Hamia kwenye habari

Je, Mashahidi wa Yehova Wana Sheria Kuhusu Urafiki wa Kimapenzi?

Je, Mashahidi wa Yehova Wana Sheria Kuhusu Urafiki wa Kimapenzi?

 Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba kanuni na amri zinazopatikana katika Biblia zinatusaidia kufanya maamuzi yanayompendeza Mungu na zinatunufaisha. (Isaya 48:17, 18) Ingawa hatukubuni sheria hizo tunaishi kulingana nazo. Ona jinsi baadhi ya kanuni hizo zinavyotumika wakati wa urafiki wa kimapenzi. *

  •   Ndoa ni muungano wa kudumu. (Mathayo 19:6) Mashahidi wa Yehova wanaona urafiki wa kimapenzi kuwa jambo zito kwa sababu ni moja ya hatua zinazoongoza kwenye ndoa.

  •   Urafiki wa kimapenzi ni kwa ajili ya wale tu walio na umri unaotosha kufunga ndoa. Wao ‘wamepita upeo wa ujana,’ au wakati ambapo tamaa ya ngono ni yenye nguvu zaidi.​—1 Wakorintho 7:​36.

  •   Wanaoanzisha urafiki wa kimapenzi wanapaswa kuwa huru kufunga ndoa. Ingawa watu fulani wametalikiana kisheria, machoni pa Mungu hawako huru kufunga ndoa kwa sababu msingi pekee wa kutalikiana ambao Mungu anaruhusu ni uasherati.​—Mathayo 19:9.

  •   Wakristo wanaotaka kufunga ndoa wanaamriwa kuchagua mwenzi ambaye ni mwamini mwenzao. (1 Wakorintho 7:​39) Mashahidi wa Yehova wanaelewa kwamba amri hii hairejelei mtu anayependezwa tu na yale tunayoamini bali anapaswa kuwa amebatizwa na anatenda kulingana na imani yetu. (2 Wakorintho 6:​14) Tangu zamani Mungu amewaagiza waabudu wake wafunge ndoa na waamini wenzao tu. (Mwanzo 24:3; Malaki 2:​11) Watafiti wamegundua kwamba amri hiyo ina faida. *

  •   Watoto wanapaswa kutii wazazi wao. (Methali 1:8; Wakolosai 3:​20) Kwa watoto walio nyumbani, amri hiyo inatia ndani kutii maamuzi ya wazazi wao kuhusu urafiki wa kimapenzi. Huenda maamuzi hayo yakahusu umri ambao mwana au binti anaweza kuanzisha urafiki na mambo anayoruhusiwa kufanya.

  •   Maadamu anafuata miongozo ya Kimaandiko, kila Shahidi anaweza kujiamulia ikiwa ataanzisha urafiki wa kimapenzi na atauanzisha na nani. Hilo linapatana na kanuni hii: “Kila mmoja ataubeba mzigo wake mwenyewe.” (Wagalatia 6:5) Hata hivyo, inapohusu urafiki wa kimapenzi, kwa hekima wengi hutafuta ushauri wa Shahidi mkomavu anayewatakia mema.​—Methali 1:5.

  •   Mambo mengi ambayo hufanywa na wale walio katika urafiki wa kimapenzi ni dhambi nzito. Kwa mfano, Biblia inatuamuru tuepuke uasherati. Uasherati unatia ndani matendo machafu kati ya watu ambao si wenzi wa ndoa, kama vile kupapasana sehemu za siri au kufanya ngono ya mdomo au ngono ya mkundu. (1 Wakorintho 6:​9-​11) Hata vitendo vinavyoamsha hamu ya ngono hadi kufika karibu sana kufanya ngono ni “uchafu” usiompendeza Mungu. (Wagalatia 5:​19-​21) Pia, mazungumzo yasiyofaa yenye “maneno machafu” yanashutumiwa katika Biblia.​—Wakolosai 3:8.

  •   Moyo (yule mtu wa ndani) ni wenye hila. (Yeremia 17:9) Unaweza kumwongoza mtu kufanya mambo anayojua ni makosa. Ili mioyo yao isiwapotoshe, watu walio na urafiki wa kimapenzi huepuka kuwa peke yao katika hali zenye kushawishi. Wanaweza kuamua kujiunga na kikundi cha marafiki au kuchagua mtu wa kuandamana nao. (Methali 28:26) Wakristo waseja wanaotafuta mwenzi wa ndoa wanatambua hatari ya kutafuta marafiki wa kimapenzi kupitia vituo vya Intaneti, na hasa hatari ya kuanzisha uhusiano na watu wasiowafahamu vizuri.​—Zaburi 26:4.

^ Katika tamaduni fulani ni jambo la kawaida kuanzisha urafiki wa kimapenzi, lakini si tamaduni zote. Biblia haisemi kuwa tunahitaji kuwa na urafiki huo au kwamba ndiyo njia pekee inayoongoza kwenye ndoa.

^ Kwa mfano, makala katika jarida la Marriage & Family Review ilisema kwamba “utafiti uliofanywa kuchunguza ni mambo gani yanayochangia zaidi kufanya ndoa zidumu kwa miaka mingi ulionyesha kwamba wenzi hao walikuwa na mtazamo, imani, na mafundisho ya kidini yanayofanana, na hivyo ndoa zao zilidumu kwa muda mrefu (miaka 25-​50 na zaidi).”​—Toleo la 38, nakala ya 1, ukurasa wa 88 (2005).