Kulingana na Luka 22:1-71

  • Makuhani wapanga njama ya kumuua Yesu (1-6)

  • Matayarisho ya Pasaka ya mwisho (7-13)

  • Mlo wa Jioni wa Bwana waanzishwa (14-20)

  • ‘Msaliti wangu yuko pamoja nami mezani’ (21-23)

  • Wabishana vikali kuhusu aliye mkuu zaidi (24-27)

  • Yesu afanya agano kwa ajili ya ufalme (28-30)

  • Yesu atabiri Petro atamkana (31-34)

  • Uhitaji wa kuwa tayari; panga mbili (35-38)

  • Yesu asali kwenye Mlima wa Mizeituni (39-46)

  • Yesu akamatwa (47-53)

  • Petro amkana Yesu (54-62)

  • Yesu adhihakiwa (63-65)

  • Kesi mbele ya Sanhedrini (66-71)

22  Sasa Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu, inayoitwa, Pasaka,+ ilikuwa imekaribia.+  Nao wakuu wa makuhani na waandishi walikuwa wakitafuta njia bora ya kumuua,+ kwa sababu waliwaogopa watu.+  Ndipo Shetani akamwingia Yuda, aliyeitwa Iskariote, ambaye alikuwa mmoja wa wale 12,+  naye akaenda kuongea na wakuu wa makuhani na makapteni wa hekalu kuhusu jinsi atakavyomsaliti kwao.+  Wakafurahishwa na jambo hilo, nao wakakubaliana kumpa fedha.+  Basi akakubali na kuanza kutafuta nafasi nzuri ya kumsaliti kwao bila umati kuwapo.  Siku ya Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu ikafika, siku ambayo dhabihu ya Pasaka hutolewa;+  basi Yesu akawatuma Petro na Yohana, akawaambia: “Nendeni mkatutayarishie Pasaka tule.”+  Wakamuuliza: “Unataka tuitayarishe wapi?” 10  Akawaambia: “Tazameni! Mtakapoingia jijini, mtakutana na mwanamume akiwa amebeba mtungi wa maji. Mfuateni mwingie katika nyumba atakayoingia.+ 11  Mwambieni mwenye nyumba hiyo, ‘Mwalimu anasema: “Kiko wapi chumba cha wageni ambamo ninaweza kula Pasaka pamoja na wanafunzi wangu?”’ 12  Mtu huyo atawaonyesha chumba kikubwa cha juu chenye vifaa. Tayarisheni humo.” 13  Basi wakaenda na kupata kama alivyokuwa amewaambia, nao wakaandaa Pasaka. 14  Wakati ulipofika, akaketi mezani pamoja na mitume.+ 15  Akawaambia: “Nimetamani sana kula Pasaka hii pamoja nanyi kabla sijateseka; 16  kwa maana ninawaambia, sitakula tena Pasaka mpaka itakapotimizwa katika Ufalme wa Mungu.” 17  Yesu akapokea kikombe, akashukuru na kusema: “Chukueni kikombe hiki na mkipitishe kutoka kwa mmoja mpaka kwa mwingine kati yenu, 18  kwa maana ninawaambia, kuanzia sasa sitakunywa tena divai ya mzabibu mpaka Ufalme wa Mungu utakapokuja.” 19  Pia, akachukua mkate,+ akashukuru na kuumega, akawapa akisema: “Huu unamaanisha mwili wangu,+ ambao utatolewa kwa ajili yenu.+ Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka.”+ 20  Pia, akafanya vivyo hivyo na kile kikombe baada ya wao kula mlo wa jioni, akisema: “Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya+ kwa msingi wa damu yangu,+ ambayo itamwagwa kwa ajili yenu.+ 21  “Lakini tazameni! mkono wa msaliti wangu uko pamoja nami mezani.+ 22  Kwa kweli, Mwana wa binadamu anaenda zake kama ilivyotabiriwa;+ lakini ole wake mtu atakayemsaliti!”+ 23  Kwa hiyo wakaanza kuulizana ni nani kati yao ambaye angemsaliti.+ 24  Hata hivyo, pia kukatokea bishano kali kuhusu ni nani aliyekuwa mkuu zaidi kati yao.+ 25  Lakini akawaambia: “Wafalme wa mataifa hupiga ubwana juu yao, na wale walio na mamlaka juu yao huitwa Wafadhili.+ 26  Hata hivyo, ninyi hampaswi kuwa hivyo.+ Lakini yule aliye mkuu zaidi kati yenu anapaswa kuwa mdogo zaidi,+ na yule anayeongoza awe kama anayehudumu. 27  Kwa maana ni nani aliye mkuu zaidi, yule anayekula* au yule anayehudumu?* Ni yule anayekula,* sivyo? Lakini mimi ni kama mtu anayehudumu* kati yenu.+ 28  “Hata hivyo, ninyi ndio mmeshikamana nami+ katika majaribu yangu;+ 29  nami ninafanya agano pamoja nanyi, kama Baba yangu alivyofanya agano pamoja nami, kwa ajili ya ufalme,+ 30  ili mle na kunywa mezani pangu katika Ufalme wangu,+ na kuketi kwenye viti vya ufalme+ ili kuyahukumu makabila 12 ya Israeli.+ 31  “Simoni, Simoni, tazama! Shetani anataka kuwapata ninyi nyote ili awapepete kama ngano.+ 32  Lakini nimeomba dua kwa ajili yako ili imani yako isidhoofike;+ nawe utakaporudi, watie nguvu ndugu zako.”+ 33  Petro akasema: “Bwana, niko tayari kwenda nawe gerezani na hata kufa nawe.”+ 34  Lakini akamwambia: “Petro ninakuambia, leo kabla jogoo hajawika utanikana mara tatu.”+ 35  Akawauliza: “Nilipowatuma bila mkoba wa pesa, mfuko wa chakula, na viatu,+ je, mlikosa chochote?” Wakajibu: “Hapana!” 36  Kisha akawaambia: “Lakini sasa yule aliye na mkoba wa pesa au mfuko wa chakula aubebe, na yule asiye na upanga, auze vazi lake la nje anunue upanga. 37  Kwa maana ninawaambia mambo yaliyoandikwa kunihusu yatatimia, yaani, ‘Naye alihesabiwa pamoja na waasi sheria.’+ Kwa maana hilo linatimia kunihusu.”+ 38  Kisha wakasema: “Bwana, tazama! hapa pana panga mbili.” Akawaambia: “Inatosha.” 39  Alipoondoka, kama kawaida yake alienda kwenye Mlima wa Mizeituni, nao wanafunzi pia wakamfuata.+ 40  Walipofika huko akawaambia: “Endeleeni kusali ili msiingie katika majaribu.”+ 41  Akawaacha na kwenda umbali wa mtupo wa jiwe, akapiga magoti na kuanza kusali, 42  akisema: “Baba, ukipenda, niondolee kikombe hiki. Hata hivyo, si kama ninavyopenda, bali mapenzi yako na yatendeke.”+ 43  Ndipo malaika kutoka mbinguni akaja na kumtia nguvu.+ 44  Lakini alikuwa na maumivu makali hivi kwamba akaendelea kusali kwa bidii zaidi;+ na jasho lake likawa kama matone ya damu yakidondoka chini. 45  Baada ya kusali, akawaendea wanafunzi, akawakuta wakiwa wamelala usingizi, wakiwa wamechoka kwa sababu ya huzuni.+ 46  Akawaambia: “Kwa nini mnalala? Amkeni mwendelee kusali, ili msiingie katika majaribu.”+ 47  Alipokuwa bado akizungumza, tazama! umati ukaja ukiongozwa na Yuda, mmoja wa wale 12, naye akamkaribia Yesu ili ambusu.+ 48  Lakini Yesu akamuuliza: “Yuda, unamsaliti Mwana wa binadamu kwa busu?” 49  Wale waliomzunguka walipoona jambo lililokuwa karibu kutukia, wakasema: “Bwana, tuwashambulie kwa upanga?” 50  Mmoja wao hata akampiga mtumwa wa kuhani mkuu na kumkata sikio la kulia.+ 51  Lakini Yesu akasema: “Inatosha.” Akaligusa sikio la yule mtumwa akamponya. 52  Kisha Yesu akawauliza wakuu wa makuhani na makapteni wa hekalu na wazee waliokuja kumkamata: “Je, mmekuja kunikamata mkiwa na mapanga na marungu kana kwamba mimi ni mwizi?+ 53  Nilipokuwa pamoja nanyi hekaluni siku baada ya siku,+ hamkunikamata.+ Lakini huu ndio wakati wenu na mamlaka ya giza.”+ 54  Ndipo wakamkamata,+ na kumpeleka nyumbani kwa kuhani mkuu; lakini Petro alikuwa akiwafuata kwa mbali.+ 55  Walipowasha moto katikati ya ua na kuketi chini pamoja, Petro alikuwa ameketi miongoni mwao.+ 56  Lakini kijakazi mmoja akamwona Petro akiwa ameketi kando ya moto, akamtazama kwa makini na kusema: “Mtu huyu pia alikuwa pamoja naye.” 57  Lakini Petro akakana, akisema: “Wewe mwanamke, mimi simjui.” 58  Baadaye kidogo mtu mwingine akamwona na kusema: “Wewe pia ni mmoja wao.” Lakini Petro akasema: “Mimi si mmoja wao.”+ 59  Baada ya saa moja hivi kupita mwanamume mwingine akaanza kusisitiza kwa nguvu: “Kwa hakika mtu huyu pia alikuwa pamoja naye, kwa maana, yeye ni Mgalilaya!” 60  Lakini Petro akasema: “Wewe mtu, mimi sielewi unachosema.” Mara tu alipokuwa akisema, jogoo akawika. 61  Ndipo Bwana akageuka, akamtazama Petro moja kwa moja, naye Petro akakumbuka maneno ambayo Bwana alimwambia: “Kabla jogoo hajawika leo, utanikana mara tatu.”+ 62  Naye akaenda nje akalia kwa uchungu. 63  Sasa wale wanaume waliokuwa wamemkamata Yesu wakaanza kumdhihaki+ na kumpiga;+ 64  na baada ya kumfunika uso wakawa wakisema: “Toa unabii! Ni nani aliyekupiga?” 65  Nao wakasema mambo mengine mengi ya kumkufuru. 66  Kulipokuwa mchana, kikundi cha wazee wa watu, yaani, wakuu wa makuhani na waandishi, wakakusanyika pamoja,+ nao wakampeleka katika jumba lao la Sanhedrini, na kumwambia: 67  “Ikiwa wewe ndiye Kristo, tuambie.”+ Lakini akasema: “Hata nikiwaambia, hamtaamini hata kidogo. 68  Isitoshe, ikiwa ningewauliza, hamngenijibu. 69  Hata hivyo, tangu sasa Mwana wa binadamu+ ataketi kwenye mkono wa kuume wenye nguvu wa Mungu.”+ 70  Ndipo wote wakasema: “Kwa hiyo, je, wewe ndiye Mwana wa Mungu?” Akawajibu: “Ninyi wenyewe mnasema kwamba mimi ndiye.” 71  Wakasema: “Kwa nini tutafute ushahidi zaidi? Kwa maana sisi wenyewe tumesikia kutoka kinywani mwake.”+

Maelezo ya Chini

Au “mtumishi.”
Au “anayeketi mezani.”
Au “mtumishi.”
Au “anayeketi mezani.”