Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kukabiliana na Changamoto ya Kuhamia Kutaniko Jipya

Kukabiliana na Changamoto ya Kuhamia Kutaniko Jipya

JE, UMEWAHI kuhamia kutaniko jipya? Ikiwa jibu ni ndiyo, huenda ukakubaliana na Jean-Charles, anayesema hivi: “Si rahisi kuzoea kutaniko jipya na wakati uleule kudumisha hali nzuri ya kiroho ya kila mtu katika familia.” Unapohama, huenda ukahitaji kutafuta kazi, mahali pa kuishi, shule mpya kwa ajili ya watoto, kuzoea hali ya hewa tofauti, utamaduni tofauti, na eneo jipya la kuhubiri.

Nicolas na Céline walikabili changamoto tofauti. Walikubali mgawo wa kuhamia katika kutaniko jipya kutoka katika ofisi ya tawi ya Ufaransa. Wanaeleza hivi: “Mwanzoni tulikuwa tumesisimka sana, lakini baadaye tulianza kuwakosa rafiki zetu. Bado tulikuwa hatujajenga uhusiano wa karibu pamoja na ndugu zetu katika kutaniko jipya.” a Licha ya changamoto hizo, unawezaje kuwa na furaha unapohamia kutaniko jipya? Wengine wanawezaje kukusaidia? Na unaweza kupata baraka gani za kiroho na kuwatiaje moyo wengine katika kutaniko lenu jipya?

KANUNI NNE ZITAKAZOKUSAIDIA KUZOEA KUTANIKO JIPYA

Mtegemee Yehova

1. Mtegemee Yehova. (Zab. 37:5) Kazumi, anayeishi nchini Japani, alihama kutaniko ambalo alikuwa ameshirikiana nalo kwa miaka 20 wakati mume wake alipohamishwa kikazi kwenda eneo lingine. Kazumi ‘alimkabidhi Yehova njia yake’ jinsi gani? Anasema hivi: “Nilimmiminia Yehova moyo wangu na kumweleza kuhusu wasiwasi, upweke, na mahangaiko niliyohisi. Kila mara nilipofanya hivyo, nilipata nguvu nilizohitaji.”

Tunawezaje kumtegemea Yehova zaidi? Kama tu ambavyo mmea unahitaji maji na virutubisho kutoka katika udongo ili kukua, ndivyo imani yetu inavyohitaji chakula cha kiroho ili iwe na nguvu. Nicolas, aliyetajwa awali, alitambua kwamba kutafakari mifano ya Abrahamu, Yesu, na Paulo—wanaume ambao walijidhabihu kwa njia kubwa ili kufanya mapenzi ya Mungu—kuliimarisha uhakika wake katika utegemezo wa Yehova. Kujifunza Biblia kibinafsi kwa ukawaida kutakusaidia kukabiliana na mabadiliko yoyote maishani na pia utajifunza mambo ambayo yatakusaidia kuwatia moyo wengine katika kutaniko lako jipya.

Epuka kulinganisha kutaniko lako la zamani na jipya

2. Epuka kulinganisha kutaniko lako la zamani na jipya. (Mhu. 7:10) Jules alihitaji kukabiliana na tofauti kubwa katika utamaduni alipohama kutoka nchini Benin kwenda Marekani. Jules anakumbuka hivi: “Nilihisi kwamba nilihitaji kumsimulia kila mtu niliyekutana naye historia ya maisha yangu.” Kwa sababu hali zilikuwa tofauti na alizozoea, alianza kujitenga na wengine kutanikoni. Hata hivyo, baada ya kufahamiana vizuri zaidi na ndugu na dada, alibadili mtazamo wake. Anasema hivi: “Sasa ninaamini kwamba mahali popote tulipo duniani, wanadamu wote tuko sawa. Ni kwamba tu wanazungumza na kutenda kwa njia tofauti. Ni muhimu sana kuwakubali watu jinsi walivyo, hata kama utu wao ni tofauti na wetu.” Hivyo, epuka kulilinganisha kutaniko lako la zamani na la sasa. Anne-Lise, dada ambaye ni painia, alisema hivi: “Sikuhamia kutaniko jipya ili kupata nilichokiacha. Nilihamia kutaniko jipya ili nijifunze mambo mapya.”

Wazee wa kutaniko pia wanahitaji kuepuka kulinganisha kutaniko lao la zamani na la sasa. Si kosa kufanya mambo kwa njia tofauti. Ni jambo la hekima kufahamu kwanza hali za eneo ulilohamia kabla ya kutoa mapendekezo. (Mhu. 3:​1, 7b) Ingefaa zaidi kuwawekea kielelezo kizuri, kuliko kuwalazimisha watu kutanikoni wafuate maoni yako.—2 Kor. 1:24.

Uwe na mengi ya kufanya katika kutaniko lako jipya

3. Uwe na mengi ya kufanya katika kutaniko lako jipya. (Flp. 1:27) Kuhamia eneo jipya kunahitaji muda mwingi na jitihada, lakini ni muhimu kuhudhuria mikutano ya kutaniko—uso kwa uso ikiwezekana—mara tu unapofika. Kwa maana, ikiwa watu katika kutaniko lako jipya hawakuoni au wanakuona mara chache sana, wanawezaje kukusaidia? Lucinda, aliyehamia katika jiji kubwa nchini Afrika Kusini pamoja na binti zake wawili, anakumbuka hivi: “Marafiki wangu walinishauri nikazie fikira kujenga uhusiano wa karibu pamoja na watu kutanikoni, kuhubiri pamoja nao, na kushiriki katika mikutano. Pia, tuliwaambia akina ndugu kwamba wanaweza kufanya mikutano ya utumishi katika nyumba yetu.”

‘Kujitahidi pamoja’ na ndugu na dada katika kutaniko lako jipya mnapofanya utendaji wa kitheokrasi ni njia nzuri ya kuchangia katika “imani ya habari njema.” Anne-Lise, aliyetajwa mwanzoni, alitiwa moyo na wazee wa kutaniko ajitahidi kuhubiri na kila mtu. Matokeo yalikuwaje? Anasema hivi: “Mara moja nilitambua kwamba hiyo ndiyo ilikuwa njia bora ya kujihisi nikiwa sehemu ya kutaniko.” Pia, kujitolea katika utendaji, kama vile usafi na udumishaji wa Jumba la Ufalme, kutaonyesha kwamba sasa unaliona kutaniko ulilohamia kuwa kutaniko lako. Kadiri unavyokuwa na mengi ya kufanya kutanikoni, ndivyo akina ndugu na dada watakavyokuzoea haraka zaidi na utajihisi ukiwa sehemu ya familia yako mpya ya kiroho.

Tafuta marafiki wapya

4. Tafuta marafiki wapya. (2 Kor. 6:​11-13) Njia bora ya kuanzisha urafiki ni kwa kuwaonyesha wengine upendezi wa kibinafsi, hivyo jitahidi kutumia muda kabla na baada ya mikutano ili uweze kuwafahamu vizuri zaidi. Jitahidi kadiri uwezavyo kukumbuka majina yao. Kukumbuka majina ya watu na kuwa mchangamfu na mwenye kufikika kutawavutia wengine kwako na bila shaka hilo litakusaidia kupata marafiki wapya wazuri.

Badala ya kujifanya kuwa tofauti na ulivyo ili watu wakupende, waruhusu ndugu na dada zako wapya wakufahamu vizuri. Jifunze kutoka kwa Lucinda ambaye alisema hivi: “Sasa tuna marafiki wa karibu kwa sababu tulichukua hatua ya kwanza ya kuwaalika wengine nyumbani kwetu.”

“MKARIBISHANE”

Huenda baadhi ya watu wakaogopa kuingia kwenye Jumba la Ufalme lililojaa watu wasiowafahamu. Hivyo, unawezaje kufanya iwe rahisi kwa wapya wanapohamia? Mtume Paulo anatutia moyo hivi: “Mkaribishane, kama vile Kristo pia alivyowakaribisha.” (Rom. 15:7) Kwa kumwiga Kristo, wazee wanaweza kuwasaidia wapya wahisi wamekaribishwa. (Tazama sanduku “ Ni Jambo Gani Litakalokusaidia Ufanikiwe Unapohama?”) Hata hivyo, wote kutanikoni, kutia ndani watoto, wanaweza kuanzisha urafiki na wale waliohamia kutanikoni.

Kuwakaribisha wengine kunatia ndani kuwakaribisha nyumbani na pia kuwapa msaada hususa wanaohitaji. Kwa mfano, dada mmoja alitumia wakati kumtembeza dada mwingine mjini na kumwonyesha jinsi ya kutumia usafiri wa umma. Jambo hilo lilimgusa sana dada huyo na kumsaidia kuzoea eneo hilo jipya.

FURSA YA KUKOMAA KIROHO

Nzige anapokua, anatoa ngozi yake ya nje mara kadhaa kabla mabawa yake yawe na uwezo wa kuruka. Vivyo hivyo, unapohamia kutaniko jipya, unahitaji kuondoa wasiwasi wowote unaokuzuia kuruka kwa njia ya mfano, na kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova. Nicolas na Céline wanasema hivi: “Kuhama kunatupatia mazoezi mazuri. Kuzoea watu wapya na mazingira tofauti kulitutia moyo tusitawishe sifa mpya.” Jean-Charles, aliyenukuliwa mwanzoni mwa makala, anaeleza jinsi familia yake ilivyonufaika. Anasema hivi: “Badiliko hili limewasaidia watoto wetu kusitawi katika kutaniko letu jipya. Baada ya miezi michache tu, binti yetu alianza kutoa migawo kwenye mkutano wa katikati ya juma na mwana wetu akawa mhubiri ambaye hajabatizwa.”

Namna gani ikiwa hali zako zinakuzuia kuhamia katika eneo lenye uhitaji? Unaweza kuliona kutaniko lako kuwa jipya kwa kujitahidi kutumia baadhi ya mapendekezo yanayotajwa katika makala hii. Mtegemee Yehova na uwe na mengi ya kufanya kutanikoni kwa kufanya mipango ya kuhubiri na wengine, na kutafuta marafiki wapya au kuimarisha urafiki ambao tayari unao pamoja na wengine. Je, unaweza kuwasaidia wapya au wenye uhitaji kwa kuwapatia msaada hususa? Kwa kuwa upendo ndio unaowatambulisha Wakristo wa kweli, kufanya hivyo kutakusaidia kukomaa kiroho. (Yoh. 13:35) Uwe na uhakika kwamba “Mungu hupendezwa na dhabihu kama hizo.”—Ebr. 13:16.

Licha ya changamoto, Wakristo wengi wamefanikiwa kuwa na furaha katika kutaniko jipya walilohamia—wewe pia unaweza kufanikiwa! Anne-Lise anasema hivi: “Kuhamia kutaniko jipya kulinisaidia kupanuka.” Sasa Kazumi anasadiki kwamba unapohama “unajionea utegemezo wa Yehova katika njia ambazo hujawahi kujionea.” Namna gani kuhusu Jules? Anasema hivi: “Urafiki niliositawisha ulinisaidia kujihisi nikiwa nyumbani. Sasa ninahisi nikiwa karibu sana na watu kutanikoni hivi kwamba haitakuwa rahisi kwangu kuondoka.”

a Ili kupata ushauri wa jinsi ya “Kukabiliana na Tatizo la Kutamani Nyumbani Katika Utumishi wa Mungu,” tazama makala yenye kichwa hicho katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 1994.