Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

BIBLIA INABADILI MAISHA

Maisha Yangu Yalizidi Kuwa Mabaya

Maisha Yangu Yalizidi Kuwa Mabaya
  • ALIZALIWA: 1952

  • NCHI: MAREKANI

  • HISTORIA: MWENYE HASIRA KALI

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nililelewa katika jiji la Los Angeles, California, nchini Marekani, katika maeneo yaliyokuwa maarufu kwa kuwa na magenge ya wahalifu na madawa ya kulevya. Nilikuwa mtoto wa pili kuzaliwa kati ya watoto sita.

Mama yetu alikuwa mshiriki wa kanisa la kiinjilisti, nasi tukawa washiriki wa dini hiyo. Hata hivyo, nilipokuwa tineja, nilianza kuishi maisha ya unafiki. Jumapili niliimba kwaya kanisani. Na siku nyingine za juma, nilishiriki katika karamu, nilitumia dawa za kulevya, na kufanya uasherati.

Nilikuwa mwenye hasira kali. Nilitumia chochote kama silaha ili kupigana. Mambo niliyojifunza kanisani hayakunisaidia. Nilikuwa nikisema hivi: “Kisasi ni cha Bwana, naye ananitumia mimi kulipiza!” Nilipokuwa katika shule ya sekondari mwishoni mwa miaka ya 1960, nilivutiwa na kikundi cha Black Panthers, kikundi cha kisiasa kilichojulikana kwa sababu ya kutumia wanamgambo ili kutetea haki za raia. Nilijiunga na kikundi cha wanafunzi cha kutetea haki za raia. Tulifanya maandamano mara kadhaa, na kila mara shule ilifungwa kwa muda.

Ilionekana kwamba maandamano hayakutosheleza tabia yangu ya kuwa mwenye hasira kali. Hivyo nilianza kushirikiana na kikundi kilichofanya uhalifu unaochochewa na chuki. Kwa mfano, pindi moja mimi na rafiki zangu tulitazama filamu iliyoonyesha jinsi watumwa wa Kiafrika walivyoteswa nchini Marekani. Tukiwa tumekasirika kutokana na ukosefu huo wa haki, tuliwashambulia vijana wazungu waliokuwa katika jumba hilo la sinema. Kisha, tulienda katika maeneo ambayo wazungu waliishi ili kutafuta watu zaidi wa kuwapiga.

Nilipokuwa nakaribia umri wa miaka 20, mimi na kaka zangu tulikuwa tukifanya uhalifu mwingi wenye jeuri. Tulikamatwa mara nyingi na wenye mamlaka. Ndugu yangu mdogo na mimi tulikuwa washiriki wa genge hatari la uhalifu. Maisha yangu yalizidi kuwa mabaya.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Rafiki yangu alikuwa na wazazi ambao ni mashahidi wa Yehova. Nilikubali mwaliko wao wa kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Kuanzia hapo niliona tofauti iliyopo kati ya Mashahidi na dini nyingine. Kila mmoja alikuwa na Biblia aliyoitumia wakati wa mkutano. Vijana walitoa hotuba katika programu hiyo. Nilivutiwa sana nilipojifunza kwamba Mungu anaitwa Yehova, na niliposikia jina hilo likitumiwa. (Zaburi 83:18) Kutaniko lilikuwa na watu kutoka mataifa mbalimbali, lakini niliona kwamba hakukuwa na ubaguzi.

Mwanzoni, sikutaka kujifunza Biblia na Mashahidi, lakini nilipenda tu kuhudhuria mikutano yao. Usiku mmoja, nilipokuwa kwenye mkutano wa Mashahidi, marafiki zangu walienda katika tamasha fulani. Walipokuwa huko, walimpiga na kumuua kijana mmoja kwa kuwa alikataa kuwapa koti lake la ngozi. Siku iliyofuata, walijigamba kwa kufanya mauaji hayo. Hata walifikiri kwamba uhalifu wao wa jeuri haukuwa jambo zito walipokuwa mahakamani. Wengi wao walihukumiwa kifungo cha maisha gerezani. Kwa kweli, nilishukuru sana kwamba sikuwa pamoja nao usiku huo. Niliazimia kubadili maisha yangu na kuanza kujifunza Biblia.

Kwa sababu nililelewa katika eneo lililokuwa na ubaguzi wa kijamii, nilishangazwa na jinsi Mashahidi walivyojiendesha. Kwa mfano, Shahidi mzungu alipotaka kwenda nchi nyingine, angewaacha watoto wake watunzwe na familia ya watu weusi. Pia, familia moja ya wazungu ilikubali kuishi na kijana mweusi aliyekosa makao. Nilikuja kuamini kwamba Mashahidi wa Yehova wanatimiza maneno ya Yesu yaliyo kwenye Yohana 13:35, yanayosema hivi: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” Nilitambua kwamba nilikuwa nimepata undugu wa kweli.

Kujifunza Biblia kulinisaidia kuanza kutambua kwamba ninahitaji kubadili mtazamo wangu. Nilihitaji kutambua kwamba ninapaswa kutenda kwa njia ya amani na pia kuona kwamba hiyo ndiyo njia bora ya maisha. (Waroma 12:2) Hatua kwa hatua, nilifanya maendeleo. Mnamo Januari 1974, nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova.

Nilihitaji kutambua kwamba ninapaswa kutenda kwa njia ya amani na pia kuona kwamba hiyo ndiyo njia bora ya maisha

Hata baada ya kubatizwa, bado nilihitaji kuendelea kudhibiti hasira yangu. Kwa mfano, wakati fulani nilipokuwa naenda nyumba kwa nyumba kwa ajili ya huduma ya Kikristo, nilimfukuza mwizi ambaye alikuwa ameiba redio ya gari langu. Nilipomkaribia, aliangusha redio na kukimbia. Nilipowaeleza wengine jinsi nilivyoipata redio yangu, mzee katika kikundi hicho aliniuliza hivi: “Stephen, ungefanya nini ikiwa ungemkamata mwizi huyo?” Swali hilo lilinifanya nitafakari na kunichochea kufanyia kazi sifa ya kuwa mwenye kufanya amani.

Katika mwezi wa Oktoba, 1974, nilianza kutumika nikiwa mhudumu wa wakati wote, nikitumia saa 100 kila mwezi kuwafundisha watu Biblia. Baadaye nilipata pendeleo la kujitolea katika makao makuu ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova, Brooklyn, New York. Mwaka 1978, nilirudi Los Angeles ili kumtunza mama yangu aliyekuwa mgonjwa. Miaka miwili baadaye, nilimwoa mke wangu mpendwa, Aarhonda. Mke wangu alinisaidia sana kumtunza mama yangu mpaka Mama alipokufa. Baadaye, mimi na Aarhonda tulihudhuria Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) na tukatumwa Panama, eneo tunaloendelea kutumika tukiwa wamishonari.

Tangu nilipobatizwa, nimekabili hali nyingi ambazo huenda zingenifanya nitende kwa jeuri. Nimejifunza kushughulikia mambo kwa njia ya amani au kujiepusha na watu ambao hujaribu kunikasirisha. Watu wengi, kutia ndani mke wangu, wamenipongeza kutokana na jinsi ninavyoshughulikia hali hizo. Jambo hilo hunishangaza! Si kwamba nimeweza kufanya mabadiliko hayo kwa uwezo wangu mwenyewe. Badala yake, ninaamini kwamba Biblia ina uwezo wa kugeuza utu wa mtu.—Waebrania 4:12.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Biblia imenifanya niwe na kusudi maishani na kunifundisha kuwa mwenye kufanya amani. Siwapigi watu tena; badala yake, ninawasaidia kupona kiroho. Hata nilimfundisha Biblia mtu aliyekuwa adui yangu shuleni! Alipobatizwa tuliishi naye kwenye chumba kimoja kwa kipindi fulani. Sisi bado ni marafiki. Mpaka sasa, mimi na mke wangu tumewasaidia watu zaidi ya 80 kuwa Mashahidi wa Yehova kwa kuwafundisha Biblia.

Namshukuru sana Yehova kwa kunipa maisha yenye kusudi na pia furaha inayotokana na kuwa na undugu wa kweli.