Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HEKIMA YA KALE INAYOFAA LEO

Kusamehe kwa Hiari

Kusamehe kwa Hiari

KANUNI YA BIBLIA: “Endeleeni . . . kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia.”—Wakolosai 3:13.

Inamaanisha nini? Biblia inasema dhambi ni kama deni, na kuomba msamaha ni sawa na kufutwa kwa deni. (Luka 11:4) Kitabu kimoja cha marejeo kinasema kwamba katika Maandiko, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “samehe” linamaanisha “kuachilia deni kwa kutodai.” Hivyo, tunapoamua kumsamehe mkosaji hatutazamii atulipe chochote. Kusamehe kwa hiari hakumaanishi kwamba tunakubaliana na tabia mbaya au maumivu tuliyopata baada ya kukosewa. Badala yake, tunaamua kutoweka kinyongo hata ikiwa tuna sababu nzuri ya “kulalamika.”

Je, hekima hiyo inafaa leo? Sote tunatenda dhambi kwa kuwa hatujakamilika. (Waroma 3:23) Hivyo, ni jambo la hekima kuwasamehe wengine kwa kuwa huenda sisi pia tukahitaji kuomba msamaha. Pia, tunanufaika tunapowasamehe wengine. Jinsi gani?

Tunajiumiza wenyewe tunapokasirika, tunapoweka kinyongo, na kukataa kuwasemehe wengine. Hisia hizo zisizofaa zinaweza kutukosesha furaha na tushindwe kufanya vizuri shughuli za kila siku za maisha. Pia, zinaweza kuhatarisha afya yetu. Ripoti moja ya gazeti linaloitwa Journal of the American College of Cardiology, iliyotolewa na Dakt. Yoichi Chida na Profesa wa Saikolojia, Andrew Steptoe, ilisema hivi: “Uchunguzi wa hivi karibuni unaonyesha kwamba kuna uhusiano kati ya hasira, chuki, na magonjwa ya moyo.”

Kwa upande mwingine, fikiria faida za kusamehe. Tunapowasamehe wengine kwa hiari, tunadumisha umoja, amani, na kuimarisha mahusiano. Jambo la muhimu hata zaidi ni kwamba tunapofanya hivyo, tunamwiga Mungu anayesamehe kwa hiari watenda dhambi wanaotubu, naye anatarajia sisi pia tuwasamehe wengine.—Marko 11:25; Waefeso 4:32; 5:1.