Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

“Mwanamke” anayetajwa kwenye Isaya 60:1 ni nani, naye ‘anainukaje’ na ‘kuangaza nuru’?

Isaya 60:1 inasema hivi: “Inuka, Ee mwanamke, angaza nuru, kwa maana nuru yako imekuja. Utukufu wa Yehova unakuangazia.” Muktadha unaonyesha kwamba “mwanamke” huyo alikuwa Sayuni, au Yerusalemu, mji mkuu wa Yuda wakati huo. a (Isa. 60:14; 62:​1, 2) Jiji la Yerusalemu liliwakilisha taifa zima. Maneno ya Isaya yanatokeza maswali mawili: Kwanza, ni lini na jinsi gani jiji la Yerusalemu ‘liliinuka’ na kuangaza nuru ya kiroho? Pili, je, maneno ya Isaya yanatimia kwa njia kubwa zaidi katika siku zetu?

Ni lini na jinsi gani jiji la Yerusalemu ‘liliinuka’ na kuangaza nuru ya kiroho? Yerusalemu na hekalu lake lilikuwa magofu wakati Wayahudi walipokuwa uhamishoni Babiloni kwa miaka 70. Lakini baada ya Wamedi na Waajemi kuwashinda Wababiloni, Waisraeli kutoka sehemu zote za Milki ya Babiloni walikuwa huru kurudi katika nchi yao na kurudisha ibada safi. (Ezra 1:​1-4) Kuanzia mwaka wa 537 K.W.K., mabaki ya Waisraeli waaminifu kutoka makabila yote 12 walifanya hivyo. (Isa. 60:4) Walianza kumtolea Yehova dhabihu, kuadhimisha sherehe mbalimbali, na kujenga upya hekalu. (Ezra 3:​1-4, 7-11; 6:​16-22) Kwa mara nyingine tena, utukufu wa Yehova ulianza kuangaza juu ya Yerusalemu, yaani, watu wa Mungu waliorudishwa. Nao wakawa chanzo cha nuru kwa mataifa ambayo yalikuwa katika giza la kiroho.

Hata hivyo, unabii wa Isaya wa kurudishwa kwa ibada safi ulitimizwa kwa sehemu tu katika Yerusalemu la kale. Waisraeli kwa ujumla hawakuendelea kumtii Mungu. (Neh. 13:27; Mal. 1:​6-8; 2:​13, 14; Mt. 15:​7-9) Baadaye, hata walimkataa Masihi, Yesu Kristo. (Mt. 27:​1, 2) Katika mwaka wa 70 W.K., Yerusalemu na hekalu lake liliharibiwa kwa mara ya pili.

Yehova alitabiri matokeo hayo yenye kusikitisha. (Dan. 9:​24-27) Ni wazi kwamba halikuwa kusudi la Yehova kwa jiji la Yerusalemu lililokuwa duniani kutimiza kila jambo kuhusu unabii wa kurudishwa kwa ibada safi katika Isaya sura ya 60.

Je, maneno ya Isaya yanatimia kwa njia kubwa zaidi katika siku zetu? Ndiyo, lakini kuhusu mwanamke mwingine wa mfano—“Yerusalemu la juu.” Mtume Paulo aliandika hivi: “[Yeye] ni mama yetu.” (Gal. 4:26) Yerusalemu la juu ni sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Mungu, linalofanyizwa na viumbe washikamanifu wa kiroho. Watoto wake wanatia ndani Yesu na Wakristo watiwa-mafuta 144,000, ambao kama Paulo, wana tumaini la kuishi mbinguni. Wakristo watiwa-mafuta wanafanyiza “taifa takatifu”—“Israeli wa Mungu.”—1 Pet. 2:9; Gal. 6:16.

Yerusalemu la juu ‘liliinuka’ na ‘kuangaza nuru’ jinsi gani? Mwanamke huyo alifanya hivyo kupitia watoto wake watiwa-mafuta walio duniani. Linganisha mambo waliyopitia na mambo yaliyotabiriwa kwenye Isaya sura ya  60.

Wakristo watiwa-mafuta walihitaji ‘kuinuka’ kwa sababu walikuwa kwenye giza la kiroho wakati magugu ya uasi-imani yaliyotabiriwa yalipoenea sana katika karne ya pili W.K. (Mt. 13:​37-43) Hivyo, wakawa katika utekwa wa Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwenguni pote ya dini za uwongo. Watiwa-mafuta waliendelea kuwa utekwani hadi “umalizio wa mfumo wa mambo,” kipindi kilichoanza mwaka wa 1914. (Mt. 13:​39, 40) Muda mfupi baadaye, katika mwaka wa 1919, waliwekwa huru na mara moja wakaanza kuangaza nuru ya kiroho kwa kufanya kazi ya kuhubiri kwa bidii. b Kwa miaka mingi, watu kutoka katika mataifa yote wamekuja katika nuru, kutia ndani wale mabaki wa Israeli wa Mungu—“wafalme” wanaotajwa kwenye Isaya 60:3.—Ufu. 5:​9, 10.

Wakati ujao, Wakristo watiwa-mafuta wataangaza nuru ya Mungu katika njia kubwa hata zaidi. Jinsi gani? Watakapomaliza mwendo wao wa kidunia, watakuwa sehemu ya “Yerusalemu Jipya,” au bibi harusi wa Kristo, wale wafalme na makuhani wenzake 144,000.—Ufu. 14:1; 21:​1, 2, 24; 22:​3-5.

Yerusalemu Jipya litakuwa na jukumu muhimu katika utimizo wa Isaya 60:1. (Linganisha Isaya 60:​1, 3, 5, 11, 19, 20 na Ufunuo 21:​2, 9-11, 22-26.) Kama tu ambavyo jiji la Yerusalemu la kidunia lilivyokuwa kitovu cha serikali ya Israeli la kale, ndivyo Yerusalemu Jipya na Kristo watakavyokuwa serikali ya mfumo mpya wa mambo. Yerusalemu Jipya “[linashuka] kutoka mbinguni kwa Mungu” jinsi gani? Kwa kuchukua hatua zinazoinufaisha dunia. Watu wanaomwogopa Mungu kutoka katika mataifa yote ‘watatembea kwa nuru yake.’ Hata watawekwa huru kutokana na dhambi na kifo. (Ufu. 21:​3, 4, 24) Matokeo ni kwamba kutakuwa na “kurudishwa [kikamili] kwa mambo yote,” kama Isaya na manabii wengine walivyotabiri. (Mdo. 3:21) Kurudishwa kwa mambo yote kwa njia hiyo kubwa kulianza wakati Kristo alipokuwa Mfalme na kutaisha mwishoni mwa Utawala wake wa Miaka Elfu Moja.

a Katika Isaya 60:​1, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inatumia neno “mwanamke” badala ya “Sayuni,” au “Yerusalemu,” kwa sababu vitenzi vya Kiebrania vya neno “inuka” na “angaza nuru” viko katika jinsia ya kike. Hivyo, neno “mwanamke” linamsaidia msomaji atambue kwamba anayezungumziwa ni mwanamke wa mfano.

b Kurudishwa kwa ibada safi kulikotokea katika mwaka wa 1919 kunafafanuliwa pia katika Ezekieli 37:​1-14 na Ufunuo 11:​7-12. Ezekieli alitabiri kuhusu kurudishwa kwa hali nzuri ya kiroho kwa Wakristo wote watiwa-mafuta baada ya kipindi kirefu cha kuwa utekwani. Unabii katika kitabu cha Ufunuo unarejelea kuzaliwa upya kiroho kwa kikundi kidogo cha ndugu watiwa-mafuta ambao wameongoza mambo baada ya kipindi kifupi cha kulazimishwa kuwa katika hali ya kutotenda kwa sababu ya kufungwa gerezani isivyo haki. Katika mwaka wa 1919, waliwekwa rasmi kuwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”—Mt. 24:45; tazama Hatimaye Ibada Safi ya Yehova Yarudishwa!, uku. 118.