Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu Ana Sifa Gani?

Mungu Ana Sifa Gani?

Kadiri tunavyojua sifa za mtu, ndivyo tunavyomfahamu vizuri, na urafiki wetu unaimarika zaidi. Vivyo hivyo, kadiri tunavyojua sifa za Yehova, ndivyo tunavyomjua vizuri, na urafiki wetu unazidi kusitawi. Ingawa Mungu ana sifa nyingi nzuri, sifa zake kuu ni: nguvu, hekima, haki, na upendo.

MUNGU ANA NGUVU

“Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova! Tazama! Uliumba mbingu na dunia kwa nguvu zako kuu.” YEREMIA 32:17.

Uumbaji hufunua nguvu za Mungu. Kwa mfano, wewe huhisije unaposimama nje jua kali linapokuwa linawaka? Miale ya jua inakuchoma, sivyo? Hizo ni nguvu za uumbaji wa Yehova. Jua lina nguvu kadiri gani? Inasemekana kwamba kiwango cha joto kwenye jua lenyewe ni nyuzi 15,000,000 Selsiasi. Kila sekunde, jua hutoa nishati ambayo ni sawa na mlipuko wa mamia ya mamilioni ya mabomu ya nyuklia.

Hata hivyo, jua ni dogo sana likilinganishwa na matrilioni ya nyota nyingine zilizo angani. Wanasayansi wanakadiria kwamba kipenyo cha moja kati ya nyota zilizo kubwa sana, inayoitwa UY Scuti, ni kirefu mara 1,700 kuliko kile cha jua. Ikiwa UY Scuti ingekuwa mahali jua lilipo, ingeimeza dunia na hata njia ambayo sayari ya Sumbula (Jupiter) hupita. Kwa kweli, hilo linatusaidia kuelewa vizuri maneno ya Yeremia kwamba Yehova Mungu aliuumba ulimwengu, yaani, mbingu na dunia, kwa nguvu zake kuu.

Nguvu za Mungu zinatunufaishaje? Uhai wetu unategemea uumbaji wa Mungu kama vile jua na vitu vingine vya asili vilivyo duniani. Kwa kuongezea, Mungu hutumia nguvu zake kumnufaisha mwanadamu mmoja-mmoja. Jinsi gani? Katika karne ya kwanza, Mungu alitumia nguvu zake kumwezesha Yesu kufanya miujiza. Tunasoma hivi: “Vipofu wanaona, viwete wanatembea, wenye ukoma wanatakaswa, viziwi wanasikia, wafu wanafufuliwa, na maskini wanahubiriwa habari njema.” (Mathayo 11:5) Namna gani leo? Biblia inasema: “Yeye humpa nguvu mtu aliyechoka.” Pia, inasema hivi: “Wale wanaomtumaini Yehova watapata nguvu tena.” (Isaya 40:29, 31) Mungu anaweza kutupatia “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili tuweze kushughulikia au kuvumilia magumu na changamoto tunazokabili maishani. (2 Wakorintho 4:7) Je, huhisi tamaa ya kumkaribia Mungu ambaye kwa upendo anatumia nguvu zake zisizo na mipaka ili kukusaidia?

MUNGU NI MWENYE HEKIMA

“Jinsi kazi zako zilivyo nyingi sana, Ee Yehova! Umezifanya zote kwa hekima.”ZABURI 104:24.

Kadiri tunavyojifunza kuhusu vitu ambavyo Mungu ameumba, ndivyo tunavyostaajabishwa na hekima yake. Ndiyo sababu hata kuna kitengo cha sayansi (biomimetics) ambacho kimekusudiwa kuchunguza uumbaji wa Yehova na kisha kuiga muundo au utendaji wa vitu vya asili ili kuboresha vitu ambavyo wanadamu wanabuni. Vitu hivyo vinatia ndani lenzi za kamera na ndege za abiria na mizigo.

Jicho la mwanadamu linafunua maajabu ya uumbaji wa Mungu

Mwili wa mwanadamu hufunua hekima ya Mungu kwa njia bora zaidi. Kwa mfano, hebu fikiria namna ambavyo mtoto hukua hatua kwa hatua katika tumbo la uzazi. Ukuzi wa mtoto huanza kwa chembe moja tu yenye maagizo yote yanayohitajika. Chembe hiyo hujigawanya na kutokeza chembe nyingine nyingi ambazo mwonekano wake unafanana. Lakini muda fulani unapofika, chembe hizo hubadilika na kufanyiza mamia ya chembe zinazotofautiana, kama vile chembe za damu, chembe za neva, na chembe za mifupa. Baada ya muda, viungo huanza kutokea na kufanya kazi. Kwa miezi tisa tu, mwili wa mtoto hukamilika ukiwa na mabilioni ya chembe zilizotokana na chembe moja tu. Watu wengi wanapoona hekima ya aina hiyo wanakubaliana na maneno ya mwandikaji wa Biblia aliyesema: “Ninakusifu kwa sababu nimeumbwa kwa njia inayoogopesha na kustaajabisha.”—Zaburi 139:14.

Hekima ya Mungu inatunufaishaje? Muumba wetu anajua mambo tunayohitaji ili tuwe na furaha. Kwa kuwa ana ujuzi mwingi na uelewaji, yeye hutupatia ushauri wenye hekima kupitia Neno lake, Biblia. Kwa mfano, Biblia inatushauri hivi: “Endeleeni . . . kusameheana kwa hiari.” (Wakolosai 3:13) Je, ushauri huo unafaa? Ndiyo. Utafiti unaonyesha kwamba kusamehe humwezesha mtu kulala vizuri na kupunguza shinikizo la damu. Pia, kusamehe kunaweza kupunguza uwezekano wa kushuka moyo na kupata matatizo mengine ya afya. Mungu ni kama rafiki mwenye hekima na anayejali, ambaye sikuzote hutupatia ushauri unaofaa na unaotunufaisha. (2 Timotheo 3:16, 17) Je, hungependa kuwa na rafiki kama huyo?

MUNGU HUTENDA KWA HAKI

“Yehova anapenda haki.”ZABURI 37:28.

Nyakati zote, Mungu hutenda yaliyo sawa. Kwa kweli, “Mungu wa kweli hawezi kamwe kuwazia kutenda uovu, na Mweza-Yote hawezi kamwe kutenda kosa!” (Ayubu 34:10) Hukumu zake ni za haki, kama mtunga zaburi alivyosema alipokuwa akimwimbia Yehova: “Utayahukumu mataifa kwa haki.” (Zaburi 67:4) Kwa kuwa “Yehova huona ndani ya moyo,” yeye hawezi kupumbazwa na unafiki, badala yake anaweza kujua ukweli na kuhukumu kwa haki. (1 Samweli 16:7) Kwa kuongezea, Mungu anaona ukosefu wote wa haki na ufisadi unaoendelea, na anaahidi kwamba hivi karibuni “waovu wataangamizwa kutoka duniani.”—Methali 2:22.

Hata hivyo, Mungu si hakimu mkatili aliye na hamu ya kuwaadhibu watu. Yeye huonyesha rehema inapofaa. Biblia inasema kwamba, “Yehova ni mwenye rehema na mwenye huruma,” hata kwa waovu ikiwa wanatubu kutoka moyoni. Hiyo ndiyo haki ya kweli, sivyo?—Zaburi 103:8; 2 Petro 3:9.

Haki ya Mungu inatunufaishaje? Mtume Petro alisema: “Mungu hana ubaguzi, lakini katika kila taifa mtu anayemwogopa na kutenda uadilifu anakubaliwa naye.” (Matendo 10:34, 35) Tunanufaishwa na haki ya Mungu kwa sababu yeye hana ubaguzi wala upendeleo. Anaweza kutukubali tuwe waabudu wake bila kujali rangi yetu, taifa, kiwango cha elimu, au jinsi jamii inavyotuona.

Mungu hana ubaguzi, na sifa zake zinaweza kutunufaisha bila kujali rangi yetu au jinsi jamii inavyotuona

Kwa kuwa Mungu anataka tufaidike na haki yake na tuielewe pia, ametupatia dhamiri. Maandiko hufafanua dhamiri kuwa sheria ‘iliyoandikwa ndani ya mioyo yetu,’ ambayo ‘hututolea ushahidi’ ikiwa mwenendo wetu unafaa au haufai. (Waroma 2:15) Tunanufaikaje? Dhamiri iliyozoezwa vizuri inaweza kutuchochea kuepuka makosa au kutuzuia kutenda kwa njia isiyo ya haki. Na tukifanya kosa, itatusukuma kutubu na kurekebisha mwenendo wetu. Kwa kweli, kuelewa jinsi Mungu anavyotenda kwa haki hutunufaisha na kufanya tutamani awe rafiki yetu!

MUNGU NI UPENDO

“Mungu ni upendo.”1 YOHANA 4:8.

Ingawa Mungu ni mwenye nguvu, hekima, na haki, Biblia haisemi kwamba Mungu ni nguvu, hekima, au haki. Badala yake, inasema Mungu ni upendo. Kwa nini? Kwa sababu nguvu za Mungu humwezesha kutenda, halafu haki na hekima huongoza matendo yake. Lakini upendo ndio humchochea kutenda. Upendo humsukuma kufanya mambo yote anayoyafanya.

Yehova angeweza kuishi peke yake bila viumbe wengine, hata hivyo, upendo ulimchochea kuumba malaika na wanadamu, viumbe ambao wangefaidika na kufurahia kuonyeshwa upendo na yeye. Kwa upendo, aliiumba dunia iwe makao yanayowafaa kabisa wanadamu. Na bado anaendelea kuwaonyesha upendo wanadamu wote, kwa kuwa “yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, na hunyesha mvua juu ya waadilifu na wasio waadilifu.”—Mathayo 5:45.

Kwa kuongezea, “Yehova ni mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema.” (Yakobo 5:11) Mungu huwaonyesha upendo mwororo wale wanaojitahidi kumjua na kumkaribia. Yeye huelekeza uangalifu wake kwa kila mmoja wao. Kwa kweli, “hayuko mbali na kila mmoja wetu.”—Matendo 17:27.

Upendo wa Mungu unatunufaishaje? Sisi hufurahia kuona jua linapotua jioni. Tunafurahi tunaposikia mtoto akicheka. Tunathamini tunapoonyeshwa upendo na familia yetu. Mambo hayo si muhimu ili kuendeleza uhai wetu, lakini hufanya tufurahie maisha kwa kiwango kikubwa sana.

Pia, Mungu ametuonyesha anatupenda kwa kutupatia zawadi ya sala. Biblia inatuhimiza hivi: “Msihangaike kuhusiana na jambo lolote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani, mjulisheni Mungu maombi yenu.” Kama baba mwenye upendo, Yehova anataka tumtafute ili kupata msaada kuhusiana na mahangaiko yaliyo ndani kabisa ya moyo wetu. Na anaahidi kwamba kwa upendo wake usio na ubinafsi, atatupatia “amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote.”—Wafilipi 4:6, 7.

Je, kuchunguza kwa ufupi sifa kuu za Mungu, yaani, nguvu, hekima, haki, na upendo, kumekusaidia kumwelewa vizuri? Tunakutia moyo usome makala zinazofuata ili ujue yale ambayo amefanya na atakayofanya kwa faida yako, na hivyo uweze kumwelewa kwa njia pana zaidi.

MUNGU ANA SIFA GANI? Yehova ana nguvu nyingi, hekima, na hutenda kwa haki kuliko kiumbe yeyote. Hata hivyo, sifa inayotuvutia zaidi ni upendo