.” *

^ Ona toleo la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 2002, ukurasa wa 12, fungu la 15.

^ Kwa mfano, karibu na mwaka wa 785 W.K., Charlemagne alitoa amri iliyosema kwamba mtu yeyote katika eneo la Wasaksoni ambaye angekataa kubatizwa na kuwa Mkristo angeuawa. Pia, mkataba wa Amani ya Augsburg, uliotiwa sahihi mnamo 1555 W.K. na vikundi vilivyokuwa vikipigana vya Milki Takatifu ya Roma, ulisema kwamba kila mtawala katika eneo lililo ya chini milki hiyo alipaswa kuwa Mkatoliki au Mlutheri na kwamba kila mtu aliye chini ya utawala wake alipaswa kukubali dini ya mtawala huyo. Wale waliokataa kujipatanisha na dini ya mtawala huyo walilazimishwa kuhama.

^ Haki kama hizo zimetiwa ndani katika Mkataba wa Afrika wa Haki za Kibinadamu, Azimio la Amerika la Haki na Wajibu wa Wanadamu, Mkataba wa Nchi za Kiarabu wa Haki za Kibinadamu wa 2004, Azimio la Nchi za Kusini-Mashariki mwa Asia la Haki za Kibinadamu (ASEAN), Mkataba wa Ulaya wa Haki za Kibinadamu, na Agano la Kimataifa la Haki za Kiraia na za Kisiasa. Hata hivyo, mataifa yanayodai kutoa haki hizo yanatofautiana katika uwajibikaji wa kuhakikisha haki hizo zinatolewa.

^ Yehova ndilo jina la Mungu wa kweli kama linavyopatikana katika Biblia.