Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SOMO LA 8

Wakati Musiba Unatokea

Wakati Musiba Unatokea

‘Munashangilia sana katika jambo hilo, ingawa kwa muda kidogo sasa, ikiwa ni lazima, mumehuzunishwa na majaribu ya namna mbalimbali.’​—1 Petro 1:6

Hata ikiwa unafanya yako yote ili kuwa na ndoa na familia yenye furaha, mambo ambayo hautazamie yanaweza kutokea na kufanya iwe vigumu kulinda furaha yako. (Mhubiri 9:11) Kwa upendo, Mungu anatusaidia wakati tunapambana na matatizo. Kutumikisha kanuni za Biblia kutakusaidia wewe na familia yako mupambane hata na matatizo makali sana.

1 MUMUTEGEMEE YEHOVA

MAMBO AMBAYO BIBLIA INASEMA: ‘Mutupe mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye anawajali ninyi.’ (1 Petro 5:7) Sikuzote mukumbuke kwamba si Mungu ambaye analeta majaribu. (Yakobo 1:13) Kadiri munaendelea kumukaribia, atawasaidia. (Isaya 41:10) ‘Mumimine mioyo yenu mbele zake.’​—Zaburi 62:8.

Mutapata pia faraja wakati mutasoma na kujifunza Biblia kila siku. Mwishowe, mutatambua namna Yehova ‘anatufariji katika ziki yetu yote.’ (2 Wakorintho 1:3, 4; Waroma 15:4) Anaahidi kuwapatia “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.”​—Wafilipi 4:6, 7, 13.

MAMBO YA KUFANYA:

  • Mumuombe Yehova awasaidie kubaki watulivu na kuwa na maoni yanayofaa juu ya misiba

  • Mufikirie mambo yote munayoweza kufanya na mufanye uamuzi muzuri zaidi

2 UJITUNZE WEWE NA FAMILIA YAKO

MAMBO AMBAYO BIBLIA INASEMA: ‘Moyo wa mutu mwenye uelewaji unajipatia ujuzi, nalo sikio la wenye hekima linatafuta kupata ujuzi.’ (Methali 18:15) Tafuta kujua habari zote juu ya familia yako. Jua mahitaji ya kila mushiriki wa familia. Zungumuza nao. Wasikilize.​—Methali 20:5.

Unaweza kufanya nini ikiwa mutu ambaye unapenda anakufa? Usijizuie kuonyesha huzuni yako. Kumbuka kwamba hata Yesu ‘alitokwa na machozi.’ (Yohana 11:35; Mhubiri 3:4) Ni lazima pia kupumuzika na kulala vya kutosha. (Mhubiri 4:6) Kufanya hivyo kutakusaidia upambane na hali yenye kuhuzunisha.

MAMBO YA KUFANYA:

  • Uzoee kuzungumuza na familia yako mbele hata ya musiba kutokea. Wakati matatizo yanatokea, hawataogopa kuongea na wewe

  • Zungumuza na wengine ambao wamekwisha kupambana na hali kama hiyo

3 TAFUTA MUSAADA

MAMBO AMBAYO BIBLIA INASEMA: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.” (Methali 17:17) Rafiki zako wanataka kukusaidia, lakini pengine hawajue namna gani wanaweza kukusaidia. Usijizuie kuwaambia mambo ambayo unahitaji kabisa. (Methali 12:25) Tena, tafuta musaada wa kiroho kwa watu ambao wanaelewa Biblia. Muongozo wa Biblia ambao watakutolea utakusaidia.​—Yakobo 5:14.

Utapata musaada ambao unahitaji ikiwa unapitisha wakati kwa ukawaida na watu ambao wanamuamini kabisa Mungu na ambao wanatumainia ahadi zake. Tena, utafarijiwa sana wakati utawasaidia wale wanaohitaji kutiwa moyo. Zungumuza nao juu ya imani yako katika Yehova na katika ahadi zake. Endelea kuwa na mengi ya kufanya katika kuwasaidia wale walio katika uhitaji, na usijitenge na watu ambao wanakupenda na kukuhangaikia.​—Methali 18:1; 1 Wakorintho 15:58.

MAMBO YA KUFANYA:

  • Muelezee rafiki wako wa karibu matatizo yako na ukubali musaada wake

  • Ueleze waziwazi mahitaji yako na useme kweli