Hamia kwenye habari

Je, Mashahidi wa Yehova Huwalazimisha Watoto Wafuate Imani Yao?

Je, Mashahidi wa Yehova Huwalazimisha Watoto Wafuate Imani Yao?

 Hapana, kwa sababu kumwabudu Mungu ni uamuzi wa kibinafsi. (Waroma 14:12) Mashahidi wa Yehova huwafundisha watoto wao kanuni za Biblia, lakini mtoto anapokomaa anajiamulia ikiwa atakuwa Shahidi wa Yehova.—Waroma 12:2; Wagalatia 6:5.

 Kama wazazi wengine, Mashahidi wa Yehova hutaka watoto wao wawe na maisha mazuri. Wanawafundisha watoto kile wanachoona kitawasaidia: ustadi wa kazi, na pia kanuni za kimaadili na imani za kidini. Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba Biblia ina kanuni zinazoweza kumsaidia mtu aishi maisha bora, hivyo wao hujifunza Biblia pamoja na watoto wao na kuwapeleka kwenye mikutano ya Kikristo ili kukazia viwango vya Biblia ndani yao. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Mtoto anapokomaa anaweza kujiamulia ikiwa atafuata dini ya wazazi wake.

 Je, Mashahidi wa Yehova hubatiza watoto wachanga?

 Hapana. Biblia haiungi mkono kuwabatiza watoto wachanga. Kwa mfano, inaonyesha kwamba kabla ya kubatizwa, Wakristo wa karne ya kwanza walisikiliza ujumbe waliopewa, ‘wakaukubali,’ na kutubu. (Matendo 2:14, 22, 38, 41) Kwa hiyo, ili mtu abatizwe anapaswa kuwa na umri wa kutosha kuelewa mafundisho ya Biblia, ayaamini, na kuamua kuishi kulingana na mafundisho hayo. Mtoto mchanga hawezi kufanya mambo yote hayo.

 Kadiri watoto wanavyokua, huenda hatimaye wakaamua kubatizwa. Hata hivyo, ili wabatizwe, wanapaswa kuelewa wajibu unaohusiana na uamuzi wao.

 Je, Mashahidi wa Yehova huwatenga watoto wao wakiamua kwamba hawataki kubatizwa?

 Hapana. Ingawa wazazi Mashahidi huhuzunika mtoto wao anapokataa kuwa Shahidi, bado wanampenda na hawavunji uhusiano wao kwa sababu hiyo.

Kila mtu anapaswa kujiamulia mwenyewe ikiwa atabatizwa au la, hata awe na umri gani

 Kwa nini Mashahidi wa Yehova huambatana na watoto wao wanapoenda kuhubiri?

 Kuna sababu kadhaa zinazotufanya tuambatane na watoto wetu tunapoenda kuhubiri. *

  •   Biblia inawaagiza wazazi wawafunze watoto wao mambo ya kiroho, na kuwazoeza kumwabudu Mungu. (Waefeso 6:4) Kwa kuwa ibada yetu inatia ndani kutangaza waziwazi imani yetu, kuhubiri ni sehemu muhimu ya kumfundisha mtoto kumhusu Mungu.—Waroma 10:9, 10; Waebrania 13:15.

  •   Biblia inawatia moyo vijana “walisifu jina la Bwana.” (Zaburi 148:12, 13, Union Version) Njia kuu ya kumtukuza Mungu ni kuwaeleza wengine kumhusu. *

  •   Watoto hujifunza mambo muhimu wanapohubiri pamoja na wazazi wao. Kwa mfano, wanajifunza kuwasiliana na watu wa namna zote, na kusitawisha sifa nzuri kama huruma, fadhili, heshima, na kutokuwa na ubinafsi. Pia, kufanya hivyo huwasaidia kuelewa msingi wa Kimaandiko wa imani yao.

 Je, Mashahidi wa Yehova husherehekea sikukuu mbalimbali?

 Mashahidi wa Yehova hawashiriki katika sikukuu za kidini au katika sherehe nyingine zinazomchukiza Mungu. * (2 Wakorintho 6:14-17; Waefeso 5:10) Kwa mfano, hatusherehekei sikukuu za kuzaliwa au Krismasi, kwa kuwa sikukuu hizo zimetokana na vyanzo visivyo vya Kikristo.

 Hata hivyo, tunafurahi kuwa pamoja na watu wa familia zetu na kuwapa watoto wetu zawadi kwa ukarimu. Badala ya kuruhusu kalenda ituamulie wakati ambapo familia itakutana na wakati wa kupeana zawadi, tunapanga tafrija za familia na kupeana zawadi wakati wowote katika mwaka.

Wazazi Wakristo hufurahi kuwapa watoto wao zawadi

^ Kwa kawaida, watoto wa Mashahidi hawashiriki katika kazi ya kuhubiri bila kuambatana na mzazi au mtu mzima anayetegemeka.

^ Biblia inataja watoto kadhaa ambao walimfurahisha Mungu kwa kuzungumza na wengine kuhusu imani yao.—2 Wafalme 5:1-3; Mathayo 21:15, 16; Luka 2:42, 46, 47.

^ Baadhi ya majina yamebadilishwa.