Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

IGENI IMANI YAO | YOSEFU

“Je, Mimi Niko Mahali pa Mungu?”

“Je, Mimi Niko Mahali pa Mungu?”

YOSEFU amesimama katika bustani yake jua linapoanza kuzama. Huenda anatazama mitende na miti mingine yenye matunda, madimbwi yenye mimea, na mbele kidogo jumba la kifalme la Farao. Wazia Yosefu akisikia sauti kwa mbali kutoka nyumbani kwake; mwana wake, Manase akimchekesha ndugu yake mdogo, Efraimu. Yosefu huenda aliwazia mke wake akitabasamu anapowaona watoto wake wakicheza pamoja. Hilo lilimfanya atabasamu pia. Alikumbuka kwamba amebarikiwa sana.

Yosefu alimwita mwana wake mzaliwa kwanza Manase, jina linalomaanisha kusahau. (Mwanzo 41:51) Kwa kweli, baraka alizopewa na Mungu katika miaka ya karibuni zilipunguza maumivu yake alipokumbuka nyumbani kwao, ndugu zake, na baba yake. Chuki ya ndugu zake wakubwa ilibadili maisha yake. Walimpiga, wakapanga kumuua, na kisha wakamuuza akiwa mtumwa kwa wafanyabiashara wanaosafiri. Tangu wakati huo, maisha yake yamekuwa na misukosuko mingi. Kwa miaka mingi, alikuwa mtumwa na kisha akafungwa gerezani—akifungwa kwa pingu za chuma kwa kipindi fulani cha wakati. Lakini sasa, yeye ni mtawala wa pili baada ya Farao, katika taifa lenye nguvu la Misri! *

Kwa miaka kadhaa, Yosefu ameona mambo yakitendeka kama Yehova alivyotabiri. Misri ilikuwa katika kipindi kilichotabiriwa cha miaka saba yenye mavuno mengi, na Yosefu alisimamia kuwekwa akiba kwa nafaka ya taifa hilo. Wakati huo, alikuwa na mke aliyeitwa Asenathi na wana wawili. Hata hivyo, mara kwa mara alikumbuka familia yake aliyoiacha maelfu ya kilomita, hasa ndugu yake mdogo, Benyamini, na baba yao mpendwa, Yakobo. Huenda Yosefu aliwaza ikiwa wako salama na wanaendelea vizuri. Huenda aliwaza pia ikiwa ndugu zake wakubwa walibadili mtazamo wao wenye jeuri au ikiwa siku moja ataweza kufanya amani na familia yake na kuwa pamoja nao.

Huenda hali zako zinafanana na za Yosefu ikiwa familia yenu haina amani kwa sababu ya wivu, usaliti, au chuki. Tunaweza kujifunza nini kutokana na imani ya Yosefu alipokuwa akiitunza familia yake?

“NENDENI KWA YOSEFU”

Yosefu alikuwa na shughuli nyingi, na miaka ilipita haraka. Mwaka wa saba wenye mazao mengi ulifuatiwa na mabadiliko makubwa kama tu Yehova alivyotabiri katika ndoto ya Farao. Hawakupata mazao! Baada ya muda mfupi njaa iliathiri nchi zote za jirani. Hata hivyo, Biblia inasema “mkate ulipatikana katika nchi yote ya Misri.” (Mwanzo 41:54) Ni wazi kwamba utabiri aliotoa Yosefu kwa mwongozo wa roho ya Mungu na mfano wake mzuri katika kupanga mambo kwa utaratibu uliwanufaisha Wamisri.

Kwa kuwa aliendelea kuwa mnyenyekevu, Yosefu alitumiwa na Yehova

Huenda Wamisri walimsifu na kumthamini sana Yosefu kwa sababu ya ustadi wake wa kupanga mambo. Hata hivyo, Yosefu alimpa sifa hizo Mungu wake, Yehova. Tukitumia vipawa tulivyo navyo kumtumikia Mungu wetu, huenda akatuwezesha kuvitumia kwa njia bora zaidi.

Hata hivyo, baada ya muda njaa iliongezeka Misri. Farao aliwaambia hivi Wamisri walipomwomba msaada: “Nendeni kwa Yosefu. Lolote atakalowaambia, fanyeni.” Basi, Yosefu akaanza kufungua maghala yote ya nafaka yaliyokuwa kati yao, na watu wakaweza kununua walichohitaji.—Mwanzo 41:55, 56.

Hali zilikuwa ngumu katika nchi za jirani. Familia ya Yosefu ilikuwa ikiteseka katika nchi ya Kanaani. Yakobo aliyezeeka aliposikia kwamba nafaka ilipatikana Misri, aliwaambia wana wake waende huko kununua chakula.—Mwanzo 42:1, 2.

Yakobo alituma watoto wake kumi na kubaki na mwana wake mdogo, Benyamini. Yakobo alikumbuka vizuri kilichotokea mara ya mwisho alipomtuma mwana wake mpendwa Yosefu peke yake ili awatembelee ndugu zake wakubwa. Hiyo ilikuwa mara ya mwisho kwa Yakobo kumwona mtoto wake. Watoto wake wakubwa walileta vazi maridadi—alilopewa Yosefu na baba yake kama wonyesho wa upendo na heshima—limechanika na likiwa na damu. Walimfanya mzee huyo aliyevunjika moyo aamini kwamba Yosefu alikuwa ameliwa na wanyama mwitu.—Mwanzo 37:31-35.

“YOSEFU AKAWATAMBUA MARA MOJA”

Baada ya safari ya ndefu, hatimaye wana wa Yakobo walifika Misri. Walipouliza kuhusu kununua nafaka, waliagizwa kwenda kwa ofisa mkubwa wa serikali aliyeitwa Zafenath-panea. (Mwanzo 41:45) Je, walipomwona walimtambua Yosefu? Hapana. Walimwona tu kuwa mtawala wa Misri mwenye cheo kikubwa waliyehitaji msaada wake. Ili kumwonyesha heshima mtawala huyo: ‘Walimwinamia kifudifudi.’—Mwanzo 42:5, 6.

Namna gani Yosefu? Aliwatambua ndugu zake mara moja! Zaidi ya hayo, alipowaona wakimwinamia, alikumbuka alipokuwa mvulana. Simulizi linatuambia kwamba “papo hapo Yosefu akakumbuka ndoto” alizoota alipokuwa mvulana, kwa msaada wa Yehova. Ndoto hizo zilitabiri kuhusu wakati ambapo ndugu zake wangemwinamia, kama tu walivyokuwa wakifanya pindi hiyo! (Mwanzo 37:2, 5-9; 42:7, 9) Yosefu angefanya nini? Je, angewakumbatia? Angelipiza kisasi?

Yosefu alijua kwamba hata hali iweje, hakupaswa kutenda kulingana na hisia zake. Ni wazi kwamba Yehova ndiye aliyekuwa anaongoza mambo hayo. Alitaka kutimiza kusudi lake. Aliahidi kwamba uzao wa Yakobo ungekuwa taifa lenye nguvu. (Mwanzo 35:11, 12) Ndugu za Yosefu wangepatwa na msiba mkubwa kama nini ikiwa bado wangekuwa wajeuri, wabinafsi, na wasiotenda haki! Isitoshe, ikiwa Yosefu angetenda kwa kufuata hisia zake, huenda angevuruga amani ya kiasi fulani iliyokuwepo na hata angehatarisha uhai wa baba yake na Benyamini. Alikuwa hajui ikiwa walikuwa hai au la. Hivyo, Yosefu aliamua kutojitambulisha ili awajaribu ndugu zake na kuona ikiwa wamebadili mtazamo wao. Huenda kufanya hivyo kungemsaidia kujua kile ambacho Yehova alitaka afanye.

Huenda usikabili hali hiyo isiyo ya kawaida. Hata hivyo, migogoro na migawanyiko ndani ya familia ni jambo la kawaida katika ulimwengu wa leo. Tunapokabili changamoto hizo, huenda tukaanza kufuata moyo wetu na kutenda kulingana na hisia zetu zenye dhambi. Litakuwa jambo la hekima tukimwiga Yosefu kwa kujitahidi kujua jinsi Mungu anavyotaka tushughulikie hali hizo. (Methali 14:12) Kumbuka kwamba ingawa ni muhimu kufanya amani na washiriki wa familia yako, ni jambo la muhimu hata zaidi kuwa na amani na Yehova na Mwana wake.—Mathayo 10:37.

‘MTAJARIBIWA’

Yosefu aliwajaribu ndugu zake ili kujua mtazamo wao. Alizungumza nao kwa ukali akitumia mtafsiri, na kudai kwamba walikuwa wapelelezi kutoka nchi nyingine. Ili kujitetea, walimweleza kuhusu familia yao na kutaja kuhusu ndugu yao mdogo waliyemwacha nyumbani. Yosefu alijaribu kuficha furaha yake. Baada ya kujua kwamba mdogo wake yuko hai, Yosefu alijua jambo la kufanya. Alisema hivi: ‘Hivi ndivyo mtakavyojaribiwa,’ kisha akawaambia kwamba ni lazima amwone ndugu yao mdogo. Baadaye, aliwaruhusu warudi nyumbani kwao ili wamlete ndugu yao mdogo ikiwa mmoja wao angekubali kubaki akiwa mfungwa.—Mwanzo 42:9-20.

Ndugu hao walipokuwa wakizungumza bila kujua kwamba Yosefu aliwaelewa, walijilaumu kwa sababu ya dhambi nzito waliyofanya miaka 20 iliyopita. Walisema hivi: “Bila shaka tuna hatia kuhusiana na ndugu yetu, kwa sababu tuliona nafsi yake ikitaabika alipotuomba kwa bidii tumwonee huruma, lakini sisi hatukusikiliza. Ndiyo sababu taabu hii imetupata.” Yosefu alielewa walichosema, naye alijitenga nao ili wasimwone alipokuwa akilia. (Mwanzo 42:21-24) Hata hivyo, alijua kwamba toba ya kweli inahusisha mengi zaidi ya kujutia tu matokeo ya matendo maovu. Hivyo, aliendelea kuwajaribu.

Alimfunga gerezani Simeoni na kuwaruhusu ndugu zake warudi nyumbani. Aliamuru pia kwamba pesa zao ziwekwe bila wao kujua katika mifuko yao ya chakula wanachopeleka nyumbani. Ndugu hao walisafiri mpaka nyumbani kwao, na baada ya jitihada nyingi walifanikiwa kumshawishi Yakobo amruhusu mwana wake mpendwa, Benyamini ili waende naye Misri. Walipofika Misri, walimwambia wazi mtumishi wa Yosefu kuhusu pesa walizopata katika mifuko yao, na hata walitaka kulipa pesa hizo. Ijapokuwa ombi hilo lilivutia, bado Yosefu alitaka kuona utu halisi wa ndugu zake. Hivyo, aliwaandalia karamu, naye alijitahidi sana kuficha hisia zake baada ya kumwona Benyamini. Kisha, aliwaruhusu warudi nyumbani kwao wakiwa na chakula kingi, lakini aliamuru kikombe cha fedha kiwekwe katika mfuko wa Benyamini.—Mwanzo 42:26–44:2.

Kisha, Yosefu akategua mtego wake. Aliagiza ndugu zake wafuatiliwe, wakamatwe, na kushtakiwa kwa sababu ya kuiba kikombe. Ndugu wote walirudishwa kwa Yosefu kikombe hicho kilipopatikana kwenye mfuko wa Benyamini. Sasa, Yosefu alikuwa na nafasi ya kujua kikweli mtazamo ndugu zake. Yuda alikuwa msemaji wao. Aliomba waonyeshwe rehema, na hata alisema kwamba ndugu wote 11 wako tayari kuwa watumwa katika nchi ya Misri. Yosefu alisisitiza kwamba Benyamini tu ndiye aliyepaswa kubaki Misri akiwa mtumwa, lakini ndugu wote walipaswa kuondoka.—Mwanzo 44:2-17.

Yuda alichochewa kujibu kwa maneno yenye kugusa moyo. Alisema hivi: “Yeye tu ndiye aliyesalia wa mama yake, na baba yake anampenda.” Ni wazi kwamba maneno hayo yaligusa moyo wa Yosefu aliyekuwa mwana mkubwa wa Raheli, mke mpendwa wa Yakobo. Raheli alikufa alipokuwa akimzaa Benyamini. Kama baba yake, ni wazi kwamba Yosefu alimkumbuka sana Raheli. Huenda hilo lilimfanya Yosefu ampende sana Benyamini.—Mwanzo 35:18-20; 44:20.

Yuda aliendelea kumsihi Yosefu asimfanye Benyamini kuwa mtumwa. Hata alijitolea kuwa mtumwa badala ya Benyamini. Kisha akamalizia kwa kutoa ombi hili lenye kugusa moyo: “Ninawezaje kwenda kwa baba yangu bila yeye nisije nikautazama msiba utakaompata baba yangu?” (Mwanzo 44:18-34) Huo ulikuwa uthibitisho ulio wazi wa mwanamume aliyebadili mtazamo wake. Hakuonyesha tu toba bali pia sifa nzuri zinazofaa kama vile hisia-mwenzi, kutokuwa na ubinafsi, na huruma.

Yosefu aliona kwamba ndugu zake walijutia matendo yao

Yosefu alishindwa kuvumilia. Aliamua kuonyesha wazi hisia zake. Baada ya kuamuru watumishi wake waondoke, alilia kwa sauti hivi kwamba watu katika nyumba ya Farao wakasikia. Hatimaye akajitambulisha kwa ndugu zake kwa kusema: “Mimi ni Yosefu ndugu yenu.” Akawakumbatia ndugu zake waliokuwa wakishangaa, na kwa fadhili akawasamehe yote waliyomtendea. (Mwanzo 45:1-15) Hivyo, alionyesha mtazamo kama wa Yehova aliye tayari kusamehe. (Zaburi 86:5) Je, sisi hufanya hivyo pia?

“UNGALI HAI”!

Farao alipoambiwa habari kamili kuhusu kelele alizosikia kutoka katika nyumba ya Yosefu, alimwambia Yosefu amlete baba yake aliyekuwa mzee na familia yote, Misri. Hatimaye, Yosefu alionana tena na baba yake mpendwa. Yakobo alilia na kusema hivi: “Sasa niko tayari kufa, kwa kuwa nimeuona uso wako, kwa maana ungali hai.”—Mwanzo 45:16-28; 46:29, 30.

Yakobo aliishi Misri kwa miaka 17. Katika kipindi hicho alitabiri baraka kwa watoto wake 12. Alimpa baraka mara mbili zaidi Yosefu, mwana wake wa 11, baraka ambazo mwana wa kwanza alipaswa kupewa. Makabila mawili ya Israeli yangetoka kwake. Vipi kuhusu Yuda, mtoto wake wa nne, aliyeonyesha waziwazi toba ya kweli? Alibarikiwa sana: Masihi angetoka katika ukoo wake!—Mwanzo, sura 48, 49.

Yakobo alipokufa akiwa na umri wa miaka 147, ndugu za Yosefu waliogopa kwamba huenda Yosefu angelipiza kisasi. Hata hivyo, Yosefu aliwahakikishia kwa upendo. Kwa muda mrefu alidumisha mtazamo wa kwamba kwa kuwa Yehova ndiye aliyewezesha familia yao ihamie Misri, ndugu zake hawakupaswa kuhisi vibaya kutokana na walichofanya. Aliwauliza swali hili la pekee: “Je, mimi niko mahali pa Mungu?” (Mwanzo 15:13; 45:7, 8; 50:15-21) Yosefu alimuona Yehova kuwa Hakimu mkamilifu. Yosefu alihisi kwamba hastahili kuadhibu wale ambao Yehova amewasamehe.—Waebrania 10:30.

Je, ni vigumu kwako kusamehe? Huenda ikawa vigumu hasa iwapo mtu fulani ametusababishia madhara kimakusudi. Hata hivyo, tukiwasamehe kutoka moyoni wale wanaoonyesha toba ya kweli, hilo litatusaidia kuponya maumivu mengi ya moyo wetu na wengine pia. Na tutakuwa tunaiga imani ya Yosefu na mfano wa Baba yake mwenye rehema, Yehova.

^ fu. 4 Soma makala zenye kichwa “Igeni Imani Yao” zilizo kwenye Mnara wa Mlinzi wa Agosti 1, 2014; Novemba 1, 2014; na Februari 1, 2015.