Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 BIBLIA INABADILI MAISHA

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha
  • MWAKA WA KUZALIWA: 1960
  • NCHI: FINLAND
  • HISTORIA: MWANAMUZIKI

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nililelewa katika eneo la watu wasio matajiri katika mji wa bandari wa Turku. Babangu alikuwa bondia maarufu, na mimi na ndugu yangu mdogo tulijihusisha pia na mchezo huo wa ngumi. Mara nyingi, nikiwa shuleni nilichokozwa na bila kusita nilipigana. Nilipokuwa kijana, nilijiunga na genge hatari, na nikawa mjeuri hata zaidi. Pia, nilivutiwa na muziki wenye mdundo mzito na nikatamani kuwa mwanamuziki maarufu.

Nilinunua ngoma kadhaa na nikaanzisha bendi, kisha nikawa mwimbaji mkuu katika bendi hiyo. Nilipenda kuimba kwa fujo nilipokuwa jukwaani. Kwa vile bendi yetu ilikuwa yenye fujo na vurugu, baada ya muda tukawa maarufu. Tukaanza kutumbuiza umati wa watu, tulirekodi nyimbo kadhaa, na rekodi ya mwisho ilipata umaarufu. Mwishoni mwa miaka ya 1980, tulisafiri kwenda Marekani ili kuendeleza bendi yetu. Tulifanya maonyesho katika majiji ya New York na Los Angeles, mara kadhaa na kufanya makubaliano na wauzaji maarufu wa muziki kabla ya kurejea Finland.

Ingawa nilifurahia kuwa kwenye bendi, nilitamani sana kuwa na maisha yenye kusudi. Sikufurahia ushindani katika biashara ya muziki na nilichoshwa na maisha yangu. Nilihisi kwamba nilikuwa mtu mwovu, na niliogopa kuchomwa kwenye moto wa mateso. Nilijaribu kutafuta majibu katika vitabu vya dini na nilisali sana ili Mungu anisaidie, hata ingawa nilihisi kwamba ingekuwa vigumu kumpendeza.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA MAISHA YANGU:

Ili kujitegemeza nilifanya kazi kwenye ofisi ya posta. Siku moja, niligundua kwamba mmoja wa wafanyakazi wenzangu alikuwa Shahidi wa Yehova. Nilimuuliza maswali mengi. Nilichochewa sana na majibu yake yaliyopatana na akili na yaliyotegemea Maandiko, na nikakubali anifundishe Biblia. Baada ya kujifunza kwa majuma kadhaa, bendi yetu ilipata mkataba ambao ungetuletea pesa nyingi wa kurekodi muziki huko Marekani. Sikutaka kupoteza nafasi hiyo.

 Nilimwambia Shahidi aliyekuwa akijifunza nami kwamba kwanza nilitaka kurekodi kwa mara ya mwisho, kisha nianze kufuata kanuni za Biblia nilizokuwa nikijifunza. Hakutoa maoni yake, badala yake aliniomba nisome maneno ya Yesu kwenye Mathayo 6:24. Mstari huo unasema: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili.” Nilishangaa nilipoelewa maana ya maneno ya Yesu. Lakini baada ya siku chache, nilimshangaza mwalimu wangu wa Biblia! Nilimwambia kwamba nilitaka kumfuata Yesu, hivyo nikaachana na ile bendi!

Biblia ilikuwa kama kioo kilichonisaidia kugundua kasoro zangu. (Yakobo 1:22-25) Nilitambua kwamba nilikuwa mkatili, mwenye majivuno, na nilijitakia makuu. Nilitumia lugha chafu, nilipigana, nilivuta sigara, na kulewa. Nilipotambua jinsi maisha yangu yalivyokuwa tofauti na kanuni za Biblia, nilivunjika moyo sana. Hata hivyo, nilikuwa tayari kufanya mabadiliko.—Waefeso 4:22-24.

“Baba yetu wa mbinguni ni mwenye rehema na anataka kuponya vidonda vya wale wanaotubu makosa yao”

Mwanzoni nililemewa na hisia za hatia kwa sababu ya makosa yangu ya zamani. Lakini Shahidi niliyekuwa nikijifunza naye alinisaidia sana. Alinionyesha andiko la Isaya 1:18 linalosema: “Hata dhambi zenu zikiwa nyekundu, zitafanywa kuwa nyeupe kama theluji.” Andiko hilo pamoja na mistari mingine ya Biblia ilinisaidia kuelewa kwamba Baba yetu wa mbinguni ni mwenye rehema na anataka kuponya vidonda vya wale wanaotubu makosa yao.

Nilipomjua Yehova na kumpenda, nilitaka kuweka maisha yangu wakfu kwake. (Zaburi 40:8) Nilibatizwa mwaka 1992 katika kusanyiko la kimataifa la Mashahidi wa Yehova huko St. Petersburg, Urusi.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Nimepata rafiki wengi wazuri miongoni mwa waabudu wa Yehova. Mara kwa mara tunakutana ili kucheza muziki na kufurahia zawadi hii nzuri kutoka kwa Mungu. (Yakobo 1:17) Baraka ya pekee ambayo nimepata ni mke wangu mpendwa, Kristina. Tumepitia mambo mengi pamoja—iwe ni shangwe au matatizo ya maisha, kutia ndani kumweleza hisia zangu za ndani kabisa.

Huenda ningekuwa nimekufa kama singekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Zamani nilikuwa na matatizo chungu nzima. Lakini sasa ninaishi maisha yenye kusudi na yenye utulivu.