Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jina Tattannu linapatikana katika bamba hili la maandishi ya kikabari

Uthibitisho Mwingine

Uthibitisho Mwingine

Je, kuna uthibitisho wa vitu vya kale vilivyochimbuliwa unaounga mkono masimulizi ya Biblia? Katika mwaka wa 2014, makala moja katika gazeti Biblical Archaeology Review ilikuwa na swali: “Ni watu wangapi wanaotajwa katika Biblia ambao wachimbuzi wa vitu vya kale wamethibitisha kuwa walikuwepo?” Jibu: “Angalau watu 50!” Mtu mmoja ambaye hakutajwa kwenye orodha hiyo ni Tatenai. Tatenai alikuwa nani? Acheni tuchunguze kifupi cheo chake kama kinavyoelezwa katika Biblia.

Wakati fulani, Yerusalemu lilikuwa sehemu ya Milki ya Waajemi. Jiji la Yerusalemu lilikuwa katika eneo ambalo Waajemi waliliita Ng’ambo ya Mto, yaani, magharibi mwa mto Efrati. Baada ya kushinda Babiloni, Waajemi waliwaachilia huru Wayahudi waliokuwa utekwani na wakawaamuru wajenge upya hekalu la Yehova huko Yerusalemu. (Ezra 1:1-4) Hata hivyo, maadui wa Wayahudi walipinga mradi huo na wakawachongea Wayahudi kwamba walikuwa wakiasi utawala wa Waajemi. (Ezra 4:4-16) Wakati wa utawala wa Dario 1 (522-486 K.W.K.), ofisa Mwajemi aliyeitwa Tatenai aliongoza uchunguzi wa madai hayo. Biblia inamwita “gavana wa Ng’ambo ya Mto.”—Ezra 5:3-7.

Mabamba kadhaa yenye maandishi ya kikabari yaliyo na jina Tatenai yamepatikana katika kile kinachoaminika kuwa rekodi za kibiashara za familia ya Tatenai na watumishi wake. Bamba linalomhusianisha mshiriki mmoja wa familia hii na yule anayetajwa katika Biblia ni hati ya kifedha ya mwaka wa 20 wa Dario 1, yaani, mwaka wa 502 K.W.K. Mtu aliyekuwa shahidi katika makubaliano hayo anatajwa kuwa mtumishi wa “Tattannu, gavana wa eneo lililo Ng’ambo ya Mto” yaani, Tatenai, mwanaume yuleyule anayetajwa kwenye Biblia katika kitabu cha Ezra.

Mwanamume huyo alikuwa na cheo gani? Katika mwaka wa 535 K.W.K., Koreshi Mkuu aligawanya milki zake katika wilaya, na moja ya wilaya hizo iliitwa “Babiloni na Ng’ambo-ya-Mto.” Baadaye, wilaya hiyo iligawanywa mara mbili, na moja ikaitwa Ng’ambo ya Mto. Ilitia ndani, Foinike, Koele-Siria, Samaria na Yuda, na huenda makao yake makuu yalikuwa Damasko. Tatenai alikuwa gavana wa wilaya hiyo kuanzia mwaka wa 520 hadi 502 K.W.K.

Baada ya kusafiri Yerusalemu kuchunguza mashtaka hayo ya uasi, Tatenai aliripoti kwa Dario kuwa Wayahudi walidai kwamba waliruhusiwa na Koreshi kujenga upya hekalu la Yehova. Uchunguzi uliofanywa katika hifadhi ya vitu vya kifalme ulithibitisha kwamba dai hilo lilikuwa la kweli. (Ezra 5:6, 7, 11-13; 6:1-3) Hivyo, Tatenai akaagizwa kutoingilia mradi huo, naye akatii.—Ezra 6:6, 7, 13.

Kwa hakika, “Tatenai, gavana wa eneo lililo Ng’ambo ya Mto” hakufanya jambo linalojulikana sana kihistoria. Hata hivyo, Maandiko yanamtaja na kueleza cheo chake halisi. Jambo hilo linatupatia uthibitisho mwingine kuwa vitu vya kale vilivyochimbuliwa vinaunga mkono kwamba Biblia ni sahihi kihistoria.