Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Tunaweza Kumpendeza Mungu?

Je, Kweli Tunaweza Kumpendeza Mungu?

Umewahi kusoma kuhusu watu wanaosifiwa sana katika Biblia na kusema, ‘siwezi kuwa kama wao!’ Huenda ukawaza hivi: ‘Mara zote mimi sifanyi yaliyo sawa, hivyo mimi si mwadilifu au asiye na lawama.’

Ayubu alikuwa “asiye na lawama na mnyoofu.” —Ayubu 1:1,

Mwanamume Ayubu anatajwa kuwa “asiye na lawama na mnyoofu.” (Ayubu 1:1) Loti aliitwa “mtu mwadilifu.” (2 Petro 2:8) Pia, Biblia inasemwa kwamba Daudi alifanya “yaliyokuwa sawa” machoni pa Mungu. (1 Wafalme 14:8) Hata hivyo, acheni tuchunguze zaidi maisha ya watu hao wanaotajwa katika Biblia. Tutaona kwamba (1) walifanya makosa, (2) tunaweza kujifunza mengi kutoka kwao, na (3) wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kumpendeza Mungu.

WALIFANYA MAKOSA

“[Mungu] alimkomboa Loti mwadilifu, aliyetaabishwa sana na kule kujitia mno katika mwenendo mpotovu kwa watu wanaokaidi sheria.”—2 Petro 2:7

Ayubu alikabili hali ngumu nyingi zilizoonekana kuwa si haki. Alifikiri kimakosa kwamba Mungu hamjali hata kama angeendelea kuwa na imani Kwake au la. (Ayubu 9:20-22) Ayubu alikazia fikira zaidi uadilifu wake hivi kwamba wengine waliona ni kana kwamba alikuwa akijitangaza kuwa mwadilifu machoni pake mwenyewe kuliko Mungu.—Ayubu 32: 2; 35:1, 2.

Loti alisita kufanya uamuzi uliokuwa wazi na rahisi. Alitaabishwa sana na upotovu wa maadili uliozidi wa watu walioishi Sodoma na Gomora, hivi kwamba ‘aliitesa nafsi yake yenye uadilifu’ kwa sababu ya tabia zao. (2 Petro 2:8) Mungu alitangaza kwamba angeangamiza majiji hayo maovu na kumpa Loti na familia yake nafasi ya kuokolewa. Huenda ungewazia kwamba Loti aliyekuwa akitaabishwa na uovu angekuwa wa kwanza kuondoka. Hata katika wakati huo muhimu, alisita. Malaika waliotumwa kumwokoa yeye na familia yake walihitaji kuwashika mikono na kuwatoa nje ya jiji ili kuwapeleka eneo salama.—Mwanzo 19:15, 16.

Daudi ‘alimfuata [Mungu] kwa moyo wake wote kwa kufanya yaliyokuwa sawa tu machoni pa [Mungu].’—1 Wafalme 14:8

Pindi moja Daudi alikosa kuonyesha sifa ya kujizuia na hivyo akafanya uzinzi na mke wa mtu mwingine. Kwa kushangaza, Daudi alijaribu kuficha jambo hilo kwa kufanya mpango wa kumuua mume wa mwanamke huyo. (2 Samweli, sura ya 11) Biblia inasema kwamba lile jambo ambalo Daudi alifanya ‘lilikuwa baya machoni pa Yehova.’—2 Samweli 11:27.

Ayubu, Loti, na Daudi walifanya makosa, na baadhi ya makosa yao yalikuwa mzito sana. Lakini, kama tutakavyoona, waliazimia kumtumikia Mungu kwa utiifu. Walikuwa tayari kuomba msamaha na kutubu makosa yao. Hivyo, Mungu akawaonyesha kibali, na kwa ujumla Biblia inawataja kuwa wanaume waaminifu.

TUNAWEZA KUJIFUNZA NINI?

Tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, hatuwezi kuepuka kufanya makosa. (Waroma 3:23) Lakini tunapokosea, tunahitaji kuomba msamaha na kisha kufanya yote tunayoweza ili kurekebisha mambo.

Ayubu, Loti, na Daudi walirekebisha jinsi gani makosa yao? Ayubu alikuwa mtu mtimilifu moyoni. Baada ya Mungu kuzungumza naye, Ayubu alirekebisha mtazamo wake usiofaa na kuomba msamaha kwa yale aliyosema. (Ayubu 42:6) Mtazamo wa Loti kuhusu upotovu wa maadili wa watu wa Sodoma na Gomora ulipatana kabisa na viwango vya Mungu. Tatizo lake lilikuwa ni kukosa kuchukua hatua kwa uharaka. Hatimaye aliondoka katika miji uliyohukumiwa na hivyo aliepuka hukumu ya Mungu. Kwa utii, Loti hakutazama nyuma mambo aliyoacha. Ingawa Daudi alifanya kosa zito kwa kuvunja sheria ya Mungu, alionyesha yaliyokuwa moyoni mwake kwa kutubu kikweli na kumsihi Mungu amwonyeshe rehema.—Zaburi 51.

Mtazamo unaofaa wa Mungu kuelekea watu hao unapatana na maoni yake yenye usawaziko kuhusu anachotarajia kutoka kwa wanadamu wasio wakamilifu. Mungu “analijua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.” (Zaburi 103:14) Hivyo, ikiwa Mungu anajua kwamba hatuwezi kuepuka kufanya makosa, anataka tufanye nini?

Mungu “analijua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.”Zaburi 103:14

WANADAMU WASIO WAKAMILIFU WANAWEZA KUMPENDEZA MUNGU JINSI GANI?

Shauri la Daudi kwa mwana wake Sulemani linatusaidia kujua jinsi tunavyoweza kumpendeza Mungu. Alimwambia hivi: “Nawe, Sulemani mwanangu, mjue Mungu wa baba yako, umtumikie kwa moyo kamili.” (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Moyo kamili ni nini? Ni moyo unaompenda Mungu na uko tayari kujua na kufanya mapenzi yake. Si kwamba moyo huo ni mkamilifu, bali unataka kumtumikia Mungu kwa utiifu na uko tayari kurekebishwa. Kwa sababu ya upendo wao kwa Mungu na kuwa tayari kumtii, Ayubu anatajwa kuwa “asiye na lawama,” Loti anatajwa kuwa “mtu mwadilifu,” na Daudi kuwa mtu ‘aliyefanya yaliyokuwa sawa tu’ machoni pa Mungu. Ingawa walifanya makosa, waliweza kumpendeza Mungu.

Moyo kamili uko tayari kujua na kufanya mapenzi ya Mungu na unachochewa na tamaa ya kumtumikia kwa utiifu

Hivyo, ikiwa mawazo yasiyofaa yanaingia akilini mwetu, tunasema jambo ambalo baadaye tunaaibikia, au tunafanya mambo ambayo baadaye tunatambua kwamba ni makosa, tunaweza kufarijika kwa kuchunguza mifano tuliyozungumzia. Mungu anajua kwa sasa hatuwezi kuwa wakamilifu. Hata hivyo, anatarajia tumpende na kujitahidi kumtii. Ikiwa tutafanya hivyo tukiwa na moyo kamili, tunaweza kuwa na uhakika kwamba sisi pia tunaweza kumpendeza Mungu.