Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu Anaitwa Nani?

Mungu Anaitwa Nani?

Unapotaka kumjua mtu, kwa kawaida jambo la kwanza utakalofanya ni kumwuliza, “Unaitwa nani?” Ungepata fursa ya kumwuliza Mungu swali hilo, unafikiri angejibuje?

“Mimi ni Yehova. Hilo ndilo jina langu.”Isaya 42:8.

Je, umewahi kusikia jina hilo? Inaelekea hujawahi, kwa sababu watafsiri wengi wa Biblia wameliondoa kabisa au kulitumia mara chache sana. Mara nyingi wao hutumia jina la cheo “BWANA.” Hata hivyo, jina la Mungu linapatikana mara 7,000 hivi katika nakala za awali za Biblia. Katika Kiebrania, jina hilo huandikwa kwa kutumia konsonanti nne, zilizo sawa na YHWH, na kwa miaka mingi limekuwa likitamkwa “Yehova” katika Kiswahili.

Jina la Mungu linapatikana kotekote kwenye nakala za Kiebrania na katika tafsiri nyingi za Biblia

Kitabu cha Zaburi cha Bahari ya Chumvi Kati ya mwaka 30 hadi 50, KIEBRANIA

Tafsiri ya Tyndale 1530, KIINGEREZA

Tafsiri ya Reina-Valera 1602, KIHISPANIA

Union Version 1919, KICHINA

KWA NINI NI MUHIMU KUJUA JINA LA MUNGU?

Mungu mwenyewe analiona jina hilo kuwa muhimu sana. Hakuna mtu aliyempatia Mungu jina hilo; alilichagua mwenyewe. Yehova alisema hivi: “Hilo ndilo jina langu milele, na hivyo ndivyo ninavyopaswa kukumbukwa kizazi baada ya kizazi.” (Kutoka 3:15) Katika Biblia, jina la Mungu, Yehova, linapatikana mara nyingi zaidi kuliko majina yake ya cheo kama vile Mweza-Yote, Baba, Bwana, au Mungu, na mara nyingi kuliko jina la mtu yeyote kama vile Abrahamu, Musa, Daudi, au Yesu. Isitoshe, Yehova anataka watu wajue jina lake. Biblia inasema: “Na watu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.”—Zaburi 83:18.

Yesu analiona jina hilo kuwa muhimu. Katika sala ambayo watu wengi huiita Sala ya Bwana, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake wasali hivi kwa Mungu: “Jina lako na litakaswe.” (Mathayo 6:9) Yesu mwenyewe alisali hivi kwa Mungu: “Baba, litukuze jina lako.” (Yohana 12:28) Jambo muhimu zaidi maishani mwa Yesu lilikuwa kutukuza jina la Mungu, na ndio sababu alisali hivi: “Nimewajulisha jina lako nami nitalijulisha.”—Yohana 17:26.

Jina hilo ni muhimu kwa wale wanaomjua Mungu. Watumishi wa kale wa Mungu walielewa kwamba ili walindwe na kuokolewa, walihitaji kujua na kuliheshimu jina la pekee la Mungu. “Jina la Yehova ni mnara wenye nguvu. Mwadilifu hukimbilia humo na kupata ulinzi.” (Methali 18:10) “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.” (Yoeli 2:32) Biblia inaonyesha kwamba jina la Mungu lingewatofautisha waabudu wake na watu wengine. “Kwa maana mataifa yote yatatembea, kila taifa katika jina la mungu wake, lakini sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu milele na milele.”—Mika 4:5; Matendo 15:14.

JINA LA MUNGU LINAFUNUA NINI?

Jina Yehova linamtambulisha Mungu kwa njia ya pekee. Wasomi wengi wa Biblia husema kwamba maana ya jina Yehova ni, “Yeye Husababisha Kuwa.” Yehova Mungu alidokeza maana ya jina lake alipojitambulisha kwa Musa kwa kutumia maneno haya: “Nitakuwa Kile Ninachochagua Kuwa.” (Kutoka 3:14) Hivyo, jina la Mungu lina maana pana zaidi ya kufunua daraka lake akiwa Muumba wa vitu vyote. Jina hilo linafunua uwezo wake wa kuwa chochote anachotaka na vilevile kusababisha uumbaji wake uwe chochote anachotaka ili kutimiza kusudi lake. Ingawa majina ya cheo yanaweza kufunua wadhifa, mamlaka, au nguvu za Mungu, ni jina Yehova tu linalomfafanua kikamili na kuonyesha kile anachoweza kuwa.

Jina hilo linaonyesha kwamba tuna thamani machoni pa Mungu. Maana ya jina la Mungu inabeba wazo la kwamba Yehova anajali sana uumbaji wake, kutia ndani sisi, na kamwe hatautelekeza. Vilevile, kwa kuwa Mungu ametujulisha jina lake, ni wazi kwamba anataka tumjue. Isitoshe, yeye alitujulisha jina lake hata kabla hatujawazia kumwuliza anaitwa nani. Kwa kweli, Yehova hataki tumwone kama Mungu asiyeeleweka ambaye yuko mbali na sisi, badala yake anataka tumwone kama Mtu halisi tunayeweza kusitawisha uhusiano wa karibu naye.—Zaburi 73:28.

Tunapotumia jina la Mungu tunaonyesha kwamba tunampenda. Wazia kwamba umemwomba mtu unayetaka awe rafiki yako awe akikuita kwa kutumia jina lako. Ungehisije ikiwa mtu huyo anakataa katakata kutumia jina lako? Inaelekea kwamba baada ya muda utaanza kuwa na mashaka ikiwa kweli mtu huyo anataka muwe marafiki. Ndivyo ilivyo na Mungu. Yehova ametuambia jina lake na anataka tulitumie. Tunapolitumia, tunaonyesha kuwa tunataka tuwe rafiki zake. Ndiyo sababu anawakazia uangalifu “wale wanaolitafakari [au, “wanaolithamini,” maelezo ya chini] jina lake”!—Malaki 3:16.

Kujua jina la Mungu ni hatua ya kwanza muhimu ya kumkaribia. Lakini si ya mwisho. Tunahitaji kumjua Yule anayewakilishwa na jina hilo, yaani, tujifunze sifa zake.

MUNGU ANAITWA NANI? Mungu anaitwa Yehova. Jina hilo pekee ndilo linalofunua uwezo wa Mungu wa kutimiza kusudi lake