Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MAWAZO YA BIBLIA

Michezo ya Feza

Michezo ya Feza

Watu fulani wanaona michezo ya feza kuwa njia ya kujifurahisha isiyokuwa na hatari yoyote, lakini wengine wanaiona kuwa tabia ya hatari sana.

Ni mubaya kucheza michezo ya feza?

MAMBO WATU WANASEMA

Watu wengi wanaona michezo ya feza kuwa njia ya kujifurahisha isiyokuwa na hatari yoyote, ikiwa tu inafanywa kulingana na sheria. Aina fulani za michezo ya feza inayokubaliwa na sheria, kama vile michezo ya bahati yenye kupangwa na serikali, inasaidia kupata feza kwa ajili ya mipango yenye kuletea watu wote faida.

MAMBO BIBLIA INASEMA

Biblia haizungumuzie sana michezo ya feza. Lakini inatoa kanuni mbalimbali zenye zinaweza kutusaidia tujue namna Mungu anaona michezo hiyo.

Kusudi la kwanza la michezo ya feza ni kupata feza zenye wengine wamepoteza. Hilo linapingana na onyo la Biblia lenye kusema ‘tujilinde na kila namna ya tamaa.’ (Luka 12:15) Michezo ya feza inachochewa na pupa (tamaa). Mashirika yenye kusimamia michezo ya feza yanaahidi watu feza nyingi, lakini hayaonyeshe ikiwa ni kweli watu wataweza katika michezo hiyo. Wanafanya hivyo kwa sababu wanajua kama tamaa ya kupata mali inachochea wachezaji kutia feza nyingi katika majumba ya michezo. Michezo ya feza haisaidie mutu kujilinda na pupa, lakini inachochea tamaa ya kupata feza kwa vyepesi.

Michezo ya feza inategemea muradi huu wa asili wa kujifikiria mwenyewe: kupata feza zenye wachezaji wengine wamepoteza. Lakini, Biblia inatia moyo kila mutu ‘aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali [lakini] ile ya yule mutu mwengine.’ (1 Wakorintho 10:24) Na amri moja kati ya Amri Kumi inasema hivi: ‘Usitamani . . . [kitu] chochote cha mwenzako.’ (Kutoka 20:17) Wakati muchezaji anakusudia sana kupata ushindi, ni kama vile anatumaini wengine wapoteze feza ili yeye azipate.

Pia Biblia inatuonya tusione bahati kama nguvu fulani isiyokuwa ya kawaida yenye inaweza kuleta baraka. Katika taifa la Israeli la zamani, watu fulani walikosa imani kwa Mungu na walianza ‘kuandaa meza kwa ajili ya mungu wa Bahati Njema.’ Mungu alikubali watu wajitoe hivyo kwa “mungu wa Bahati Njema?” Hapana, aliwaambia hivi: ‘Muliendelea kufanya yaliyokuwa mabaya machoni pangu.’—Isaya 65:11, 12.

Kwa kweli, katika inchi fulani michezo ya feza yenye kukubaliwa na sheria inasaidia kupata feza za kutumia katika mipango ya masomo, maendeleo katika mambo ya feza, na mipango mingine ya kusaidia watu wote. Lakini namna feza hizo zinatumiwa haibadilishe namna zilipatikana, ni kusema, kupitia matendo yenye kuchochea waziwazi pupa na kujifikiria, na wazo la kupata kitu fulani kwa bure.

‘Usitamani . . . [kitu] chochote cha mwenzako.’—Kutoka20:17.

Michezo ya feza inaweza kumuletea muchezaji matokeo gani mabaya?

MAMBO BIBLIA INASEMA

Biblia inatuonya kuwa ‘wale ambao wameazimia kuwa matajiri wanaanguka katika jaribu na mutego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kuzuru, ambazo zinatumbukiza watu katika maangamizi na uharibifu.’ (1 Timotheo 6:9) Pupa ndiyo inachochea mutu kucheza michezo ya feza, na pupa inaharibu sana. Ndiyo maana Biblia inataja pupa kati ya mambo yenye tunapaswa kuepuka kabisa.—Waefeso 5:3.

Michezo ya feza inafanya watu wakuwe na upendo wa feza kwa sababu inawachochea kupata utajiri kwa vyepesi. Biblia inasema kuwa upendo huo wa feza ni “chanzo cha mambo mabaya ya namna zote.” Tamaa ya feza inaweza kwa vyepesi kumutawala mutu sana katika maisha yake; hilo linaweza kumuletea mahangaiko mengi na kuharibu imani yake kwa Mungu. Kwa njia ya mufano, Biblia inasema kuwa wale wenye wamenaswa na upendo wa feza “wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.”—1 Timotheo 6:10.

Pupa inafanya mutu asitosheke na feza zenye anapata na hilo linamufanya apoteze furaha yake. ‘Anayependa feza hatatosheka na feza, wala anayependa mali hatatosheka na mapato.’—Mhubiri 5:10.

Watu wengi sana wenye wameshawishiwa na michezo ya feza wamekuwa watumwa wa tabia hiyo mbaya. Tatizo hilo limeenea sana; inakadiriwa kuwa kuna mamilioni ya watumwa wa michezo ya feza katika inchi ya Amerika tu.

Mezali moja inasema hivi: ‘Uriti wenye kupatikana kwa pupa mwanzoni, wakati wake ujao hautabarikiwa.’ (Methali 20:21) Wale wenye wamekuwa watumwa wa michezo ya feza wamejiingiza katika madeni ao hata kupoteza mali yao. Na wengi kati yao wamepoteza kazi, marafiki, na hata ndoa zao zimevunjika. Kutumikisha kanuni za Biblia kunaweza kusaidia mutu aepuke matokeo mabaya yenye michezo ya feza inaweza kuleta katika maisha na kumusaidia asipoteze furaha yake.

‘Wale ambao wameazimia kuwa matajiri wanaanguka katika jaribu na mutego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kuzuru, ambazo zinatumbukiza watu katika maangamizi na uharibifu.’1 Timotheo 6:9.