Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kudhibiti Wasiwasi

Jinsi ya Kudhibiti Wasiwasi

 Kuwa na wasiwasi kupita kiasi kunaweza kuathiri mwili na hisia zako. Hata kunaweza kukusababishia matatizo makubwa zaidi ya tatizo ambalo awali lilifanya uwe na wasiwasi.

Madokezo ya jinsi ya kudhibiti wasiwasi

  •  Punguza kiasi cha habari mbaya unazopata. Si lazima upate taarifa kuhusu kila tatizo linaloendelea ulimwenguni. Kufuatilia kupita kiasi taarifa mbaya kutakuongezea hofu na kukuvunja moyo.

     Kanuni ya Biblia: “Roho iliyopondeka humfyonza mtu nguvu.”—Methali 17:22.

     “Ni rahisi sana kuzoea kupata habari mpya na zenye kushtua, lakini hilo si jambo zuri. Wasiwasi wangu hupungua sana ninapopunguza kiasi cha habari ninazopata.”—John.

     Jambo la kufikiria: Ni mara ngapi ambazo kwa kweli unahitaji kupata habari za karibuni zaidi?

  •  Uwe na ratiba na uifuate. Amka mapema, kula chakula, fanya kazi za nyumbani, na lala wakati uleule kwa kufuata ratiba yako. Kuwa na ratiba kutakusaidia uhisi kwamba mambo hayajabadilika maishani mwako, na hilo litakupunguzia wasiwasi.

     Kanuni ya Biblia: “Mipango ya wenye bidii hakika huleta mafanikio.”—Methali 21:5.

     “Ugonjwa wa COVID-19 ulipoanza, niliacha kabisa kufuata ratiba yangu, nilitumia wakati mwingi kutazama burudani. Nilitaka kutumia vizuri wakati wangu, hivyo nilipanga ratiba ya mambo ninayopaswa kufanya kila siku.”—Joseph.

     Jambo la kufikiria: Je, una ratiba inayokusaidia uhisi kwamba umetimiza jambo fulani kila siku?

  •  Kazia fikira mambo mazuri. Kukazia fikira hali mbaya na ambazo huwezi kubadili kutakufanya uzidi kuwa na wasiwasi. Badala yake, fikiria mambo mawili au matatu yanayofanya uwe mwenye shukrani.

     Kanuni ya Biblia: “Mjionyeshe kuwa wenye shukrani.”—Wakolosai 3:15.

     “Kusoma Biblia hunisaidia kuepuka kutafuta habari mbaya na badala yake kukazia fikira mambo mazuri. Huenda hilo likaonekana kuwa jambo rahisi sana, lakini ni jambo la uhakika!”—Lisa.

     Jambo la kufikiria: Je, wewe hukazia fikira mambo mabaya unayokabili maishani na kusahau mambo mema?

  •  Wafikirie wengine. Badala ya kujitenga—jambo ambalo ni rahisi kufanya hasa ukiwa na wasiwasi—fikiria namna unavyoweza kuwasaidia walio na uhitaji.

     Kanuni ya Biblia: “Mkiangalia, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.”—Wafilipi 2:4.

     “Kuwasaidia wengine huniletea furaha. Ninafanya mambo ambayo yatawafanya wahisi vizuri, na wakati uleule, ninapunguza wasiwasi wangu. Kwa kweli, ninakosa muda wa kuwa na wasiwasi.”—Maria.

     Jambo la kufikiria: Kati ya watu unaowajua, ni nani walio na uhitaji wa pekee, na unaweza kuwasaidiaje?

  •  Tunza afya yako. Fanya mazoezi na pumzika vya kutosha. Kula vyakula vyenye afya. Kutunza afya yako kunaweza kuboresha mtazamo wako kuhusu maisha na kukusaidia kuondoa wasiwasi wowote ulio nao.

     Kanuni ya Biblia: “Mazoezi ya kimwili ni yenye faida.”—1 Timotheo 4:8, maelezo ya chini.

     “Mimi na mwana wangu hatuwezi kufanya mazoezi nje kama tunavyopenda, hivyo tuna ratiba ya kufanya mazoezi ndani ya nyumba. Kufanya hivyo kumetusaidia tuhisi vizuri na kutendeana kwa fadhili.”—Catherine.

     Jambo la kufikiria: Je, unahitaji kuboresha mlo wako na kufanya mazoezi zaidi ili uwe na afya njema?

 Mbali na kutumia madokezo hayo ili kupunguza wasiwasi, watu wengi wamenufaika na kujifunza kuhusu tumaini hakika la wakati ujao linalopatikana katika Biblia. Ona makala “Ufalme wa Mungu Utatimiza Nini?