Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MUSAADA KWA FAMILIA | NDOA

Namna ya Kuomba Musamaha

Namna ya Kuomba Musamaha

MAGUMU

Wewe na bibi ao bwana yako munatoka tu kubishana. Unajiambia hivi: ‘Haiko lazima niombe musamaha. Haiko mimi nilianzisha mabishano hayo!’

Unaacha tu, lakini tatizo linaendelea. Unawaza tena juu ya kuomba musamaha, lakini unashindwa kusema maneno mepesi “Unisamehe.”

SABABU GANI JAMBO HILO LINATOKEA?

Kiburi. Charles, * mwanaume mwenye kuoa, anasema hivi: “Wakati fulani ni vigumu kusema ‘Unisamehe’ kwa sababu ya kujiona kuwa wa maana.” Kiburi kinaweza kufanya usikie haya ya kuitika kuwa wewe pia uko na kosa.

Mawazo yako. Unaweza kuwaza kuwa ni lazima uombe musamaha ikiwa tu ni wewe ulileta tatizo. Jill, mwanamuke mumoja mwenye kuolewa, anasema hivi: “Wakati ninajua kama ni mimi nilikosea kabisa, ni vyepesi kusema ‘Unisamehe.’ Lakini ni vigumu kuomba musamaha wakati sisi wote wawili tulisema mambo yenye tunahuzunikia. Ni kusema, sababu gani niombe musamaha ikiwa sisi wawili tuko na kosa?”

Unaweza hata zaidi kuona kama hauna sababu ya kuomba musamaha ikiwa unawaza kama bibi ao bwana yako ndiye alikosea kabisa. Joseph, mwanaume mumoja mwenye kuoa, anasema hivi: “Wakati unaamini kabisa kama haukufanya jambo fulani mbaya, kukosa kuomba musamaha ni njia ya kuonyesha kama hauna kosa.”

Namna ulikomaa. Pengine ulikomalia katika familia kwenye watu hawakuzoea kuomba musamaha. Ikiwa ni vile, pengine haukujifunza kuitika makosa yako. Kwa sababu haukuzoea kuomba musamaha wakati ulikuwa mutoto, ni vigumu kwako kuomba musamaha wa kweli wakati unakuwa mutu muzima.

MAMBO UNAWEZA KUFANYA

Kuomba musamaha kunaweza kuzimisha moto wenye kuletwa na ugomvi

Fikiria bibi ao bwana yako. Kumbuka wakati mutu fulani alikuomba musamaha na namna hilo lilikufanya ujisikie muzuri. Sababu gani usiombe musamaha ili kufanya bibi ao bwana yako ajisikie pia muzuri? Hata kama hauamini kuwa ulifanya kosa, unaweza kuomba musamaha kwa sababu bibi ao bwana yako anajisikia kuwa ameumia ao kwa sababu matendo yako yameleta matokeo mabaya yenye haukukusudia. Kuomba musamaha kunaweza kusaidia bibi ao bwana yako ajisikie muzuri.—Kanuni ya Biblia: Luka 6:31.

Fikiria ndoa yako. Usione kama kuomba musamaha kunaonyesha umeshindwa, lakini uone kama ni ushindi kwa ndoa yenu. Kwa kweli, andiko la Methali 18:19 linasema kama mutu anayebakia mwenye kukwazika ni ‘mugumu kuliko muji wenye nguvu.’ Ni vigumu ao hata haiwezekane kurudisha amani katika hali kama hiyo ya kupenda kujitetea. Lakini wakati unaomba musamaha, unazuia kikwazo kuwa tatizo kubwa. Kwa kufanya hivyo, unatanguliza ndoa yako kuliko kujitanguliza.—Kanuni ya Biblia: Wafilipi 2:3.

Usikawie kuomba musamaha. Kwa kweli, inaweza kuwa vigumu kuomba musamaha ikiwa hauna kosa kabisa. Lakini makosa ya bibi ao bwana yako hayakupatie sababu ya kuonyesha tabia mbaya. Kwa hiyo, usikawie kuomba musamaha kwa kuwaza kama atasahau vile siku ziko zinapita. Kama unaomba musamaha, inaweza kuwa vyepesi kwa bibi ao bwana yako kuomba musamaha pia. Na kama unajizoeza kuomba musamaha, itakuwa vyepesi kwako kufanya hivyo.—Kanuni ya Biblia: Mathayo 5:25.

Onyesha kuwa unaomba musamaha wa kweli. Kutetea tabia yako haiko kuomba musamaha. Na pengine kusema kwa zihaka, “Unisamehe basi kwa sababu jambo hili linafanya ukasirike haraka!” haiko kuomba musamaha wa kweli. Uitike matokeo ya matendo yako na utambue kama bibi ao bwana yako anakwazika hata kama unaamini kuwa ana sababu ya kukwazika ao hapana.

Uitike kama unaweza kukosea. Uitike kwa unyenyekevu kama utakosea. Kwa kweli, kila mutu anafanya makosa! Hata kama unawaza kuwa hauna kosa kabisa katika hali fulani, utambue kama pengine haujue mambo yote juu ya hali yenye ilitokea. Biblia inasema hivi: ‘Mutu wa kwanza katika kesi yake ni muadilifu; mwenzake anaingia naye hakika anamuchunguza kwa undani.’ (Methali 18:17) Utakuwa tayari kuomba musamaha kama uko na mawazo ya muzuri juu yako mwenyewe na juu ya makosa yako.

^ fu. 7 Majina fulani yamebadilishwa katika habari hii.