Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 BIBLIA INABADILI MAISHA

“Yehova Hakuwa Amenisahau”

“Yehova Hakuwa Amenisahau”
  • ALIZALIWA: 1922

  • NCHI: HISPANIA

  • HISTORIA: MWALIMU WA KATEKISIMU

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilizaliwa jijini Bilbao, kaskazini mwa Hispania katika mtaa wa watu wenye mapato ya kadiri. Nilikuwa mtoto wa pili katika familia ya watoto wanne. Wazazi wetu walikuwa Wakatoliki wenye bidii, kwa hiyo nilihudhuria Misa kila siku. Nilipokuwa na umri wa miaka 23, nikawa mwalimu—kazi niliyopenda na kuifanya kwa miaka 40. Kati ya masomo yote, nilipenda sana kufundisha somo la Ukatoliki, na kila jioni nilifundisha katekisimu, yaani, niliwafundisha wasichana waliotarajia kupata ekaristi ya kwanza.

Baada ya miaka 12 ya ndoa yenye furaha, mume wangu alikufa na kuniacha na mabinti wanne. Nilikuwa na umri wa miaka 33 tu! Nilitafuta faraja katika dini yangu ya Kikatoliki, lakini nilisumbuliwa na maswali mengi. Nilijiuliza: ‘Ikiwa Kristo alitukomboa, kwa nini wanadamu wanaendelea kufa? Kwa nini tunasali Ufalme wa Mungu uje ikiwa watu wema huenda mbinguni?’ Zaidi ya yote, nilijiuliza: ‘Ikiwa Mungu anatuhukumu tunapokufa, kwa nini tena baadaye tutahitaji kutoka mbinguni, toharani, au motoni ili kuhukumiwa tena?’

Niliwauliza mapadri niliokutana nao maswali hayo. Padri mmoja alinijibu: “Sijui. Muulize askofu. Kwa nini unauliza maswali hayo yote? Unamwamini Mungu, sivyo? Achana na maswali hayo!” Hata hivyo niliendelea kutafuta majibu. Baadaye nilihudhuria mafundisho ya Wayesuti, Wapentekoste, na Waagnosti. Hata hivyo, sikupata majibu yenye kuridhisha.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Nilipokuwa na umri wa miaka 60 hivi, msichana mwenye umri wa miaka saba alinialika nihudhurie mkutano wa Mashahidi wa Yehova. Nilifurahia yale niliyoona na kusikia, lakini kwa sababu nilikuwa na shughuli nyingi, sikuwasiliana tena na Mashahidi. Miaka miwili baadaye, nilitembelewa na wenzi wa ndoa Juan na Maite waliokuwa Mashahidi. Kwa miezi mitatu, tulikuwa na majadiliano mazuri, na mwishowe nikakubali kujifunza Biblia.

Nilifurahia sana mafundisho hayo! Nilichunguza mambo  yote kwa makini, nikitumia tafsiri tatu tofauti za Biblia ili kuhakikisha kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wakifundisha kweli. Niligundua kwamba kwa miaka mingi sikuwa nimefundishwa ukweli katika dini yangu. Niliona tofauti kubwa kati ya mafundisho ya dini yangu na yale niliyokuwa nikijifunza katika Biblia. Nililazimika kubadili mambo niliyoamini zamani, ni kana kwamba mti wenye mizizi yenye kina ulikuwa uking’olewa.

Nilijua kwamba nilikuwa nimepata hazina

Baadaye, mume wangu wa pili aliugua sana na kufa. Wakati huo nilistaafu na nikaondoka Bilbao kwa muda. Juan na Maite pia walihama. Kwa kusikitisha niliacha kujifunza Biblia. Hata hivyo, moyoni nilijua kwamba nilikuwa nimepata hazina.

Miaka 20 baadaye, nikiwa na umri wa miaka 82, Juan na Maite walirudi Bilbao na wakanitembelea. Nilifurahi sana kuwaona! Nilitambua kwamba Yehova hakuwa amenisahau, na nikaanza kujifunza tena. Juan na Maite walinifundisha kwa subira na uvumilivu, kwa sababu mara nyingi niliuliza swali lilelile mara kwa mara. Nilitaka kusikia maoni ya Biblia tena na tena ili kubadili imani niliyokuwa nayo. Pia, nilitaka kuijua Biblia vizuri ili niweze kuwaeleza watu wa familia na rafiki zangu.

Hatimaye nikabatizwa—nikiwa na umri wa miaka 87—ilikuwa siku yenye furaha zaidi katika maisha yangu. Nilibatizwa kwenye kusanyiko la Mashahidi wa Yehova. Mzee Mkristo alitoa hotuba ambayo ilitegemea Biblia iliyokusudiwa hasa kwa ajili yetu tuliotaka kubatizwa. Nilitokwa na machozi nilipokuwa nikisikiliza hotuba hiyo. Nilisikiliza kwa makini kana kwamba Yehova alikuwa akizungumza nami. Baada ya kubatizwa, Mashahidi wengi walikuja kunipongeza—ingawa wengi wao hawakunifahamu!

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Sikuzote nilijua kwamba Yesu Kristo ndiye “njia.” (Yohana 14:6) Lakini mafundisho ya Biblia yalinisaidia kumjua Yehova, ambaye Yesu anatuongoza kwake. Sasa ninaweza kusali kwa Mungu akiwa Baba na Rafiki yangu mpendwa. Kusoma kitabu Mkaribie Yehova * kulibadili maisha yangu. Mara ya kwanza nilikisoma chote kwa usiku mmoja! Niliguswa moyo nilipojifunza jinsi Yehova alivyo mwenye rehema.

Ninapofikiria jitihada zangu za kutafuta mafundisho ya kweli, ninakumbuka maneno haya ya Yesu: “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kupiga hodi, nanyi mtafunguliwa.” (Mathayo 7:7) Kwa sababu nimepata majibu niliyokuwa nikitafuta kwa miaka mingi, sasa ninafurahi kuwaeleza wengine mambo hayo.

Ingawa nina umri wa miaka 90, bado ninaendelea kujifunza kumhusu Yehova. Kila mkutano ninaohudhuria kwenye Jumba la Ufalme ni muhimu—kwa sababu ya mambo ninayojifunza na ushirika mzuri wa ndugu na dada zangu wapendwa. Ninatamani kuwa mwalimu tena kwenye dunia itakayokuwa Paradiso. (Ufunuo 21:3, 4) Kwa kweli ninatamani sana kuwaona wapendwa wangu watakapofufuliwa na kupata nafasi ya kuwafundisha Biblia. (Matendo 24:15) Pia, ninatamani kuwaeleza jinsi Yehova alivyonipa zawadi yenye thamani uzeeni!

^ fu. 15 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.