Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Bado Ukweli Ni Muhimu?

Je, Bado Ukweli Ni Muhimu?

 Je, unahisi kwamba siku hizi si rahisi kutambua kati ya ukweli na uwongo? Ni kana kwamba siku hizi watu wanafanya maamuzi wakiongozwa na hisia na maoni ya kibinafsi na si kwa kutegemea ukweli au mambo ya hakika. Ulimwenguni pote leo, watu wengi hawaamini ukweli unaweza kupatikana popote.

 Mtazamo huo ulikuwepo tangu zamani. Miaka 2,000 hivi iliyopita, Gavana Mroma Pontio Pilato alimwuliza Yesu hivi kwa kejeli: “Kweli ni nini?” (Yohana 18:38) Ingawa Pilato hakusubiri Yesu ajibu, swali lake lilikuwa muhimu. Biblia inatusaidia tupate jibu lenye kuridhisha, na inaweza kutupatia mwongozo katika ulimwengu huu ambao watu wanashindwa kutofautisha kati ya ukweli na uwongo.

Je, ukweli unaweza kupatikana leo?

 Ndiyo. Biblia inatumia neno “kweli” inaporejelea mambo ya hakika na pia kuhusu mambo ambayo ni sahihi na yanayofaa. Inafundisha kwamba Yehova a Mungu ndiye Chanzo cha ukweli kamili, hata inasema kwamba yeye ni “Mungu wa ukweli.” (Zaburi 31:5) Biblia ina kweli kutoka kwa Mungu, na inalinganisha kweli hiyo na mwangaza, kwa sababu kweli inaweza kutuongoza katika ulimwengu huu ambao hauna mwelekeo.​—Zaburi 43:3; Yohana 17:17.

Unaweza kupataje kweli?

 Mungu hataki tukubali kweli iliyo katika Biblia bila kuichunguza. Badala yake, anatualika tuichanganue kwa kutumia nguvu zetu za kufikiri na si kwa kutegemea hisia zetu. (Waroma 12:1) Anataka tumjue na kumpenda ‘kwa akili yetu yote,’ naye anatutia moyo tujihakikishie ikiwa mambo tunayojifunza katika Biblia ni ya kweli.​—Mathayo 22:37, 38; Matendo 17:11.

Uwongo ulianzia wapi?

 Biblia inasema kwamba uwongo ulianzishwa na adui ya Mungu, Shetani Ibilisi, ambaye Biblia inamwita “baba ya uwongo.” (Yohana 8:44) Aliwaambia wanadamu wa kwanza uwongo kumhusu Mungu. (Mwanzo 3:1-6, 13, 17-19; 5:5) Tangu wakati huo, Shetani ameendelea kueneza uwongo na kuficha ukweli kumhusu Mungu.​—Ufunuo 12:9.

Kwa nini uwongo ni jambo la kawaida leo?

 Biblia inaziita siku zetu kuwa “siku za mwisho.” Leo, Shetani anazidi kuwapotosha watu. Ni jambo la kawaida kwa watu kuwaambia wengine uwongo ili kuwalaghai. (2 Timotheo 3:1, 13) Pia, uwongo unatawala katika dini nyingi leo. Kama Biblia ilivyotabiri kuhusu siku zetu, watu ‘wanajikusanyia walimu ili masikio yao yafurahishwe,’ wakichagua ‘kuacha kuisikiliza ile kweli.’​—2 Timotheo 4:3, 4.

Kwa nini kweli ni muhimu?

 Ukweli ndio msingi wa kuwafanya watu waaminiane. Watu wanapokosa kuaminiana, urafiki na jamii kwa ujumla hudhoofika. Biblia inasema kwamba Mungu anataka ibada yetu itegemee kweli. Inasema hivi: “Wale wanaomwabudu [Mungu] lazima wamwabudu kwa roho na kweli.” (Yohana 4:24) Ili ujifunze jinsi kweli kutoka katika Biblia inavyoweza kukusaidia kutambua uwongo wa kidini na kujiepusha nao, soma mfululizo wa makala “Uwongo Unaofanya Watu Wasimpende Mungu.”

Kwa nini Mungu anataka mimi nijue kweli?

 Mungu anataka upate wokovu, na unahitaji kujifunza ukweli kumhusu yeye ili ustahili kuokolewa. (1 Timotheo 2:4) Ukijifunza viwango vya Mungu kuhusu mema na mabaya na kuishi kupatana navyo, utakuwa na urafiki wa karibu pamoja naye. (Zaburi 15:1, 2) Mungu alimtuma Yesu duniani ili kuwasaidia watu wajifunze kweli. Mungu anataka tusikilize mafundisho ya Yesu.​—Mathayo 17:5; Yohana 18:37.

Je, Mungu atakomesha uwongo?

 Ndiyo. Mungu anachukia watu wanapowalaghai wengine kwa kuwadanganya. Ameahidi kwamba atawaangamiza wale walioazimia kuendelea kusema uwongo. (Zaburi 5:6) Mungu atakapofanya hivyo, atatimiza ahadi yake inayosema hivi: “Midomo inayosema ukweli itadumu milele.”​—Methali 12:19.

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala “Yehova Ni Nani?