Hamia kwenye habari

Je, Ni Lazima Mtu Awe Katika Dini Fulani?

Je, Ni Lazima Mtu Awe Katika Dini Fulani?

Jibu la Biblia

 Ndiyo, kwa sababu Mungu anataka watu wakutane kwa ajili ya ibada. Biblia inasema: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe.”​—Waebrania 10:24, 25.

 Yesu alisema kwamba wafuasi wake wangekuwa katika kikundi kilichopangwa alipowaambia hivi: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Njia kuu ambayo wanafunzi wa Kristo wangeonyesha upendo huo ni kwa kukutana pamoja na waamini wenzao. Wangepangwa katika makutaniko yanayokutana kwa ukawaida kwa ajili ya ibada. (1 Wakorintho 16:19) Kwa ujumla, wangefanyiza undugu wa ulimwenguni pote.​—1 Petro 2:​17.

Mengi yanahitajika kuliko kuwa tu katika dini fulani

 Ingawa Biblia inaonyesha kwamba watu wanapaswa kukutana ili kumwabudu Mungu, haifundishi kwamba mtu anaweza kumpendeza Mungu kwa kuwa tu mshiriki wa dini fulani. Ili mtu apate kibali cha Mungu, dini yake inapaswa kuathiri maisha yake ya kila siku. Kwa mfano, Biblia inasema: “Namna ya ibada iliyo safi na isiyotiwa unajisi kwa maoni ya Mungu wetu na Baba ni hii: kuwatunza mayatima na wajane katika dhiki yao, na kuendelea kujitunza bila doa kutokana na ulimwengu.”​—Yakobo 1:27.