Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Mika 6:8​—“Kwenda kwa Unyenyekevu na Mungu Wako”

Mika 6:8​—“Kwenda kwa Unyenyekevu na Mungu Wako”

 “Ee mwanadamu, amekuambia yaliyo mema. Na Yehova anataka nini kutoka kwako? Anataka tu utekeleze haki, uthamini sana ushikamanifu, na utembee kwa kiasi na Mungu wako!”​—Mika 6:8, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Ee mwanadamu, yeye amekuonyesha yaliyo mema; na BWANA anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!”​—Mika 6:8, Union Version.

Maana ya Mika 6:8

 Nabii Mika anasema kwamba si vigumu kwa wanadamu kumpendeza Yehova a Mungu. (1 Yohana 5:3) Mstari huu unaonyesha kwa ufupi kwamba Mungu anatarajia mambo matatu muhimu kutoka kwetu. Mambo mawili ya kwanza yanahusisha uhusiano pamoja na wanadamu wengine, na jambo la tatu linahusisha uhusiano wa mtu mmoja mmoja pamoja na Mungu.

 “Utekeleze haki.” Mungu anawahimiza waabudu wake watende kwa haki. Hilo linatia ndani kufikiri na kutenda kupatana na viwango vya Mungu vya mema na mabaya. (Kumbukumbu la Torati 32:4) Kwa mfano, watu wanaofuata viwango vya Mungu wanajitahidi kutenda kwa unyoofu kuelekea watu wote, na bila ubaguzi, licha ya malezi yao, taifa wanalotoka, au hali yao ya kiuchumi.​—Mambo ya Walawi 19:15; Isaya 1:17; Waebrania 13:18.

 “Uthamini sana ushikamanifu.” Maneno haya yanaweza kutafsiriwa kuwa “upende upendo mshikamanifu.” (Mika 6:8, maelezo ya chini) Katika lugha ya awali, ya Kiebrania, neno “ushikamanifu” linaashiria zaidi ya kuwa mwaminifu katika uhusiano bali linatia ndani kuonyesha mtu mwingine fadhili na rehema, yaani, kumfanyia zaidi ya yale tunayotarajiwa kufanya. Anawahimiza wale wanaotaka kumpendeza waonyeshe fadhili na rehema na pia wapende au wathamini sifa hizo. Hili linamaanisha kwamba waabudu wake wanapaswa kufurahia kuwasaidia wengine, hasa wale walio na uhitaji. Kutoa huleta shangwe.​—Matendo 20:35.

 “Utembee kwa kiasi na Mungu wako.” Katika Biblia, neno “utembee” linaweza kumaanisha “kufanya mambo kwa njia fulani hususa.” Mtu anatembea pamoja na Mungu kwa kufuata njia ya maisha ambayo inampendeza Mungu. Mfano mmoja ni Noa. “Alitembea pamoja na Mungu wa kweli” kwa sababu alikuwa mwadilifu machoni pa Mungu na “alijithibitisha mwenyewe kuwa mtu asiye na kosa miongoni mwa watu wa siku zake.” (Mwanzo 6:9) Sisi pia, ‘tunatembea pamoja na Mungu’ kwa kuishi kulingana na mafundisho yaliyo katika Neno lake, Biblia. Ili kufanya hivyo, tunahitaji kuwa wenye kiasi, kukubali kwamba hatuna uwezo kamili na kwamba tunahitaji kumtegemea Mungu katika mambo yote.​—Yohana 17:3; Matendo 17:28; Ufunuo 4:11.

Muktadha wa Mika 6:8

 Mika alikuwa nabii katika Israeli la kale katika karne ya nane K.W.K. Wakati huo, nchi ilikuwa imejaa ibada ya sanamu, udanganyifu, na ukandamizaji. (Mika 1:7; 3:1-3, 9-11; 6:10-12) Waisraeli wengi walikuwa wakipuuza matakwa ya Mungu yaliyokuwa yameandikwa katika Sheria aliyopewa Musa, inayoitwa Sheria ya Musa. Wakati huo, watu wengi walifikiri kimakosa kwamba wangeweza kupata kibali cha Mungu kwa kushiriki tu tamaduni fulani za kidini na kutoa dhahibu.​—Methali 21:3; Hosea 6:6; Mika 6:6, 7.

 Karne nyingi baada ya kipindi ambacho Mika aliishi, Yesu alirejelea tena maneno hayo na kusemakwamba Baba yake anapendezwa na wale wanaoonyesha upendo, haki, na rehema lakini anachukizwa na wale wanaofanya mambo tu ili watu wengine waone kuwa wanamtumikia Mungu. (Methali 21:3; Hosea 6:6; Mika 6:6, 7) Maneno ya Yesu yanatusaidia kuelewa yale ambayo Mungu anatarajia kutoka kwa waabudu wake leo.

 Tazama video hii fupi ili upate habari zaidi kuhusu kitabu cha Mika.

a Jina Yehova ni tafsiri ya Kiswahili ya jina la Kiebrania la Mungu, yaani, herufi hizi nne: יהוה (YHWH), zinazojulikana kama Tetragramatoni. Katika Biblia ya Union Version, jina hili limeandikwa “BWANA.” Ili kujua mengi zaidi kumhusu Yehova na sababu zinazofanya tafsiri nyingine za Biblia kutumia majina mengine badala ya hili, ona makala yenye kichwa “Yehova Ni Nani?