Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Macho ya Jairo—Njia Yake ya Kumwabudu na Kumtumikia Mungu

Macho ya Jairo—Njia Yake ya Kumwabudu na Kumtumikia Mungu

Hebu wazia ukiwa umeshindwa kuudhibiti mwili wako isipokuwa macho tu. Ndugu yangu Jairo anakabili hali hiyo ngumu. Licha ya hilo, hajakata tamaa maishani. Kabla sijawaeleza jinsi alivyopata kusudi maishani, acheni niwaeleze zaidi kumhusu.

Jairo alizaliwa akiwa na ugonjwa wa kupooza ubongo unaoitwa spastic quadriplegia. * Kwa sababu hiyo, hawezi kudhibiti baadhi ya viungo vya mwili wake. Ubongo wake hauwezi kuongoza misuli yake vizuri, na hilo husababisha miguu yake kujipinda, au kuyumbayumba. Nyakati nyingine anaweza kujigonga na kujiumiza bila kutarajia, na hivyo watu walio karibu naye wanaweza kuumia wasipojihadhari. Inasikitisha kwamba mara kwa mara mikono na miguu yake inahitaji kufungwa kwenye kiti chake cha magurudumu ili kuzuia hali hiyo.

KUPAMBANA NA MAUMIVU TANGU UTOTONI

Jairo amekuwa na maumivu mengi sana katika ukuzi wake wa kimwili. Alipokuwa na umri wa miezi mitatu tu, alianza kuanguka ghafula na kupoteza fahamu. Mara nyingi Mama angemshikilia kwa nguvu na kumkimbiza hospitalini akifikiri kwamba amekufa.

Kwa sababu ya kukakamaa kwa misuli, mifupa ya Jairo ilijipinda baada ya muda. Alipokuwa na umri wa miaka 16, aliteguka nyonga na hivyo akafanyiwa upasuaji mkubwa kwenye paja, kiuno na nyonga. Bado nakumbuka jinsi Jairo alivyolia kila siku kwa sababu ya maumivu makali.

Kwa sababu ya ulemavu huo, imembidi Jairo kuwategemea wengine kufanya mambo ya kawaida kama vile kula, kuvaa na kulala. Baba na Mama humsaidia kufanya mambo hayo. Ingawa sikuzote Jairo anahitaji msaada, wazazi wetu humkumbusha kwamba maisha yake hayategemei wanadamu tu bali pia Mungu.

NJIA YA MAWASILIANO YAPATIKANA

Wazazi wetu ni Mashahidi wa Yehova, na wamekuwa wakimsomea Jairo hadithi za Biblia tangu alipokuwa mtoto mchanga. Wametambua sikuzote kwamba maisha huwa yenye kusudi ikiwa mtu ana uhusiano mzuri pamoja na Mungu. Ingawa Jairo ana ugonjwa mbaya sana, bado anaweza kuwa na tumaini imara la wakati ujao. Hata hivyo, walijiuliza ikiwa angeweza kupata ujuzi wa Biblia.

Siku moja Jairo alipokuwa bado mtoto, Baba alimuuliza hivi: “Jairo, unaweza kuongea nami?” Kisha akaongeza hivi: “Ikiwa kweli unanipenda, utazungumza nami!” Jairo alianza kutokwa na machozi Baba alipokuwa akimsihi aseme angalau neno moja. Ingawa alijitahidi kueleza hisia zake kwa maneno, alitoa sauti ambayo haikueleweka. Baba alihisi vibaya kwa sababu alimfanya Jairo alie. Lakini hilo lilionyesha kwamba Jairo alielewa kile ambacho Baba alikuwa amesema. Tatizo ni kwamba hangeweza kuzungumza.

Baadaye wazazi wetu waligundua kwamba nyakati nyingine Jairo aliyazungusha macho yake haraka akijaribu kuwasilisha mawazo na hisia zake. Jairo alivunjika moyo kwa sababu wakati mwingine hakueleweka. Lakini Jairo angetabasamu kwa furaha wazazi wetu walipojifunza kuelewa ishara alizotoa kwa macho yake na kumpa msaada aliohitaji. Hiyo ndiyo iliyokuwa njia yake ya kuonyesha shukrani.

Mtaalamu wa usemi alipendekeza kwamba ili tuwasiliane vizuri na Jairo, tulipaswa kuinua mikono yetu tulipotaka kumuuliza swali ili ajibu ndiyo au hapana. Mkono wa kulia ulimaanisha ndiyo na wa kushoto ulimaanisha hapana. Hivyo angeweza kujibu kwa kuelekeza macho yake katika mkono aliochagua.

HATUA MUHIMU SANA KATIKA MAISHA YA JAIRO

Mashahidi wa Yehova hukusanyika mara tatu kila mwaka ili kusikiliza hotuba mbalimbali za Biblia. Kila mara Jairo alipohudhuria makusanyiko hayo alifurahishwa sana na hotuba ya ubatizo. Jairo alipokuwa na umri wa miaka 16, Baba alimuuliza, “Jairo, ungependa kubatizwa?” Mara moja Jairo aliutazama mkono wa kulia wa Baba na hilo likaonyesha wazi kwamba alitaka kubatizwa. Kisha Baba akaendelea kumuuliza, “Je, umemwahidi Mungu katika sala kwamba utamtumikia milele?” Jairo aliutazama tena mkono wa kuume wa Baba. Ilikuwa wazi kwamba alikuwa ameweka wakfu maisha yake kwa Yehova.

Baada ya Jairo kujifunza Biblia kwa kipindi fulani cha wakati, ilionekana wazi kwamba alielewa umuhimu wa ubatizo wa Kikristo. Kwa hiyo, katika mwaka wa 2004 aliulizwa swali muhimu sana, “Je, umejiweka wakfu kwa Mungu ili ufanye mapenzi yake?” Jairo alijibu swali hilo kwa kuinua macho yake. Alikuwa amepanga mapema kujibu ndiyo kwa njia hiyo. Kwa hiyo alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova akiwa na umri wa miaka 17.

MACHO YANAYOKAZIA MAMBO YA MUNGU

Katika mwaka wa 2011, Jairo alipata njia mpya ya kuwasiliana kwa kutumia kompyuta ya pekee inayoongozwa kwa macho. Kifaa hicho hutambua mwendo wa mboni ya jicho lake na hilo humsaidia kuchagua alama kwenye skrini ya kompyuta. Kwa kupepesa au kukazia jicho alama iliyo kwenye kompyuta ni sawa na kuifungua kwa kutumia kipanya cha kompyuta. Ubao wa pekee uliochorwa picha na ishara ulitengenezwa ili kumsaidia Jairo kuwasiliana. Anapopepesa macho yake kuelekea picha au ishara hizo, programu ya kompyuta hubadili ujumbe wa maandishi ili usikike.

Kadiri Jairo alivyozidi kuelewa Biblia, ndivyo tamaa yake ya kuwasaidia watu wengine kiroho ilivyoongezeka. Tunapojifunza Biblia kila juma tukiwa familia, mara nyingi Jairo huniangalia kisha huitazama kompyuta yake ili kunikumbusha kwamba ninapaswa kumwandikia majibu atakayotoa kwenye mikutano ya Kikristo.

Katika mkutano yeye huangalia skrini ya kifaa hicho na kuchagua jibu atakalotoa kwa kutumia kompyuta hiyo ili kila mtu asikie. Jairo hutabasamu kila mara anapotoa maelezo yanayotia moyo washiriki wa kutaniko. Alex, rafiki kijana wa Jairo, anasema hivi: “Mimi hufurahi sana ninaposikia Jairo akitoa maelezo kuhusu Biblia.”

Jairo hutumia kompyuta ya pekee inayoongozwa na macho yake ili kutoa majibu katika mikutano na pia kuwaeleza wengine kuhusu imani yake

Jairo hutumia macho yake pia kuwaeleza wengine kuhusu imani yake. Njia moja anayotumia kufanya hivyo ni kwa kuchagua picha inayoonyesha bustani yenye wanyama na watu wa kabila zote wakiishi kwa amani. Baada ya kuchagua picha hiyo, kompyuta yake hutoa sauti na kusema, “Biblia inaahidi kwamba dunia itakuwa paradiso na kifo na magonjwa havitakuwapo tena, Ufunuo 21:4.” Ikiwa mtu anayemsikiliza anapendezwa na ujumbe huo, Jairo humwuliza hivi kupitia kompyuta, “Je, ungependa tujifunze Biblia pamoja?” Kwa kushangaza, babu yetu alikubali kujifunza Biblia Jairo alipomwuliza hivyo. Inasisimua sana kumwona Jairo akisaidiwa na Shahidi mwenzake wakimfundisha Babu Biblia! Tulifurahi sana Babu alipobatizwa katika kusanyiko la eneo lililofanywa jijini Madrid, mwezi wa Agosti 2014.

Walimu wa shule anayosoma Jairo wanaiona bidii yake ya kumtumikia Mungu. Rosario, mmoja wa wataalamu wa usemi wanaomsaidia Jairo alisema hivi: “Ikiwa nitafikiria kujiunga na dini, nitakuwa Shahidi wa Yehova. Nimeona jinsi maisha ya Jairo yamekuwa yenye kusudi kwa sababu ya imani yake, ingawa ana hali ngumu sana.”

Macho ya Jairo hung’aa kila mara ninapomsomea ahadi hii ya Biblia: “Kilema atapanda juu kama vile paa anavyofanya, na ulimi wa bubu utapaaza sauti kwa furaha.” (Isaya 35:6) Ingawa wakati mwingine huvunjika moyo, kwa ujumla Jairo ni mwenye furaha. Yeye huwa na furaha kwa sababu anatumia maisha yake kumtumikia Mungu na kushirikiana na marafiki zake Wakristo. Mtazamo wa Jairo wenye furaha na imani yake yenye nguvu ni uthibitisho wa kwamba tunapomtumikia Yehova tunakuwa na kusudi maishani licha ya hali ngumu.

^ fu. 5 Cerebral Palsy (CP) ni aina fulani ya ugonjwa wa kupooza kwa ubongo unaofanya mtu ashindwe kutembea au hata kusonga. Ugonjwa huo unaweza kumfanya mtu aanguke ni kana kwamba ana kifafa, apate matatizo ya kula, na ashindwe kuzungumza vizuri. Ugonjwa wa kupooza ubongo unaoitwa Spastic quadriplegia ndio mbaya zaidi kati ya magonjwa yote ya kupooza ubongo kwani unaweza kumfanya mgonjwa akakamae mikono na miguu na hata kusababisha shingo yake ilegee.