Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU

Je, Unapaswa Kusali?

Je, Unapaswa Kusali?

Huenda ukajiuliza, ‘Ikiwa Mungu anajua kila kitu kutia ndani mawazo na mahitaji yangu, kwa nini nisali?’ Hilo ni swali zuri. Hata Yesu alisema kwamba Mungu “anajua ni vitu gani mnavyohitaji hata kabla hamjamwomba.” (Mathayo 6:8) Mfalme Daudi wa Israeli la kale alitambua jambo hilo na akaandika hivi: “Hamna neno hata moja katika ulimi wangu, lakini, tazama! Ee Yehova, tayari unajua yote.” (Zaburi 139:4) Basi kwa nini tusali kwa Mungu? Ili kujibu swali hilo, acheni tuchunguze yale ambayo Biblia inasema kuhusu sala za waabudu wa Mungu. *

“Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”Yakobo 4:8

 SALA HUTUSAIDIA TUMKARIBIE MUNGU

Ingawa Biblia inasema Yehova * Mungu anajua kila kitu, inaonyesha kwamba haridhiki tu na kukusanya habari kuhusu waabudu wake. (Zaburi 139:6; Waroma 11:33) Kumbukumbu yake kubwa si kama kompyuta ambayo inahifadhi habari nyingi bila kufikiri. Kwa kweli, Mungu anapendezwa sana na hisia zetu za ndani kabisa kwa sababu anataka tumkaribie. (Zaburi 139:23, 24; Yakobo 4:8) Hiyo ndiyo sababu Yesu aliwatia moyo wafuasi wake wasali, hata ingawa Baba yake anajua vizuri mahitaji yetu ya lazima. (Mathayo 6:6-8) Kadiri tunavyomweleza Muumba wetu mawazo yetu, ndivyo tunavyozidi kumkaribia.

Nyakati nyingine huenda tusijue hasa tunachohitaji kuomba katika sala. Katika hali hizo, huenda Mungu akatambua hisia zetu za ndani na kutumia ujuzi wake mwingi kuhusu hali zetu ili kututimizia mahitaji yetu. (Waroma 8:26, 27; Waefeso 3:20) Tunapotambua kwamba Mungu amejibu sala zetu, hata katika njia isiyo ya moja kwa moja, tunamkaribia zaidi.

JE, MUNGU HUJIBU SALA ZOTE?

Biblia inatuhakikishia kwamba Mungu Mweza-Yote hujibu sala za watumishi wake waaminifu, na pia inatueleza kwa nini hasikilizi sala fulani. Kwa mfano, jeuri ilipokuwa imeenea sana katika Israeli la kale, Mungu alimwongoza nabii wake Isaya awaambie watu hivi: “Hata mjapotoa sala nyingi, mimi sisikilizi; mikono yenu imejaa umwagaji wa damu.” (Isaya 1:15) Ni wazi kwamba wale wanaopuuza sheria za Mungu au kusali wakiwa na malengo yasiyofaa hawawezi kusikilizwa na Mungu.Methali 28:9; Yakobo 4:3.

Kwa upande mwingine, Biblia inasema: “Hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.” (1 Yohana 5:14) Je, hilo linamaanisha kwamba Mungu huwatimizia waabudu wake chochote wanachoomba? La hasha. Hebu mfikirie mtume Paulo aliyemwomba Mungu mara tatu amwondolee “mwiba katika mwili.” (2 Wakorintho 12:7, 8) Huenda Paulo alikuwa na tatizo la macho kwa muda mrefu. Hilo lilimvunja moyo sana! Paulo alikuwa amepewa zawadi ya kuponya na hata alikuwa amemfufua mtu, lakini alilazimika kuvumilia ugonjwa wake mwenyewe. (Matendo 19:11, 12; 20:9, 10) Ingawa sala yake haikujibiwa kama alivyotaka, Paulo alithamini jinsi Mungu alivyojibu sala yake.2 Wakorintho 12:9, 10.

“Huu ndio uhakika ambao tunao kwake, kwamba, hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.”1 Yohana 5:14

Ni kweli kwamba sala za watu fulani wanaotajwa katika Biblia zilijibiwa kimuujiza. (2 Wafalme 20:1-7) Lakini haikuwa hivyo sikuzote, hata katika nyakati za Biblia. Waamini fulani walikasirika ilipoonekana kwamba Mungu hakuwa amejibu sala zao. Mfalme Daudi aliuliza: “Utanisahau mpaka wakati gani, Ee Yehova? Milele?” (Zaburi 13:1) Lakini mwanamume huyo mwaminifu alipokumbuka jinsi Yehova alivyokuwa amemsaidia mara nyingi, Daudi alikiri tena jinsi alivyomtegemea Mungu. Katika sala hiyohiyo, Daudi aliongezea hivi: “Nami nimezitegemea fadhili zako zenye upendo.” (Zaburi 13:5) Kama Daudi, leo huenda waabudu wa Mungu wakahitaji kusali mara nyingi kabla Mungu hajajibu maombi yao.Waroma 12:12.

 JINSI MUNGU ANAVYOJIBU SALA

Mungu anatutimizia mahitaji muhimu.

Kwa kufaa, wazazi wanaojali hawawapi kila mara watoto wao kitu wanachoomba wakati wanapokiomba. Vivyo hivyo, huenda Mungu asitutimizie maombi yetu jinsi tunavyotazamia au wakati tunaotarajia. Lakini tunaweza kuwa na hakika kwamba Muumba wetu, kama baba mwenye upendo, atatutimizia mahitaji yetu muhimu wakati unaofaa na kwa njia inayofaa.—Luka 11:11-13.

Huenda Mungu akajibu sala zetu kupitia maandiko ya Biblia

Huenda Mungu asijibu moja kwa moja.

Namna gani ikiwa tunasali ili tupate kitulizo kutokana na tatizo linaloendelea? Je, tunapaswa kuamua kwamba kwa vile sala zetu hazijajibiwa kimuujiza, basi Yehova hajajibu? La hasha, ni vizuri tuchunguze kama Mungu ametusaidia kwa njia isiyo ya moja kwa moja. Kwa mfano, labda rafiki anayejali alitupatia msaada tuliohitaji wakati unaofaa. (Methali 17:17) Je, inawezekana kwamba Yehova alimtumia rafiki huyo kutusaidia? Kwa kuongezea, huenda Mungu akajibu sala zetu kupitia maandiko ya Biblia. Huenda tukapata katika Biblia hekima tunayohitaji kukabiliana na hali ngumu.2 Timotheo 3:16, 17.

Mungu anaweza kutumia marafiki wanaojali kutupatia msaada tunaohitaji wakati unaofaa

Badala ya kutuondolea tatizo, wakati mwingine Mungu huwapa watu wake nguvu za kulikabili. (2 Wakorintho 4:7) Kwa mfano, Yesu alipomsihi Baba yake amwondolee hali fulani, akiogopa kwamba jina la Mungu lingetiwa suto, Yehova alimtuma malaika ili amwimarishe. (Luka 22:42, 43) Vivyo hivyo, Mungu anaweza kutumia marafiki wa karibu kutuimarisha tunapohitaji sana kufarijiwa. (Methali 12:25) Kwa vile jibu kama hilo si la moja kwa moja, huenda tukahitaji kuwa macho ili kutambua jinsi Mungu anavyojibu sala zetu.

Huenda tukahitaji kusubiri Mungu ajibu kwa wakati wake.

Biblia inaonyesha kwamba Mungu Mweza-Yote anawaonyesha kibali watu wanyenyekevu “wakati unaofaa.” (1 Petro 5:6) Basi, tunapohisi kwamba Mungu anakawia kujibu maombi yetu, hatupaswi kufikiri hatujali. Badala yake, kwa vile ana ujuzi mwingi, Muumba wetu mwenye upendo huchunguza maombi yetu huku akifikiria kinachotufaa.

“Jinyenyekezeni chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu, ili awainue ninyi katika wakati unaofaa.”1 Petro 5:6

Kwa mfano: Jiwazie ukiwa mzazi wa mvulana mdogo anayekuomba umnunulie baiskeli. Je, utamnunulia mara moja? Ukihisi kwamba anaweza kuhatarisha maisha yake kwa kuendesha baiskeli, huenda ukaamua kumnunulia wakati mwingine. Hata hivyo, baada ya muda unaweza kumnunulia unapojua kwamba haitakuwa hatari kwake. Vivyo hivyo, huenda Mungu akatupatia “maombi ya moyo [wetu]” wakati unaofaa tukiendelea kusali.Zaburi 37:4.

UWE NA HAKIKA KWAMBA MUNGU HUSIKILIZA

Biblia inawatia moyo Wakristo wasipuuze nguvu ya sala. Huenda wengine wakasema ‘Si rahisi kufanya hivyo.’ Ni kweli kwamba kama tumekuwa tukipambana na tatizo kwa muda mrefu au kutendewa isivyo haki, huenda tukashindwa kusubiri Mungu ajibu sala zetu. Hata hivyo, ni vizuri kukumbuka Yesu alifundisha kuhusu uhitaji wa kuendelea kusali sikuzote.

Yesu alitoa mfano wa mjane maskini aliyeenda tena na tena kwa mwamuzi fulani ili kupata haki. (Luka 18:1-3) Ingawa mwanzoni mwamuzi alikataa  kumsaidia, mwishowe alijiambia: “Nitahakikisha kwamba atapata haki, ili asiendelee kuja kunishambulia mpaka animalize.” (Luka 18:4, 5) Kulingana na maneno ya lugha ya awali, mwamuzi alimsikiliza yule mjane ili “asimpige [mwamuzi] chini ya jicho,” au kwa maana nyingine, “kumharibia [mwamuzi] sifa.” * Kama mwamuzi asiyemwogopa Mungu alimsaidia mjane ili asiharibiwe sifa, je, Mungu wetu mwenye upendo hatawatendea haki wale ambao “wanampaazia sauti mchana na usiku”? Kama Yesu alivyosema, Mungu “atasababisha watendewe haki upesi.”Luka 18:6-8.

“Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa.”Luka 11:9

Ingawa huenda nyakati nyingine tukachoka kuomba msaada au kibali, hatupaswi kuvunjika moyo. Kwa kuendelea kusali, tunaonyesha kwamba kwa kweli tunatamani kupata msaada wa Mungu. Pia, tunajionea jinsi Mungu anavyojibu maombi yetu, na hivyo, tunamkaribia zaidi. Ndiyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atajibu sala zetu ikiwa tutaendelea kusali tukiamini kwamba atatusikiliza.Luka 11:9.

^ fu. 3 Ikiwa tunataka Mungu asikilize sala zetu, tunapaswa kujitahidi kabisa kufuata amri zake. Tukifanya hivyo, tunaweza kujionea nguvu za sala, kama inavyozungumziwa kwenye makala hii. Kwa habari zaidi, soma sura ya 17 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, au utembelee www.pr418.com/sw.

^ fu. 5 Yehova ni jina la Mungu kama linavyofunuliwa katika Biblia.

^ fu. 22 Nyakati za Biblia, Mungu aliwaagiza waamuzi Waisraeli wawatendee wajane na mayatima kwa njia ya pekee.Kumbukumbu la Torati 1:16, 17; 24:17; Zaburi 68:5.