Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

BIBLIA INABADILISHA MAISHA YA WATU

Nilielewa Kama Yehova Ni Mwenye Huruma na Mwenye Kusamehe

Nilielewa Kama Yehova Ni Mwenye Huruma na Mwenye Kusamehe
  • ALIZALIWA MWAKA WA: 1954

  • INCHI: KANADA

  • ALIKUWA: ANADANGANYA WATU, NA KUCHEZA MICHEZO YA FEZA

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilikomalia katika eneo masikini katika muji wa Montréal.

Wakati nilikuwa na miezi sita, baba yangu alikufa, na mama yangu alibakia na kazi ya kutunza familia yote. Nilikuwa mutoto wa mwisho katika familia ya watoto munane.

Wakati nilikuwa ninakomaa, maisha yangu ilitawaliwa na dawa za kulewesha, jeuri, na nilikuwa ninajiunga na vikundi vyenye kutendea watu mubaya. Wakati nilikuwa na miaka 10, nilianza kutumikia makahaba na watu wenye kukopesha feza ili kuomba faida ya juu sana; nilikuwa ninaenda kuwanunulia vitu. Mara nyingi nilikuwa ninasema uwongo, na nilifurahia kudanganya watu kwa njia yoyote ili kuwaiba feza. Kwangu, hilo lilikuwa kama dawa ya kulewesha.

Wakati nilikuwa na miaka 14, nilikuwa nimejua kutunga njia nyingi za kudanganya watu. Kwa mufano, nilikuwa ninanunua saa za mukononi, vikomo, na vitu vya masikio vyenye kupakwa zahabu kidogo na ninaandika kwenye vitu hivyo kuwa vimetengenezwa kwa zahabu nyingi. Kisha nilikuwa ninaviuzisha katika barabara, na mahali watu wanasimamisha motokari katika eneo la biashara. Nilifurahia sana kupata feza bila kuchoka. Wakati fulani, nilipata dola 10000 katika siku moja tu!

Wakati nilikuwa na miaka 15, nilifukuzwa kwenye masomo ya kufundisha watoto tabia ya muzuri. Sikukuwa tena na mahali pa kuishi. Nilikuwa ninalala katika mabarabara, mabustani, ao katika nyumba za marafiki fulani.

Kwa sababu ya mambo yenye nilikuwa ninafanya ili kudanganya watu, mara nyingi polisi walinisambisha. Sikuwa ninauzisha vitu vya wizi; kwa hiyo hakuna siku walinifunga katika gereza. Lakini walinilipisha feza nyingi kwa sababu ya kudanganya watu, kuuzisha vitu vya uongo, na kuuzisha bila kuwa na karatasi ya kuniruhusu. Sikuwa ninaogopa mutu yeyote; hata nilikusanya feza kwa ajili ya watu wenye kukopesha feza ili kuomba faida ya juu sana. Ilikuwa hatari sana kufanya kazi hiyo, na wakati fulani nilibeba bunduki. Tena nilitumika na vikundi vya watu wenye walikuwa wanapanga na kufanya mambo mabaya.

BIBLIA ILIBADILISHA MAISHA YANGU:

Nilisoma Biblia kwa mara ya kwanza wakati nilikuwa na miaka 17. Nilikuwa ninaishi pamoja na rafiki yangu mwanamuke wakati alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Lakini sikukubali mambo yenye Biblia inasema juu ya mwenendo muzuri, kwa hiyo nilimuacha na nikaenda kuishi na mwanamuke mwengine mwenye nilikuwa ninachumbia.

Badiliko kubwa katika maisha yangu lilitokea wakati rafiki yangu wa pili mwanamuke alianza pia kujifunza na Mashahidi wa Yehova! Alifanya mabadiliko katika maisha yake, na nilishangaa kuona namna alikuwa sasa mupole na muvumilivu zaidi. Nilikubali wakati nilialikwa kwenye mukutano kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Watu wenye walinikaribisha walikuwa wenye heshima na wapole. Walikuwa tofauti kabisa na watu wenye nilikuwa ninajua! Hakuna siku nilijisikia kuwa watu wa familia yangu wananihangaikia; wakati nilikuwa mutoto sikujisikia kuwa kuna mutu ananipenda kabisa. Uchangamufu wenye Mashahidi wa Yehova walinionyesha ndilo jambo nilikuwa ninatamani kabisa. Wakati Mashahidi wa Yehova waliniambia kuwa wanapenda kunifundisha Biblia, nilikubali kwa furaha.

Pengine mambo yenye nilikuwa ninajifunza katika Biblia yaliokoa uzima wangu. Mimi na wenzangu wawili tulikuwa tunapanga kuiba mahali fulani ili niweze kulipa deni ya zaidi ya dola 50000. Ni michezo ya feza ndiyo iliniingiza katika deni hiyo. Ninafurahi sana kuona nilijiondoa katika mupango huo! Wenzangu hao waliendelea na mupango huo. Mumoja alikamatwa na mwengine aliuawa.

Wakati niliendelea kujifunza Biblia nilitambua kuwa nilipaswa kufanya mabadiliko mengi katika maisha yangu. Kwa mufano, nilijifunza mambo haya yenye Biblia inasema katika andiko la 1 Wakorintho 6:10: ‘Wala wezi, wala watu wenye pupa, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyanganyi hawataurithi Ufalme wa Mungu.’ Wakati nilisoma andiko hilo nilitokwa na machozi kwa sababu niliona kuwa nilikuwa na mwenendo mubaya sana. Nilitambua kama nilipaswa kubadilisha kabisa maisha yangu. (Waroma 12:2) Nilikuwa ninapenda kupigana, nilikuwa mukali, na maisha yangu yote ilitawaliwa na uongo.

Lakini wakati nilikuwa ninajifunza Biblia, nilielewa pia kama Yehova ni mwenye huruma na mwenye kusamehe. (Isaya 1:18) Nilisali kwa bidii, nilimuomba sana Yehova anisaidie ili niweze kuacha maisha yangu ya zamani. Kwa sababu Yehova alinisaidia, nilibadilisha maisha yangu pole kwa pole. Nilifikia jambo la maana sana wakati mimi na rafiki yangu mwanamuke tuliandikisha ndoa yetu kwenye serikali.

Leo ninaendelea kuishi kwa sababu ninatumia kanuni za Biblia

Nilikuwa na miaka 24 na nilikuwa na watoto watatu wakati nilioa. Nilipaswa sasa kutafuta kazi yenye kupatana na sheria. Lakini nilikuwa na masomo ya chini na sikukuwa na karatasi yenye kuonyesha kama nilitumika mahali fulani. Wakati huo nilisali tena kwa bidii. Kisha nilienda kutafuta kazi. Niliambia watu wenye nilikuwa ninaomba kazi kama nilipenda kubadilisha maisha yangu na kufanya kazi yenye kuheshimika. Wakati fulani, niliwaambia kuwa nilikuwa ninajifunza Biblia na nilipenda kabisa kuwa mutu muzuri. Wengi walikataa kunipatia kazi. Mwishowe, wakati niliomba kazi kwa mutu fulani, nilimuelezea waziwazi maisha yangu yote mabaya ya zamani. Mutu huyo alisema hivi: “Sijue ni sababu gani, lakini ninajisikia kuwa inafaa tu nikupe kazi.” Ninaamini kama hiyo ilikuwa jibu kwa sala zangu. Kisha wakati fulani, mimi na bibi yangu tulibatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova.

FAIDA YENYE NIMEPATA:

Leo ninaendelea kuishi kwa sababu ninatumia kanuni za Biblia na ninaishi maisha ya Kikristo. Niko na familia ya muzuri. Niko na zamiri safi kwa sababu niko hakika kama Yehova amenisamehe makosa yangu.

Katika miaka 14 yenye imepita, nimetumia saa 70 hivi kila mwezi katika mahubiri ili kusaidia wengine wajifunze mambo Biblia inafundisha. Hivi karibuni bibi yangu ameanza kufanya kama mimi. Katika miaka 30 yenye imepita, nimefurahi kusaidia watu 22 wenye ninatumika nao waanze kumuabudu Yehova. Ningali ninaenda katika maeneo ya biashara, lakini siende huko ili kudanganya watu kama vile nilikuwa ninafanya zamani. Sasa wakati ninaenda huko, mara nyingi ninaelezea wengine mambo ninaamini. Ninapenda kuwatolea kitu fulani, ni kusema, tumaini la kuishi katika dunia mupya yenye haitakuwa na watu wenye kudanganya wengine.—Zaburi 37:10, 11.