Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 BIBLIA INABADILI MAISHA

Walitumia Biblia Kujibu Maswali Yangu Yote!

Walitumia Biblia Kujibu Maswali Yangu Yote!
  • ALIZALIWA:1950

  • NCHI:HISPANIA

  • HISTORIA:MTAWA MKATOLIKI

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilipozaliwa, wazazi wangu walikuwa na shamba dogo kijijini huko Galicia, kaskazini magharibi mwa Hispania. Nilikuwa mtoto wa nne kati ya watoto wanane. Tuliishi maisha yenye furaha. Enzi hizo nchini Hispania, ilikuwa kawaida kwa angalau mtoto mmoja katika familia kwenda kwenye shule ya seminari au kuwa mtawa. Katika familia yetu, watatu kati yetu tuliamua kufanya hivyo.

Nilipofikisha umri wa miaka 13, nilijiunga na dada yangu kwenye makao ya watawa huko Madrid. Hali haikuwa nzuri. Hakukuwa na urafiki, badala yake kulikuwa na sheria chungu nzima, kusali kila mara, na hakukuwa na muda wa michezo. Kila siku alfajiri tulikusanyika kanisani ili kutafakari, ingawa akili yangu ilitangatanga. Kisha tuliimba nyimbo za kidini na kuhudhuria Misa, mambo yote yaliendeshwa kwa Kilatini. Sikuelewa chochote na nilihisi kwamba Mungu hanijali. Yalikuwa maisha yasiyo na uchangamfu. Hata mimi na dada yangu tulipokutana tulisalimiana kwa kusema tu, “Salamu Maria.” Baada ya kila mlo tuliruhusiwa kuzungumza kwa nusu saa tu. Ilikuwa tofauti sana na jinsi tulivyoishi nyumbani. Nilijihisi mpweke na nililia mara kwa mara.

Ingawa sikumpenda sana Mungu, nilikula kiapo cha kuwa mtawa nilipokuwa na umri wa miaka 17. Kwa kweli, nilijitahidi kufuata maagizo, lakini baada ya muda nikaanza kujiuliza ikiwa kweli Mungu alitaka niwe mtawa. Watawa walisema kwamba mtu ambaye alikuwa na shaka angeenda kuteswa motoni! Hata hivyo, bado niliendelea kuwa na shaka. Nilijua kwamba Yesu Kristo hakujitenga na watu, bali aliwafundisha na kuwasaidia. (Mathayo 4:23-25) Nilipokuwa na umri wa miaka 20, sikutaka kuendelea kuwa mtawa. Kwa kushangaza, msimamizi wa watawa aliniambia ikiwa nilikuwa na shaka, afadhali niondoke mara moja. Huenda aliogopa kwamba ningewashawishi wengine. Hivyo nikaondoka.

 Niliporudi nyumbani, wazazi wangu walinielewa. Kwa sababu sikuweza kupata kazi kijijini kwetu, niliamua kuhamia Ujerumani, ambako kaka yangu alikuwa anaishi. Alikuwa mwanachama wa kikundi cha Kikomunisti cha wahamiaji Wahispania. Nilifurahia kuwa miongoni mwa watu hao waliopigania haki za wafanyakazi na usawa wa wanawake. Hivyo, mimi pia nikawa Mkomunisti na nikaolewa na mmoja wa wanachama wa kikundi hicho. Nilifikiri kwamba nilikuwa nikifanya jambo muhimu, kugawa machapisho ya Kikomunisti na kujihusisha kwenye maandamano.

Hata hivyo, baada ya muda nikakata tamaa tena. Niliona kwamba Wakomunisti hawakutenda kulingana na mambo waliyosema. Hisia hizo zilizidi mwaka wa 1971, baadhi ya vijana wa kikundi chetu walipochoma jengo la ubalozi wa Hispania jijini Frankfurt. Walifanya hivyo ili kulalamikia ukosefu wa haki nchini Hispania. Hata hivyo, niliamini kwamba hiyo haikuwa njia sahihi ya kulalamika.

Mwana wangu wa kwanza alipozaliwa, nilimwambia mume wangu kwamba ningeacha kuhudhuria mikutano ya Wakomunisti. Nilihisi mpweke kwa sababu marafiki wangu wa zamani hawakunitembelea. Nilijiuliza kuhusu kusudi la maisha. Je, kulikuwa na faida yoyote ya kujaribu kuboresha jamii?

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Mwaka wa 1976, nilitembelewa na wenzi wa ndoa Wahispania waliokuwa Mashahidi wa Yehova, na wakanipatia machapisho. Waliporudi tena niliwauliza maswali mengi kuhusu mateso, usawa, na ukosefu wa haki. Nilishangaa kuona kwamba walitumia Biblia kujibu kila swali! Mara moja nikakubali wanifundishe Biblia.

At first, mMwanzoni nilitaka tu kujifunza mambo mapya. Lakini mambo yalibadilika wakati mimi na mume wangu tulipoanza kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Kufikia wakati huo tulikuwa na watoto wawili. Mashahidi walitubeba kwenye magari yao na kutusaidia kuwatuliza watoto wetu mikutanoni. Nikaanza kuwapenda sana Mashahidi.

Licha ya hayo, bado nilikuwa na shaka kuhusu dini. Niliamua kutembelea familia yangu huko Hispania. Mjomba wangu, ambaye alikuwa kasisi, alijaribu kunivunja moyo nisiendelee kujifunza Biblia. Lakini Mashahidi wa eneo hilo walinisaidia sana. Walitumia Biblia kujibu maswali yangu, sawa tu na wale Mashahidi wa Ujerumani. Niliamua kuendelea kujifunza Biblia niliporudi Ujerumani. Ingawa mume wangu aliacha kujifunza Biblia, mimi niliendelea. Kisha mwaka wa 1978, nikabatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Ujuzi sahihi wa Biblia umenisaidia kupata kusudi na mwongozo maishani. Kwa mfano, andiko la 1 Petro 3:1-4 linawatia moyo wake ‘wajitiishe’ kwa waume zao na wawe “na heshima kubwa” na kusitawisha “roho ya utulivu na ya upole, ambayo ni ya thamani kubwa machoni pa Mungu.” Kanuni hizo zimenisaidia kutimiza wajibu wangu kama mke na pia mama.

Zaidi ya miaka 35 imepita tangu nilipoamua kuwa Shahidi wa Yehova. Nafurahi kuwa miongoni mwa familia ya kiroho, na pia nafurahi kwa sababu watoto wangu wanne kati ya watano wamefanya hivyo pia.