Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

BIBLIA INABADILI MAISHA

Nilijifunza Kwamba Yehova Ni Mwenye Rehema na Mwenye Kusamehe

Nilijifunza Kwamba Yehova Ni Mwenye Rehema na Mwenye Kusamehe
  • ALIZALIWA: 1954

  • NCHI: KANADA

  • HISTORIA: MLAGHAI, MCHEZA-KAMARI

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nililelewa katika eneo la bonde katika mji wa Montreal.

Baba yangu alikufa nilipokuwa na umri wa miezi sita, hivyo mama yangu alihitaji kuitunza familia. Nilikuwa mtoto wa mwisho katika familia yenye watoto nane.

Nililelewa katika mazingira yenye watu waliotumia dawa za kulevya, waliocheza kamari, wajeuri, na wahalifu. Nilipokuwa na umri wa miaka kumi, nilianza kutumwa na makahaba na wakopeshaji wa mikopo isiyo halali. Nilidanganya mara nyingi na nilifurahia kulaghai watu. Kufanya hivyo kulikuwa kwangu kama kutumia dawa ya kulevya.

Nilipokuwa na umri wa miaka 14, nilikuwa na uwezo mkubwa wa kudanganya watu. Kwa mfano, ningenunua saa, vikuku, na pete zilizofunikwa kwa dhahabu, na kupiga mhuri usio halali unaoonyesha karati 14 za dhahabu, na kisha kuuza vitu hivyo barabarani na katika maegesho ya magari. Nilifurahia sana kupata pesa kwa njia rahisi. Pindi moja, nilipata dola 10,000 kwa siku!

Nilipokuwa na umri wa miaka 15, nilifukuzwa kutoka katika shule ya kurekebisha tabia, nami sikuwa na mahali pa kuishi. Nililala mitaani, katika bustani za kupumzika au kwa rafiki zangu.

Kwa sababu ya kuwa mlaghai, nilihojiwa mara kwa mara na polisi. Kwa kuwa mali nilizouza hazikuwa za wizi, sikuwahi kufungwa gerezani. Hata hivyo, nililipa faini mara kadhaa kwa sababu ya ulaghai, kughushi na kufanya biashara bila kibali. Pia, nilikusanya pesa bila hofu kwa niaba ya wakopeshaji wa mikopo isiyo halali. Hilo lilikuwa jambo hatari sana, na mara kadhaa nilibeba bunduki. Katika pindi fulani, nilishirikiana na magenge ya wahalifu.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Nilianza kusikia ujumbe wa Biblia nilipokuwa na umri wa miaka 17. Nilikuwa nikiishi na rafiki yangu wa kike alipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, kwa kuwa nilipinga viwango vya maadili vya Biblia, nilimwacha na kuanza kuishi na msichana mwingine niliyetarajia kumuoa.

Mambo yalibadilika wakati rafiki yangu wa kike wa pili alipoanza pia kujifunza na Mashahidi! Alifanya mabadiliko katika maisha yake, na nilipendezwa kwamba alianza kuwa mpole na mwenye subira zaidi. Nilikubali mwaliko wa kuhudhuria mkutano katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Nilikaribishwa na watu wenye heshima na fadhili. Hilo lilikuwa jambo jipya maishani mwangu! Sikuwahi kuhisi kwamba ninathaminiwa na familia yetu; nilipokuwa mtoto sikutendewa kwa fadhili na wororo. Uchangamfu nilioonyeshwa na Mashahidi wa Yehova ndio niliohitaji hasa. Nilikubali mara moja Mashahidi walipojitolea kunifundisha Biblia.

Ninahisi kwamba kila jambo nililojifunza katika Biblia liliokoa uhai wangu. Mimi na wenzangu wawili tulipanga kuiba pesa ili niweze kulipa deni la zaidi ya dola 50,000 lililotokana na kucheza kamari. Hata hivyo, ninafurahi sana kwamba nilijiondoa katika mpango huo! Wenzangu walienda kuiba. Mmoja wao alikamatwa na mwingine aliuawa.

Nilipokuwa nikiendelea kujifunza Biblia, nilitambua kwamba nilihitaji kufanya mabadiliko mengi. Kwa mfano, nilijifunza kile ambacho Biblia inasema katika 1 Wakorintho 6:10: “Wala wezi, wala watu wenye pupa, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi hawataurithi ufalme wa Mungu.” Niliposoma mstari huo, hali yangu ilinihuzunisha sana hivi kwamba nikatokwa na machozi. Nilitambua kwamba nilihitaji kubadili kabisa maisha yangu. (Waroma 12:2) Nilikuwa mjeuri, mkali, na nilizoea kusema uwongo maishani.

Hata hivyo, nilijifunza pia katika Biblia kwamba Yehova ni mwenye rehema na mwenye kusamehe. (Isaya 1:18) Nilimsihi Yehova kupitia sala kwamba anisaidie kufanya mabadiliko maishani. Kwa msaada wake, pole kwa pole niliweza kubadili utu wangu. Mimi na rafiki yangu wa kike tulifanya uamuzi muhimu wa kuhalalisha ndoa yetu.

Niko hai leo kwa sababu ninafuata kanuni za Biblia

Nilikuwa na mke na watoto watatu nilipokuwa na umri wa miaka 24. Hivyo, nilihitaji kutafuta kazi halali. Hata hivyo, sikuwa na elimu ya kutosha wala wadhamini. Kwa mara nyingine tena, nilimsihi Yehova katika sala. Kisha, nikaenda kutafuta kazi. Niliwaambia wale walionihoji ili kuniajiri kwamba nilitaka kubadili maisha yangu na kufanya kazi iliyo halali. Nyakati nyingine, niliwaeleza kwamba nilikuwa najifunza Biblia na kwamba nilitaka kuwa raia mwema. Hata hivyo, wengi wao walikataa kuniajiri. Hatimaye, baada ya kumweleza wazi mwenendo wangu wa zamani mwajiri mmoja aliyenihoji, aliniambia hivi: “Sijui ni nini, lakini ninahisi kwamba ninapaswa kukuajiri.” Ninaamini kwamba hilo lilikuwa jibu la sala zangu. Baada ya muda, mimi na mke wangu tulibatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Niko hai leo kwa sababu ninafuata kanuni za Biblia na kuishi maisha ya Kikristo. Nina familia yenye furaha. Ninafurahi kuwa na dhamiri safi kwa sababu nina hakika kwamba Yehova amenisamehe.

Kwa miaka 14 sasa nimetumika nikiwa mtumishi wa wakati wote, nikiwasaidia wengine kujifunza yale ambayo Biblia inafundisha, na hivi karibuni mke wangu ameniunga mkono katika utumishi wa wakati wote. Kwa zaidi ya miaka 30 nimepata shangwe inayotokana na kuwasaidia wafanyakazi wenzangu 22 waanze kumwabudu Yehova. Bado ninaenda madukani, lakini si kwa lengo la kuwalaghai watu kama nilivyokuwa nikifanya zamani. Kila mara ninapoenda huko, mimi huwaeleza wengine kuhusu imani yangu. Ninataka kuwapa kitu fulani: tumaini la kuishi katika ulimwengu mpya ujao ambao walaghai hawatakuwapo tena.—Zaburi 37:10, 11.