Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Elias Hutter na Biblia Zake Bora Sana za Kiebrania

Elias Hutter na Biblia Zake Bora Sana za Kiebrania

JE, UNAWEZA kusoma Biblia ya Kiebrania? Huenda huwezi. Labda hata hujawahi kuona Biblia ya Kiebrania. Hata hivyo, huenda utaithamini zaidi nakala yako ya Maandiko Matakatifu kwa kuchunguza jambo fulani kumhusu msomi Elias Hutter wa karne ya 16 na matoleo mawili ya Biblia za Kiebrania aliyochapisha.

Elias Hutter alizaliwa mwaka wa 1553 huko Görlitz, mji mdogo ulio Ujerumani karibu na mpaka wa nchi hiyo na nchi ya Poland na Jamhuri ya Cheki. Hutter alijifunza lugha za watu wa Mashariki ya kati katika Chuo Kikuu cha Lutheran huko Jena. Alipokuwa na umri wa miaka 24 tu, alichaguliwa kuwa profesa wa lugha ya Kiebrania huko Leipzig. Akiwa mwanaharakati wa mambo ya elimu, alianzisha shule huko Nuremberg ambapo wanafunzi wangejifunza Kiebrania, Kigiriki, Kilatini, na Kijerumani ndani ya miaka minne. Hakuna shule au chuo kikuu kingine chochote kilichokuwa na uwezo wa kufanya hivyo.

“UBORA WA TOLEO HILI”

Ukurasa wenye kichwa katika Biblia ya Kiebrania ya Hutter ya mwaka wa 1587

Mwaka wa 1587, Hutter alichapisha toleo la Kiebrania la Maandiko ambayo wengi huyaita Agano la Kale. Toleo hilo lilikuwa na kichwa Derekh ha-Kodesh, kinachomaanisha “Njia ya Utakatifu” na kilitolewa katika andiko la Isaya 35:8. Muundo wa herufi unaopendeza ulimchochea mtu fulani aseme kwamba “kila kitu [katika Biblia hii] kinaonyesha ubora wa toleo hili.” Hata hivyo, thamani kubwa zaidi ya Biblia hiyo ilitokana na jinsi ilivyowasaidia wanafunzi waliokuwa wakijifunza Kiebrania.

Ili kuelewa kwa nini Biblia ya Kiebrania ya Hutter ilikuwa msaada mkubwa, fikiria changamoto mbili ambazo mtu aliyekuwa akijifunza Kiebrania alikabili alipokuwa akisoma Biblia katika lugha hiyo. Kwanza, ina alfabeti ambayo si ya kawaida na yenye muundo wa pekee, na pili, viambishi vilivyotumiwa vilifanya iwe vigumu kutambua mzizi wa neno. Kwa mfano, fikiria neno la Kiebrania נפשׁ (ne’phesh), linalomaanisha “nafsi.” Katika andiko la Ezekieli 18:​4, kiambishi awali kilichotumiwa katika neno hilo ni ה (ha), na hivyo kufanyiza neno הנפשׁ (han·ne’phesh). Kwa mtu asiyejua Kiebrania vizuri, huenda neno הנפשׁ (han·ne’phesh) likaonekana kuwa tofauti kabisa na נפשׁ (ne’phesh).

Ili kuwasaidia wanafunzi wake, Hutter alichapisha maneno ya Kiebrania kwa herufi zilizokolezwa wino na nyingine zisizokolezwa. Mbinu nzuri kwelikweli! Alitumia wino uliokolezwa katika mzizi wa neno, na wino usiokolezwa katika viambishi. Mbinu hiyo rahisi iliwawezesha wanafunzi kutambua mzizi wa neno la Kiebrania, na hivyo kuwasaidia kujifunza lugha hiyo. Biblia ya marejeo (New World Translation of the Holy Scriptures) inatumia mbinu inayofanana na hiyo katika maelezo ya chini. Mizizi ya maneno ya Kiebrania imeandikwa kwa wino uliokolezwa, ilhali viambishi vimeandikwa kwa njia ya kawaida. Mfano uliopo kwenye picha unaonyesha muundo wa herufi uliotumiwa katika Biblia ya Hutter ya Kiebrania kwenye andiko la Ezekieli 18:4 na ule uliotumiwa katika Biblia ya marejeo kwenye maelezo ya chini ya andiko hilohilo.

TOLEO LA KIEBRANIA LA “AGANO JIPYA”

Hutter alichapisha pia Maandiko ambayo wengi huyaita Agano Jipya, katika lugha 12 ndani ya buku moja. Toleo hilo lilichapishiwa jijini Nuremberg mwaka wa 1599 na linajulikana kama Nuremberg Polyglot. Hutter alitaka tafsiri ya lugha ya Kiebrania ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo iwe pia katika toleo hilo. Lakini alisema kwamba “hata ikiwa [angekuwa] tayari kutoa kiasi kikubwa sana cha pesa” ili apate tafsiri ya Kiebrania, haingewezekana kuipata. * Hivyo, aliamua kutafsiri mwenyewe Maandiko ya Agano Jipya kutoka Kigiriki kwenda Kiebrania. Hutter alikazia fikira zake zote katika kazi ya kutafsiri na akafaulu kuikamilisha ndani ya mwaka mmoja!

Tafsiri ya Hutter ya Kiebrania ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilikuwa bora kadiri gani? Mwaka wa 1891 msomi Mwebrania Franz Delitzsch aliandika hivi: “Tafsiri yake ya Kiebrania inafunua uelewaji wa lugha ambao ni nadra sana kuupata kati ya Wakristo na mpaka sasa tunaweza kuirejelea kwa sababu alifanikiwa kuchagua maneno yanayofaa kabisa katika visa mbalimbali.”

MATOKEO YENYE KUDUMU

Tafsiri ya Hutter haikumtajirisha; inaelekea kwamba matoleo yake hayakununuliwa sana. Ingawa hivyo, kazi yake imetoa msaada mkubwa wenye kudumu. Kwa mfano, tafsiri yake ya Kiebrania ya Agano Jipya iliboreshwa na kuchapishwa upya na William Robertson katika mwaka wa 1661, na baadaye katika mwaka wa 1798 na Richard Caddick. Alipokuwa akitafsiri kutoka kwenye Kigiriki cha awali, Hutter alitumia jina “Yehova” (יהוה, JHVH) badala ya majina ya cheo Kyʹri·os (Bwana) na The·osʹ (Mungu) katika sehemu zilizokuwa zimenukuliwa kutoka kwenye Maandiko ya Kiebrania au pale alipohisi kuwa vyeo hivyo vinamrejelea Yehova. Jambo hilo linapendeza kwa sababu ingawa tafsiri nyingi za Agano Jipya hazitumii jina la Mungu la kibinafsi, tafsiri ya Hutter inalitumia na hivyo imesaidia sana katika kurudisha jina hilo kwenye Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.

Hivyo basi kila mara unapoona jina la Mungu, Yehova, katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, kumbuka kazi ya Elias Hutter na Biblia zake bora sana za Kiebrania.

^ fu. 9 Bila shaka, tayari baadhi ya wasomi walikuwa wametafsiri Agano Jipya katika Kiebrania. Mmoja wao alikuwa Simon Atoumanos, katika miaka ya 1360. Mwingine alikuwa Oswald Schreckenfuchs, msomi Mjerumani, katika miaka ya 1565. Tafsiri hizo hazikuwahi kuchapishwa na hatimaye zilitoweka.