Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

1 Petro 5:6, 7—“Nyenyekeeni Chini ya Mkono wa Mungu Ulio Hodari, . . . Mkimtwika Yeye Fadhaa Zenu Zote”

1 Petro 5:6, 7—“Nyenyekeeni Chini ya Mkono wa Mungu Ulio Hodari, . . . Mkimtwika Yeye Fadhaa Zenu Zote”

 “Kwa hiyo, jinyenyekezeni chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu, ili awainue kwa wakati unaofaa, huku mkitupa mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye anawajali ninyi.”​—1 Petro 5:6, 7, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake; huku mkimtwika yeye fadhaa zenu zote, kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu.”​—1 Petro 5:6, 7, Union Version.

Maana ya 1 Petro 5:6, 7

 Kupitia maneno hayo, mtume Petro anawahakikishia Wakristo kwamba wanaweza kusali kwa Mungu kuhusu matatizo na mahangaiko yao wakiwa na uhakika. Mungu anawapenda watu wanyenyekevu, naye atawathawabisha sana.

 “Jinyenyekezeni chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu.” Katika Biblia, mara nyingi mkono wa Mungu unarejelea nguvu zake za kuokoa na kulinda. (Kutoka 3:19; Kumbukumbu la Torati 26:8; Ezra 8:22) Wakristo hujinyenyekeza chini ya mkono wa Mungu wanapomtegemea. Wanakubali mipaka yao na kutambua kwamba hawawezi kukabiliana na majaribu bila msaada. (Methali 3:5, 6; Wafilipi 4:13) Wanasadiki kwamba Mungu ana nguvu za kutenda kwa niaba yao kwa wakati unaofaa na kwa njia bora kabisa.​—Isaya 41:10.

 “Ili awainue kwa wakati unaofaa.” Wale wanaovumilia majaribu kwa subira wanaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu atawainua hatimaye, au kuwathawabisha. Hataruhusu waabudu wake wajaribiwe milele au kupita wanavyoweza kuhimili. (1 Wakorintho 10:13) Tofauti na hilo, wakiendelea kutenda mema, hatimaye Mungu atawathawabisha “kwa wakati unaofaa.”​—Wagalatia 6:9.

 “Huku mkitupa mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye anawajali ninyi.” Wakristo wanaweza kutupa, au kumtwika, Mungu mahangaiko yao yote kwa kusali kwake kwa unyenyekevu. Kitabu kimoja cha marejeo kinaeleza hivi: “Kitenzi kutupa kinawakilisha tendo la kutumia nguvu kurusha kitu kikuondokee. Kinafafanua tendo ambalo mtu hufanya kimakusudi.” Mara tu Mkristo anapomtupia Mungu mahangaiko yake, anaweza kupunguza wasiwasi wake na kufurahia kile ambacho Biblia inaita “amani ya Mungu.” (Wafilipi 4:6, 7) Anaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu anataka kumsaidia kwa sababu anajua Mungu anamjali na anaweza kutumia nguvu zake nyingi kumtegemeza.​—⁠Zaburi 37:5; 55:22.

Muktadha wa 1 Petro 5:6, 7

 Sura ya 5 ndiyo mwisho wa barua ya kwanza ambayo mtume Petro aliwaandikia Wakristo. (1 Petro 1:1) Kama tu ilivyo leo, wafuasi wa Kristo walioishi wakati huo, walikabili majaribu mbalimbali ambayo yalijaribu imani yao na ambayo yangeweza kuwafanya wawe na wasiwasi. (1 Petro 1:6, 7) Kwa kuwa Petro alitambua hali ngumu walizokuwa wakikabili, aliwaandikia barua changamfu na yenye kutia moyo katika mwaka wa 62-64 W.K. hivi.​—1 Petro 5:12.

 Petro anamalizia barua yake kwa kikumbusho kinachotia moyo kwa ajili ya wote wanaokabili majaribu kutokana na imani yao. Wakiendelea kuwa wanyenyekevu na kumtegemea Mungu, wanaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu atawasaidia kusimama imara. (1 Petro 5:5-10) Vivyo hivyo, maneno ya Petro yanaweza kuwatia moyo Wakristo ambao leo wanateswa.

 Tazama video hii fupi uone muhtasari wa kitabu cha 1 Petro.