Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

BIBLIA INABADILI MAISHA

Nipe Amani na Furaha kwa Mwaka Mmoja Tu

Nipe Amani na Furaha kwa Mwaka Mmoja Tu
  • ALIZALIWA: 1971

  • NCHI: UFARANSA

  • HISTORIA: MHALIFU, ALITUMIA DAWA ZA KULEVYA, NA ALIKUWA NA MAADILI MAPOTOVU

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Familia yetu iliishi katika kijiji cha Tellancourt, kilichopo kaskazini-mashariki mwa Ufaransa. Baba yangu alikuwa Mfaransa na mama yangu Mwitaliano. Nilipokuwa na umri wa miaka nane, tulihamia katika eneo lenye watu maskini jijini Roma, Italia. Maisha yalikuwa magumu. Wazazi wangu waligombana sana kwa sababu ya matatizo ya kiuchumi.

Nilipokuwa na umri wa miaka 15, mama yangu alinitia moyo nitafute marafiki. Hivyo nilitumia wakati mwingi mbali na nyumbani. Baada ya muda nilianza kupata marafiki wabaya. Siku moja, nilikutana na mwanamume mmoja aliyejifanya mwenye urafiki. Alinipatia dawa za kulevya na nilizitumia ili nionekane mtu mzima. Muda si muda nilianza kutumia dawa za kulevya na kuwa na maadili mapotovu. Nilitendewa vibaya kingono mara nyingi. Maisha hayakuwa na maana yoyote kwangu wala sikujali ikiwa nitaishi au nitakufa. Nilikuwa mpweke sana. Nilipokuwa na umri wa miaka 16 nilijaribu kujiua kwa kunywa pombe kali na kisha kujirusha ziwani. Nilipoteza fahamu kwa siku tatu.

Nilianza kuthamini uhai, hata hivyo nikawa mkatili na mwenye hila. Nilijitolea kufanya ngono na watu, niliwalewesha kwa dawa za kulevya nyumbani kwao, na kisha kuwaibia vitu vyao vya thamani. Nilitumiwa na wahalifu wakubwa kufanya biashara ya dawa za kulevya nchini Italia. Nilikamatwa na polisi mara nyingi. Ijapokuwa nilikosa mwelekeo maishani bado niliamini kwamba niliumbwa kwa kusudi fulani. Nilimwomba Mungu anipatie amani na furaha kwa mwaka mmoja tu.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Nilihamia Uingereza nilipokuwa na umri wa miaka 24. Kwa kuwa nilishirikiana na walanguzi wa dawa za kulevya, maisha yangu yalikuwa hatarini. Kabla ya kuhamia Uingereza, nilimtembelea mama yangu na nilishangaa kumkuta akifundishwa Biblia na mwanamume anayeitwa Annunziato Lugarà. * Niliogopa sana nilipomwona kwa kuwa nilijua alikuwa mhalifu. Aliniambia kuhusu mabadiliko makubwa aliyofanya maishani mwake ili awe Shahidi wa Yehova, na alinisihi nizungumze na Mashahidi nitakapohamia Uingereza. Nilikubali kufanya hivyo. Hata hivyo, nilipohamia huko, niliendelea na maisha yangu.

Siku moja nilikutana na Shahidi aliyekuwa akihubiri na kuwaachia watu magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! katika mtaa mmoja wenye shughuli nyingi jijini London. Ili kutimiza ahadi niliyompa Annunziato, nilimwomba Shahidi huyo anifundishe Biblia.

Nilishangazwa sana na mafundisho ya Biblia. Kwa mfano, niliguswa sana na maneno ya 1 Yohana 1:9 yanayosema: “Tukiungama dhambi zetu, yeye ni mwaminifu na mwadilifu hata atusamehe dhambi zetu na kutusafisha.” Mstari huo ulinigusa sana kwa kuwa nilijiona kuwa mchafu kutokana na maisha niliyoishi. Nilianza mara moja kuhudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Mashahidi walinikaribisha kwa uchangamfu. Nilipoona jinsi walivyo na urafiki wa karibu, nilitaka sana kuwa miongoni mwa washiriki wa kutaniko lililo kama familia kwa kuwa hilo ni jambo ambalo nilitamani kwa muda mrefu.

Ijapokuwa niliweza kuacha mara moja maisha mapotovu na kutumia dawa za kulevya, ilikuwa vigumu sana kwangu kurekebisha utu wangu. Niligundua kwamba nilihitaji kuwafikiria na kuwatendea watu kwa heshima. Kwa kweli, bado napambana ili kuacha tabia fulani zisizofaa. Pamoja na hayo, Yehova amenisaidia kufanya maendeleo. Nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova miezi sita baada ya kuanza kujifunza Biblia. Huo ulikuwa mwaka wa 1997.

JINSI NILIVYOFAIDIKA:

Baada ya kubatizwa, nilifunga ndoa na mwanamke anayeitwa Barbara aliyekuwa pia ametoka tu kubatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Rafiki yangu mmoja alipoona jinsi nilivyofanya mabadiliko makubwa maishani, alianza pia kujifunza Biblia. Baada ya muda, yeye na dada yake wakawa Mashahidi. Pia, dada ya bibi yangu, aliyekuwa na umri wa miaka zaidi ya 80, alianza kujifunza na akabatizwa kabla ya kifo chake.

Sasa ninatumikia nikiwa mzee katika kutaniko, pia mimi na mke wangu tunatumikia tukiwa wahudumu wa wakati wote tukiwafundisha Biblia wanaozungumza Kiitaliano katika jiji la London. Wakati mwingine mimi huhuzunika sana ninapokumbuka maisha mapotovu niliyoishi, hata hivyo, Barbara amekuwa msaada mkubwa sana kwangu. Hatimaye sasa nina Baba mwenye upendo na maisha bora ya familia niliyotamani sana. Nilimwomba Mungu anipe amani na furaha kwa mwaka mmoja tu, lakini amenipa mengi zaidi!

Hatimaye sasa nina Baba mwenye upendo na maisha bora ya familia niliyotamani sana

^ fu. 10 Tazama makala “Biblia Inabadili Maisha—Nilitembea na Bunduki Kila Wakati,” na usome simulizi la Annunziato Lugarà, katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 2014, ukurasa wa 8-9.